Thursday 7 January 2016

PROFESA MUHONGO AWATAKA WATENDAJI KUBADILIKA




WAZIRI wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, amewataka watendaji  wa wizara na wakuu wa taasisi zilizo chini yake, kukubali kubadilika kwa kufanyakazi kwa bidii.
Amesema watendaji hao wanapaswa kuhakikisha kuwa sekta  za nishati na madini zinakuwa na manufaa makubwa kwa taifa, ikiwemo mabadiliko kiuchumi.
Profesa Muhongo aliyasema hayo juzi, mjini Dar es Salaam, wakati wa kikao cha utambulisho wa viongozi wapya wa wizara.
Kikao hicho kilihusisha menejimenti ya wizara, taasisi zilizo chini yake, zikiwemo Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Shirika la Maendeleo ya Petroli la Tanzania (TPDC), Wakala wa Ukaguzi wa Madini (TMAA), Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST), Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Chuo cha Madini Dodoma (MRI) na watendaji kutoka Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC).
“Ni lazima tujitume. Hili ndilo jukumu letu la kwanza. Wananchi wanataka umeme na wanataka mabadiliko kupitia sekta za nishati na madini.
“Pia tunatakiwa tufanyekazi kwa umoja na uwazi kwa sababu tumepewa fursa ya kuwatumikia wananchi hivyo ni lazima tubadilike na mabadiliko ni lazima. Asiyeweza kuendana na kasi ya awamu hii aondoke, hakuna atakayeonewa,” alisisitiza Profesa Muhongo.
Aliongeza kuwa kutokana na uzoefu wa viongozi hao na watendaji wa wizara na taasisi, anaamini yatakuwepo mabadiliko makubwa katika sekta hizo kutokana na sifa zao kitaaluma na kiutendaji.
“Wananchi wana imani kubwa na uteuzi wetu na uwepo
wetu katika  wizara. Tufanyekazi kwa manufaa ya taifa letu,” aliagiza.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Profesa Justin Ntalikwa, alisema uongozi huo mpya unatarajiwa kufanyakazi kwa uadilifu na umakini mkubwa.
“Jukumu lililo mbele yetu ni kubwa. Tunahitajika kufanya kazi kwa bidii, tukitumia uzoefu wetu katika kutekeleza majukumu yaliyo mbele yetu,” alisema Profesa Ntalikwa.
Naye, Naibu Katibu Mkuu, anayeshughulikia masuala ya madini, Profesa James Msofe, alisema anatarajia kujifunza kwa kasi kubwa majukumu yake ili kuweza kufikia matarajio ya wananchi na taifa.

No comments:

Post a Comment