Thursday 16 March 2017

MAHAKAMA YASHANGAA UPELELEZI KESI YA RWAKATARE KUCHUKUA MIAKA MITATU




MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, imesema kinachoendelea katika kesi inayomkabili Mkurugenzi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Wilfred Lwakatare na mwenzake ni maajabu matupu kutokana na upelelezi kuchukua miaka mitatu bila kukamilika.

Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba, alisema hayo jana, mahakamani hapo, baada ya Mwendesha Mashitaka, Inspekta Hamis Said, kudai upelelezi haujakamilika.

Baada ya Mwendesha Mashitaka huyo kudai hayo, Hakimu Simba alitaka kujua maendeleo ya kesi hiyo, ambapo mwendesha mashitaka alidai wapelelezi wanakamilisha mambo madogo madogo.

“Kinachoendelea ni maajabu matupu. Kesi ililetwa kwa mara ya kwanza Mei 20, 2013, mpaka leo imekuwa ikiahirishwa mara ngapi?

“Kama kuachiwa, waachiwe na kama wanafungwa wafungwe, haipendezi miaka mitatu. Ikija mara nyingine, nakuja kuwaachia washitakiwa wenu, hii sio haki,” alisema.

Awali, mdhamini wa Lwakatare, ambaye hakuwepo mahakamani hapo, aliieleza mahakama kwamba, amelazwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.

Kutokana na hilo, Hakimu Simba alimueleza mdhamini huyo kumpelekea tarehe ya kufika mahakamani, ambayo ni Aprili 12, mwaka huu.

Kwa mujibu wa hati ya mashitaka, Lwakatare na Ludovick Joseph wanadaiwa Desemba 28, mwaka 2013, katika eneo la King’ong’o, Kinondoni, Dar es Salaam, walikula njama za kutoa sumu kwa nia ya kumdhuru aliyekuwa Mhariri wa Gazeti la Mwananchi, Dennis Msacky.

No comments:

Post a Comment