![]() |
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NIDA, Dk. Modestus Kipilimba |
MAMLAKA ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), imetangaza
kusitisha mikataba ya wafanyakazi 597, katika ofisi zake nchi nzima kutokana na
kutokuwa na ufanisi.
Wafanyakazi hao ni wale walioajiriwa kwa ajira za
mikataba huku ikitangaza kuanza kuwachunguza watumishi wake wengine 802, ambao
ajira zao ni za kudumu.
Hatua hiyo inalenga kuikwamua mamlaka hiyo kuondokana
na mzigo mzito wa kuwalipa watumishi, ambao ni wengi kuliko idadi halisi
inayohitajika katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku kuwahudumia
Watanzania.
Pia, NIDA imetangaza kuchunguza mikataba yote, ambayo
mamlaka imeingia na kampuni ama watu binafsi, kuona iwapo ina tija na
itakayobainika kuwa ya kinyonyaji, itavunjwa mara moja.
Kufutwa kazi kwa watumishi hao ni mwendelezo wa hatua
za kuisafisha NIDA, zinazochukuliwa na serikali ya Rais Dk. John Magufuli,
ambapo tayari alishamng’oa Mkurugenzi Mkuu wake, Dickson Maimu.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dar es
Salaam, jana, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NIDA, Dk. Modestus Kipilimba, alisema
idadi ya watumishi iliyopo haiendani na uzalishaji wa vitambulisho, ambavyo
vinatakiwa kutengenezwa.
Amesema kuwa NIDA ina jumla ya wafanyakazi 1,399,
wakiwemo wa kudumu na mikataba, lakini vitambulisho inavyozalisha kwa siku ni 1,200
tu badala ya 24, 000.
Kutokana na hali hiyo, Dk. Kipilimbi alisema uongozi
umelazimika kuchukua uamuzi mgumu wa kusitisha mara moja ajira zote 597, za
mikataba kwa kuanzia na baadaye itachunguza zaidi watumishi waliobaki.
“Nina muda mfupi sana tangu nimepewa kukaimu nafasi
hii, lakini nimegundua mambo mengi ambayo hayako sawa hapa NIDA. Tuna
wafanyakazi wa mikataba 597 na wa kudumu 802, lakini tunazalisha vitambulisho
1,200 kwa siku wakati idadi halisi tunayotakiwa kuzalisha ni 24,000.
“Hili ni tatizo kubwa, huwezi kuwa na idadi kubwa ya
watumishi kuliko bidhaa unayozalisha, sasa tumeona tuanze na hawa 597 na
tutakuja kwa hawa wengine kuona kama uwepo wao una tija kwa mamlaka.
“Ukiangalia utaona hakuna ufanisi kabisa, yaani ni
sawa na kila mfanyakazi kuzalisha kitambulisho kimoja kwa siku,” alisema Dk.
Kipilimbi, ambaye alikabidhiwa nafasi hiyo Febrauri 15, mwaka huu, baada ya
Maimu kutumbuliwa jipu.
Alisema kusitishwa kwa mikataba hiyo kutatoa fursa
kwa mamlaka kujipanga upya ili iweze kufanya kazi zake kwa ufanisi na kufikia
malengo, ambayo serikali na Watanzania wanayatarajia.
Alisema malengo ya NIDA ni kuhakikisha Watanzania
wote wanapata vitambulisho na kwamba, kasi ya kutoa vitambulisho itaongezwa
maradufu.
Aliongeza kuwa anataka kuona kila mtumishi ndani ya
NIDA analipwa kulingana na kazi anayoifanya na kwamba, wasiostahili
wataondolewa haraka.
“Hawa wafanyakazi wenye mikataba ya kudumu
tutawangalia kwa umakini mkubwa kubaini kama wanastahili kuendelea kuwepo ama
kuondolewa.
“Tukibaini kuna watumishi ambao hawastahili kuwepo
hapa, tutawarudisha utumishi huko watafahamu ni wapi kwa kuwapeleka. Tunataka
kufanya kazi na tutakuwa tayari kuwa na watu wanaofanya kazi.
“Tunapenda watu wawe na ajira, lakini kama huzalishi
inavyotakiwa, huna sababu ya kuwepo…tutaendelea kuhakiki hadi hapo
tutakapojiridhisha,” alisema.
Kuhusu uboreshaji wa huduma zake, alisema NIDA
inatarajia kupata mashine 3,000 kutoka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), ambazo
kwa sasa zinafanyiwa marekebisho ili kuongeza kasi ya utoaji wa vitambulisho.
Aidha, alisema uhakiki utakwenda sambamba na kupunguza
gharama kwa kubaki na watumishi wachache na kufunga ofisi zake katika maeneo
mbalimbali ili kuanza kushirikiana na halmashauri nchini.
Alisema hakuna sababu ya kuwa na ofisi nyingi
zilizotapakaa kila mahali na kwamba, maofisa wake watakuwa na ofisi kwenye
majengo ya halmashauri nchini, ambako shughuli zote zitafanyika huko kama
kawaida.
Mikataba
mibovu
Kuhusu mikataba mbalimbali, Dk. Kipilimbi alisema
NIDA imeingia mikataba mingi na mingine ni mikubwa, hivyo ni lazima
kujiridhisha iwapo yote ina tija na maslahi kwa mamlaka.
Alisema uchunguzi na uhakiki wa mikataba hiyo utaanza
mara moja na kwamba, itakayobainika inainyonya mamlaka, itafanyiwa marekebisho
ama kuvunjwa kabisa.
“Mamlaka imeingia mikataba mingi ambayo ni lazima
tujiridhishe kama iko sawa, sasa tukibaini haina tija kwetu, tunaomba ushauri
wa kisheria kwa mamlaka zingine ili kuondokana nayo haraka,” alisema.
Hata hivyo, mikataba ambayo huenda ikaibua majipu ni
ile, ambayo NIDA imeingia kukodisha majengo kwa ajili ya ofisi zake katika
maeneo mbalimbali nchini.
Miongoni mwa majengo hayo yapo maghorofa ambayo
yanatumika kama ofisi za NIDA, yanayotajwa kumilikiwa na vigogo, wakiwemo
wanasiasa, yanayogharimu mamilioni ya shilingi kama kodi ya pango.
Sahihi
za vitambulisho
Kuhusu vitambulisho vingi kutokuwa na sahihi, Dk.
Kipilimbi alisema hilo linaendelea kufanyiwa kazi na kwamba, vitaboreshwa zaidi
na kwamba kwa sasa vinaweza kuendelea kutumika kwa waliokwishachukua.
Alisema vitambulisho vitakavyoanza kutolewa kwa sasa
vitakuwa na sahihi ya mtoaji na mmiliki na kuwa, vilivyokwishatolewa vitarudishwa
na wahusika kupewa vingine vya kisasa.
“Vitambulisho vipya vitakuwa na sahihi ya mmiliki na
mtoaji, hivyo wananchi wasiwe na shaka kabisa…kwa waliokwishachukua tutaandaa
utaratibu wa kuvikusanya na kuwapatia vingine. “Hili tutatangaza, lakini kwa sasa
wanaweza kuendelea kutumia walivyonavyo kwa kuwa vinatambulika kisheria,
wasifanye haraka,” alisema.
No comments:
Post a Comment