Wednesday 30 August 2017

MAMBOSASA: NATAKA DAR ISIYO NA UHALIFU


KAMISHNA  Msaidizi Mwandamizi wa  Polisi  Kanda  Maalumu ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa, amesema hataki kuona  jiji hilo  likiwa ni  sehemu ya maficho kwa wahalifu  kukimbilia na kujiona wako salama.

Pia, amewataka wananchi  kuhakikisha wanatoa ushirikiano  kwa polisi  ili kuibua matukio ya kiuhalifu yanayozuia maendeleo yao.

Alitoa tamko hilo Dar es Salaam, jana, wakati alipokuwa akijitambulisha kwa waandishi wa habari  na kuelezea mikakati  yake  baada ya kuteuliwa  kuiongoza  kanda hiyo.

Mambosasa alisema yupo  kwa ajili ya  kupambana na  uhalifu  na  kutengeneza  mazingira  rafiki kwa wananchi  kwa ajili ya kuondoa kero  zinazozuia maendeleo kutokana na usumbufu  wa wahalifu.

"Taarifa za uhalifu kwangu ni  mtaji  na  ndizo zinazoniwezesha kufanyakazi vizuri. Hatutaki kuona  Dar es Salaam, inakuwa  maficho yao kwani tutawakamata  kabla hawajafika waendako na wahakikishe wanatafuta
mkoa mwingine  wa kwendakufanya uhalifu, siyo hapa," alisema.

Kamishna huyo, aliitaja mikakati  aliyonayo katika kupambana na kudhibiti uhalifu kuwa ni  kuhakikisha  kila mwananchi anafanya shughuli za  maendeleo  pasipo kusumbuliwa .

Pia, alisema amepanga kushirikiana na  vyombo vya ulinzi  na usalama  kuanzia kamati za mitaa, kata na hadi mkoa.

Aliwataka wananchi kuhakikisha  kila  mtu anakuwa mlinzi kwa mwenzake, kutokukubali kukaa na wahalifu na kutokuwa sehemu ya uhalifu.

Katika  hatua  nyingine, Mambosasa alisema hayuko  tayari kuona uhuru wa mtu ukichezewa na askari  kwa  kuwanyanyasa  wananchi.

"Mara nyingi polisi wamekuwa wakikamata mtu na kusema ni  amri kutoka juu. Kwangu mimi  ukisikia hivyo, kata rufani kwa sababu polisi huwa anafanyakazi kwa kufuata sheria," alisema.

Wakati huo huo, Kamishna huyo alizungumzia kuhusiana na  tukio  la  kuungua kwa kampuni  ya  mawakili na  kusema kuwa, polisi bado wanaendelea kufanya upelelezi.

Alisema tatizo ni baadhi ya watu kuchukulia  tatizo hilo na kuliingiza katika masuala ya kisiasa.

"Tambueni  matukio kama hayo, hasa  yanayoashiria kuwepo na mlipuko wa bomu, lazima tufanye uchunguzi wa kikemikali ili kubaini aina ya mlipuko na kuja kuutolea ufafanuzi, siyo jambo la haraka haraka," alisema.

Aliwataka wananchi kutokurupuka kutoa taarifa za masuala ya uchunguzi, bali waviachie vyombo sahihi, hasa vya usalama kufanyakazi yake.

No comments:

Post a Comment