Tuesday 3 November 2015

WANASIASA WAZIPASHA NCHI ZINAZOINGILIA ZANZIBAR


MWENYEKITI wa  Taifa  wa Chama cha  (AFD),  Said Soud Said, akifafanua jambo kwa wandishi wa habari wakati wa mkutano huo.


NA WILLIAM SHECHAMBO
VIONGOZI na wawakilishi wa vyama vya siasa hapa nchini, wamezitaka nchi wadau wa maendeleo kuacha kuliingilia suala la kurudiwa kwa uchaguzi mkuu wa Rais na wawakilishi visiwani Zanzibar.
Wamesema ni ukweli usiopingika kuwa kuna uzembe mkubwa uliofanywa na Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), katika kusimamia uchaguzi huo, uliofanyika Oktoba 25, mwaka huu, hivyo kusababisha kutokuwa huru na haki.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na UHURU, Dar es Salaam, jana, wanasiasa hao waliokuwa kwenye maandalizi ya hafla itakayofanyika leo ya kumuaga Rais Jakaya Kikwete, walisema hali iliyoko Zanzibar itatulizwa na Watanzania wenyewe.
Walisema Rais Kikwete ana uwezo mkubwa wa busara ambayo awali ilisaidia kuleta amani visiwani humo kwa kuwaleta pamoja viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na CUF ili washirikiane kuongoza dola.
“Hakuna haja na mtu mwingine kuingilia suala hili, Rais Kikwete ana busara sana, tunaamini ataweza kulitatua kwa falsafa na busara aliyoitumia kipindi kile cha kuwapatanisha Maalim Seif na Aman Karume. Kitendo cha hawa wenzetu kuleta maneno mengi kutavuruga zaidi mambo,” alisema Juma Ali Hatib.
Hatib, ambaye ni mgombea urais wa Zanzibar kwa tiketi ya ADA-TADEA na Makamu wa Rais wa chama hicho Taifa, alisema kuwa hali iliyoko Zanzibar inazidi kuwa mbaya kwa maisha ya watu kutokana na kupanda kwa gharama za maisha.
“Wiki mbili zilizopita, gunia la viazi mbatata Zanzibar lilikuwa sh. 100,000, leo hii nazungumza na wewe ni sh. 250,000 na hii ni kwa sababu boti kutoka bara zinaenda mbili tu kwa siku wakiogopa usalama,” alisema.
Alisema jinsi siku zinavyozidi kwenda, ndivyo mambo yanavyozidi kuwa magumu kwa wananchi, hivyo umefika wakati wa Rais Kikwete kulivalia njuga suala hilo ili uchaguzi huo ufanyike tena kwa uangalifu tofauti na awali.
Said Sudi Said, ambaye ni Mwenyekiti wa AFP Taifa, alisema hakuna sababu ya nchi wahisani kuingilia suala la Zanzibar kwa kuwa siku chache zijazo mambo yatarudi kama yalivyokuwa awali.
Alisema kinachotakiwa kufanyika ni kuundwa kwa serikali ya mpito, ambayo itasubiri kurudiwa kwa uchaguzi mkuu ambao utamruhusu rais kupewa madaraka yake kikatiba.
“Tunajua katiba haisemi kuwepo kwa serikali ya mpito, ila ninashauri wakubaliane iwepo kwa siku hizo za kusubiri uchaguzi ufanyike tena ili kuepusha zogo la kisiasa,” alisema.
Aidha, alimshauri mgombea urais wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, kupunguza jazba na kusubiri uchaguzi urudiwe ili haki itendeke kwa anayestahili.

No comments:

Post a Comment