Saturday 4 February 2017

SIMULIZI ZA SIKU YA KUZALIWA KWA CHAMA CHA MAPINDUZI


                                                                                                            Yaliyojiri siku ya tarehe 5 Februari, 1977. 

Na Pius  Msekwa.

Sababu  ya  CCM  kuzaliwa  tarehe  5 Februari.
Wakati wa uhai wa Vyama vya siasa vya TANU (kwa upande wa Tanzania Bara), na  ASP  (kwa upande wa Zanzibar);  Tarehe  5  Februari  ya kila mwaka ilikuwa ni siku maalum  ya kumbu kumbu  za matukio  muhimu  kwa upande wa kila Chama.  

Kwa upande wa TANU, tarehe hiyo ilikuwa ni siku ya kuadhimisha  kuzaliwa  kwa  Azimio  la Arusha,  ambalo  liliainisha Itikadi  ya Chama hicho,  ya Ujamaa na Kujitegemea; na kwa upande wa  Afro-Shirazi  Party, siku  ilikuwa  ni siku ya  kuadhimisha  kuzaliwa  kwa  Chama hicho  cha  ASP. 

Napenda  vile vile  kuendelea kuweka wazi  kwamba  hiyo  ndiyo  ilikuwa  ni  sababu  peke yake  iliyoifanya ile Tume   iliyokuwa  ikiitwa  ‘Tume ya Watu  Ishirini’, (ambayo ilikuwa imepewa kazi ya kufanya  maandalizi ya kuzaliwa kwa Chama cha Mapinduzi)  kuichagua na kupendekeza  tarehe hiyo kuwa  ndiyo tahehe ya kuzaliwa CCM.  Pendekezo  liikubaliwa na vikao husika, na ndiyo sababu Chama cha Mapinduzi kilizaliwa tarehe  5 Februari, 1977.

Matukio  ya siku  ya  kuzaliwa  CCM.

Ndiyo sababu kulikuwa na jumla ya sherehe tatu  siku  hiyo, ambapo  sherehe  mbili  zilitangulia sherehe kubwa  ya kuzaliwa kwa CCM.  Sherehe ya kwanza  ilifanyika  majira  ya  asubuhi,  katika  Uwanja  wa Sheikh  Amri Abedi  mjini Arusha, ikiwa na lengo la  kuadhimisha  miaka kumi ya uhai wa  Azimio la Arusha, ambalo lilizaliwa hapo  hapo  Arusha  tarehe  5 Februari, 1967.Sherehe ya pili ilifanyika  majira ya mchana  katika Uwanja  wa Amani  mjini Zanzibar, ikiwa na lengo  la kuadhimisha kuzaliwa  kwa  Afro-Shirazi  Party.  Sherehe ya tatu ndiyo hiyo ya kuzaliwa kwa Chama cha Mapinduzi (CCM), ambayo   ilifanyika  majira ya  jioni,  katika Uwanja  huo  huo  wa  Amani,  mjini  Zanzibar. 


Yaliyomsibu  Mwalimu  Nyerere siku  hiyo.

Kuna mambo  mawili  yasiyotegemewa, yaliyomsibu  Mwalimu Nyerere   siku hiyo.                                                La kwanza, lilikuwa  ni  madhara  ya kiafya aliyoyapata kutokana na kula samaki aina ya  prawns  wakati wa chakula cha mchana   huko  Arusha. Kwani  kufuatia kumalizika kwa  maadhimisho  ya  miaka  kumi ya  uhai  wa  Azimio la Arusha, ilikuwa imeandaliwa  hafla  ya chakula cha  mchana  katika  hoteli  ya  Mount  Meru, kwa ajili ya wageni mashuhuri  walioalikwa  kuhudhuria  maadhimisho  hayo,  ikiwa ni pamoja na Mwalimu Julius Nyerere.  

Miongoni mwa vyakula vingi na vya aina mbali mbali vilivyokuwapo,  palikuwapo  vile vile  na samaki   aina  ya  prawns.   Mwalimu Nyerere  ni  miongoni mwa wale waliochagua  samaki  hao,  ambao   kumbe  walikuwa tayari  wameanza  kuchina,  lakini hakuna aliyegundua jambo hilo mapema.  

Baada ya hapo, Mwalimu Nyerere akaendelea na safari  yake ya  kwenda  kwenye  sherehe  kubwa   za  kule  Zanzibar, za kuadhimisha  kuzaliwa kwa CCM. Sherehe hizo zilimalizika  vizuri kabisa, na hatimaye  Mwalimu   Nyerere  akaenda  zake  kulala  katika hoteli  ya  Bwawani  alikokuwa  amepangiwa.  

 Usiku  ule, ndipo  yakatokea hayo mambo mawili yaliyomsibu Mwalimu  Nyerere,  na  kumnyima  raha ya  usingizi.    La kwanza  lilikuwa ni milio mikubwa na mingi sana  ya fataki, au  fash fash,  ilipofika saa sita usiku. 

Alivyotusimulia  yeye  mwenyewe  baadaye, ni  kwamba  kabla ya hapo, alikuwa amesikia minong’ono ya kwamba  kulikuwa  na  maadui  fulani  ambao  eti  walikuwa  wamepanga  kuipindua  Serikali  ya Zanzibar  usiku huo. 

Kwa kuwa yeye hakuwa ameelezwa juu ya mpango wa  fash fash  hizo  za saa sita usiku,  basi akadhani   kuwa  ilikuwa ni milio ya bunduki, yaani kwamba  hao maadui walikuwa  wametekeleza  nia  yao  hiyo.  Kwa hiyo akaamka, akavaa  nguo akiwa  gizani kwani aliogopa  hata  kuwasha  taa,  na baada ya  hapo, akakaa  tu  akisubiri  kuokolewa na walinzi wake.  

Ndipo  alipopigiwa simu na mkuu wa walinzi hao, kumjulisha  kuwa  hapakuwa  na  hatari yoyote, ilikuwa  ni  fash fash  tu   za  sherehe.   Akashukuru, na  kurudi   kulala.  

Ndipo  madhara ya pili kwake  yakatokea.  Kwani   ilipofika majira ya saa kumi na  moja  alfajiri, suala  la kuwa  alikula  prawns  waliokuwa  wamechina  wakati  wa  chakula cha  mchana  kule  Arusha, likaanza  kumuadhibu.   Alianza  kuharisha  mfululizo  hadi  akajisikia  amedhoofika  sana.   

Matokeo yake yalikuwa kwamba alishiindwa kuondoka Zan zibar kurejea  DaresSalaa  majira ya asubuhi,  kama alivyokuwa amepangwa.  Ilibidi asubiri mpaka  majira ya mchana,  hali yake ilipomruhusu kuondoka. 

Kwa hakika, usiku wa tarehe 5 Februari 1977, haukuwa  mzuri kwa  Mwalimu Nyerere, Mwenyekiti mpya wa Chama kipya cha Mapinduzi, kilichokuwa  kimezinduliwa  muda mfupi  tu  kabla ya hapo,  yaani  jioni  tu  ya  siku  ya  jana   yake.

Wakati  wana-CCM  wengi  wengine  wakiwa  katika furaha tele  ya kuzaliwa  kwa  Chama  chao  kipya, kumbe Mwenyekiti wao Mwalimu Nyerere  alikuwa  katika  matatizo  hayo  makubwa  yaliyomsibu.

No comments:

Post a Comment