Thursday 24 March 2016

KAMATI YA BUNGE YAIWEKA KIPORO UDA




KAMATI ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) , imesitisha kujadili suala la Shirika la Usafiri  Dar es Salaam (UDA) na Kiwanda cha Nyama cha East Afrika Meat (EAMEATCO), baada ya Makamu Mwenyekiti wa awali, Kangi Lugola kutokuwepo kwenye kikao.

Lugora ni miongoni mwa wabunge walioondolewa kwenye kamati hiyo, wakisubiri uchunguzi wa tuhuma za rushwa zinazozikabili kamati mbalimbali za Bunge .

Pia, hoja hizo zimeshindwa kujadiliwa  kutokana na ugeni wa Meya wa Jiji, aliyechaguliwa juzi, hivyo hajui chochote kuhusu  sakata hilo.

Akizungumza jana, Dar es  Salam, Kaimu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Abdallah Chikota, alisema kutokana na unyeti wa suala hilo, kamati yake haitaweza kuendelea kusikiliza hoja kuhusiana na miradi hiyo muhimu kwa jamii.

Mbali na kuahirisha kikao hicho, Chikota, ambaye ni mbunge wa jimbo la Nanyamba, alisema kamati hiyo imeazimia kutoa maagizo mawili kwa serikali, ikiwemo kurejesha kiwanda cha nyama kwa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, ili iwe mali yake na kuacha kujadili hoja yoyote ili wajumbe wapate taarifa za kutosha.

“Ni lazima tupange siku maalumu, hata kama ni Jumamosi ili suala la kiwanda cha nyama na UDA lifike mwisho kwani limekuwa bughudha katika kamati,”alisema Chikota.

Kwa upande wake, Waziri wa  Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na  Serikali za Mitaa (OR- TAMISEMI), George Simbachawene, aliipongeza kamati kwa uamuzi huo kwa kuwa utaleta maslahi kwa jamii.

Alisema muda walioutoa utasaidia wajumbe hao kutoa taarifa za kina kutokana na unyeti wa suala hilo, hasa kiwanda cha nyama.

“Sisi wenyewe tumechoshwa na hizi hoja, tunahitaji kufahamu kwa kina suala hili kwa sababu lina wadau wengi. Ifike wakati tuite wadau wote ili kila mmoja aelezee mtazamo wake na athari zake, kwa kuwa zinagusa maisha ya kila mmoja na hisa za wawekezaji,”alisema  Simbachawene.

Aliongeza kuwa ana imani kwa mfumo huo, watalitekeleza suala hilo kwa usahihi bila kuleta athari yoyote.

Naye Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita, alisema hana chochote anachokifahamu kuhusiana na mjadala uliopo mbele ya kamati hiyo na kwamba, hatakuwa tayari kuzungumzia suala hilo.

No comments:

Post a Comment