KATIBU Mkuu Kiongozi, Balozi John Kijazi, ameonya
kuwa kasi ya utumbuaji majipu itaendelea na kusisitiza imelenga kurejesha
nidhamu kwa watumishi wa umma.
Amesema kamwe watumishi hawapaswi kutekeleza majukumu
yao kwa kusukumwa, hivyo atasimamia kikamilifu vipaumbele vya serikali ya awamu
ya tano katika kupambana na rushwa, ufisadi pamoja na uwajibikaji kwa
watumishi.
Balozi Kijazi, ambaye awali alikuwa Balozi wa
Tanzania nchini India, aliyasema hayo jana, muda mfupi baada ya kuapishwa kushika
wadhifa huo na Rais Dk. John Magufuli.
Baada ya Dk. Magufuli kumuapisha jana, Ikulu Dar es
Salaam, Balozi Kijazi anakuwa Katibu Mkuu Kiongozi wa nane kushika wadhifa huo
katika historia ya nchi tangu mwaka 1962.
Makatibu hao ni Dustan Omari (1962-1964), Joseph
Namata (1964-1967), Dickson Nkendo (1967-1974), Timothy Apiyo (1974-1986), Paul
Rupia (1986-1995).
Wengine ni Marten Lumbanga (1995-2006), Philemon
Luhanjo (2006-2011) na Balozi Ombeni Sefue (2011-2016).
Balozi Kijazi alisema, atafanyakazi kwa karibu
kuhakikisha vipaumbele vilivyowekwa vinafikiwa, ikiwemo kusimamia utendajikazi
kwa watumishi wa serikali.
Aliongeza kuwa atamsaidia Dk. Magufuli katika utekelezaji
wa majukumu yake kwa kuandaa vikao vya Baraza la Mawaziri na kushirikiana
pamoja na viongozi wengine wakuu wa serikali.
Alivitaja vipaumbe ambavyo amejikita katika
kufanikisha vinatekelezwa kama, ambavyo rais anavyohitaji kuwa ni kuongeza
uwezo wa serikali kwenye makusanyo ya kodi, kupambana na rushwa na kurejesha
nidhamu ya utendaji kwa watumishi wa umma.
Awali, Katibu Mkuu aliyemaliza muda wake, Balozi
Ombeni Sefue, alimshukuru Rais Dk. Magufuli kwa kumwezesha kutumikia nafasi
hiyo katika kipindi chake cha utumishi.
Pia, alimshukuru Rais mstaafu Jakaya Kikwete, kwa
kumuamini na kumteua kushika nafasi hiyo mwaka 2010, wakati alipokuwa Balozi wa
Kudumu wa Tanzania kwenye Umoja wa Mataifa (UN).
Alisema licha ya kutumikia serikali ya awamu ya nne
iliyomaliza muda wake, lakini Rais Dk. Magufuli alimwamini na kuendelea na
wadhifa huo kwa kipindi cha miezi mitatu.
“Baada ya kumalizika kwa awamu ya nne ya serikali,
sikuwa na ulazima wa kuendelea, lakini rais aliona ni vyema nibakie
kushirikiana naye kwenye masuala mbalimbali,” alisema Balozi Sefue, ambaye
atapangiwa majukumu mengine.
WASIFU
WA BALOZI KIJAZI
Kabla ya uteuzi huo, Balozi Kijazi alikuwa Mwakilishi wa
Tanzania nchini India, Singapore, Sri Lanka, Bangladesh na Nepal, mwenye makazi
yake jijini New Delhi, India, kuanzia mwaka 2007.
Vilevile, hadi uteuzi wake, Balozi Kijazi amekuwa Mkuu wa
Mabalozi wa Afrika nchini India.
Akiwa nchini humo, alikuwa mtetezi mkuu wa wanafunzi wenye
asili ya Kiafrika katika masuala mbalimbali, hususan yaliyohusiana na vitendo
vya unyanyasaji.
Kabla ya kuwa balozi, Mhandisi Kijazi alikuwa Katibu Mkuu
Wizara ya Ujenzi na baadaye Wizara ya Maendeleo ya Miundombinu kuanzia mwaka
2002 hadi 2006.
Baadaye aliteuliwa kuwa Balozi ndani ya Wizara ya Mambo ya
Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na hatimaye kupangiwa kituo cha New Delhi,
India.
Kati ya mwaka 1996 hadi 2002, Balozi Kijazi alikuwa Mhandisi
Mwandamizi wa Ujenzi wa Barabara ndani ya Wizara ya Ujenzi kabla ya kupandishwa
cheo na kuwa Mkurugenzi wa Barabara za Mikoa ndani ya wizara hiyo.
Balozi Kijazi alipata Shahada ya Sayansi ya Uhandisi wa Umma
mwaka 1982 kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na baadaye Shahada ya Uzamili
katika Uhandisi wa Barabara Kuu kutoka Chuo Kikuu cha Birmingham, Uingereza
mwaka 1992.
No comments:
Post a Comment