Tuesday 3 November 2015

MCHAKATO KURA ZA MAONI CCM HANDENI KURUDIWA, NCHIMBI, BULEMBO, MAUA DAFTARI KUSIMAMIA




NA MWANDISHI WETU
KAMATI Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), imeamua kurudiwa kwa mchakato wa kura za maoni katika jimbo la Handeni mkoani Tanga.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Ofisi Ndogo za Chama, Lumumba mjini Dar es Salaam, Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema uchaguzi huo, unarudiwa leo, chini ya wasimamizi Maua Abeid Daftari, Dk. Emmanuel Nchimbi na Abdalla Bulembo.
Nape alisema uamuzi huo ulitolewa jana na kikao cha Kamati Kuu, chini ya mwenyekiti wake, Rais Jakaya Kikwete.
Alisema kikao hicho kilikuwa maalumu kwa ajenda maalumu, ambapo pamoja na mambo mengine, kilijadili majimbo ambayo hayakufanya uchaguzi kwa sababu mbalimbali.
Nape alisema mchakato wa kumpata mgombea katika jimbo la Handeni, ulikamilika lakini hakuna mgombea aliyepata kura za kuridhisha.
Alisema kutokana na hali hiyo, Kamati Kuu, imeamua uchaguzi wa kura za maoni urudiwe na kwamba wagombea wawili ndio watapigiwa kura katika uchaguzi huo.
Nape aliwataja wagombea hao kuwa ni pamoja na Omari Kigoda na Khamis Mnondwa, ambao walipata kura za juu.
Hata hivyo, alisema kuwa mtoto wa kiongozi si hoja ya kukosa sifa ya kugombea kwani, nafasi ya ubunge inatangazwa hivyo kila Mtanzania mwenye sifa anayo haki ya kugombea.
Uchaguzi wa Jimbo la Handeni, unarudiwa kufuatia kifo cha aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Dk. Abdalah Kigoda, kilichotokea nchini India, alikokuwa amelazwa kwa matibabu.
Dk. Kigoda ambaye pia alikuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, alifariki dunia Oktoba 12, mwaka huu.

No comments:

Post a Comment