Tuesday 12 January 2016

NDUGAI ATEUA 15 KAMATI YA KANUNI





SPIKA wa Bunge, Job Ndugai, amewateua wabunge 15 kwenye Kamati ya Kudumu ya Kanuni za Bunge, itakayokuwa na jukumu la kufanyia marekebisho ya nyongeza ya nane ya kanuni za kudumu za bunge.

Pia, kamati hiyo itakuwa na jukumu la kuaninisha majukumu ya kamati zingine za bunge na serikali kwa kuzingatia muundo wa baraza la mawazili lililopo.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Ofisi ya Bunge, kamati hiyo itaongozwa na Spika, ambaye ni Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti wake ni Naibu Spika, Dk. Tulia Atson pamoja na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Geogre Masaju na kiongozi wa kambi ya upinzani.

Wajumbe wengine ni Makame Kassim Makame, Mbunge Jimbo la  Mwera, Tundu Lissu, Mbunge wa Jimbo la Singida Mashariki, Jasson Rweikiza, Mbunge wa Jimbo la Bukoba Vijijini, Dk. Charles Tizeba, Mbunge wa Jimbo la Buchosa na Ally Saleh Ally, Mbunge wa Jimbo la Malindi.

Wengine ni Magdalena Sakaya, Mbunge wa Jimbo la Kaliua, Salome Makamba, Mbunge wa  Viti Maalumu, Dk. Jasmine Bunga, Mbunge wa  Viti Maalumu,  Zainab  Katimba, Mbunge Viti Maalumu, Balozi Adadi Rajab, Mbunge wa Jimbo la Muheza pamoja na Kangi Lugola, ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Mwibara.

Aidha, taarifa hiyo imeeleza kuwa, Spika atakamilisha uteuzi wa wajumbe katika kamati zingine za Bunge kabla ya kuanza kwa mkutano wa pili wa bunge, Januari 26, mwaka huu, ili kutoa fursa kwa kamati zote kuchagua viongozi wake na kuandaa mpango kazi kwa mwaka 2016/17.

Kwa mujibu wa Kanuni ya 116 (3) ya Kanuni za Kudumu za Bunge, Toleo la Aprili, 2013, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano amepewa mamlaka ya kuteua wajumbe wa Kamati za Kudumu za Bunge kwa namna, ambayo itawezesha kila mbunge kuwekwa kwenye kamati mojawapo.

No comments:

Post a Comment