Sunday 25 September 2016

MSAJILI WA VYAMA VYA SIASA ANAYO MAMLAKA YA KISHERIA KUSHUGHULIKIA MALALAMIKO NA HOJA ZILIZOWASILISHWA KWAKE NA BAADHI YA WANACHAMA NA VIONGOZI WA CUF



UTANGULIZI

Kuna baadhi ya watu wanadai kuwa, Msajili wa Vyama vya Siasa hana mamlaka ya kuingilia maamuzi ya chama cha siasa, hivyo msimamo wake juu ya mgogoro wa uongozi wa chama cha CUF ni batili. Napenda kutumia fursa hii kuwafahamisha kuwa, Msajili wa hana mamlaka ya kuingilia uamuzi halali uliofanywa na kikao halali cha chama cha siasa, Lakini, kama uamuzi ni batili na kikao ni batili au uamuzi ni halali umefanywa na kikao batili au uamuzi batili umefanywa na kikao halali, msajili hawezi kuutambua, kwani Sheria ya Vyama vya Siasa inampa Msajili wa Vyama vya Siasa wajibu wa kusimamia utekelezaji wa baadhi ya maamuzi ya chama cha siasa ikiwamo suala la upatikanaji wa viongozi wa kitaifa wa chama cha siasa kwa mujibu wa katiba na kanuni za chama husika. Ni vyeme ieleweke wazi kuwa kwa mujibu wa kanuni ya 5(1) ya Kanuni za Usajili wa Vyama vya Siasa uamuzi wa kufanya mabadiliko yoyote kwa viongozi wa kitaifa wa chama cha siasa ni lazima upelekwe kwa Msajili wa Vyama vya Siasa ili atambue mabadiliko hayo.

Hivyo, kuhusu mgogoro wa uongozi katika chama cha CUF uliojitokeza kufuatatia kujiudhuru kwa Profesa Lipumba ni kwamba, malalamiko na hoja zilizowasilishwa kwa Msajiili wa Vyama vya Siasa na baadhi ya viongozi wa CUF ikiwamo Profesa Lipumba zilikuwa za aina tatu, ambazo ni zifuatazo:-
1.    Kupinga utaratibu uliotumika kuendesha Mkutano Mkuu wa Taifa wa tarehe 21 Agosti, 2016;
2.    Kujiuzulu na kutengua kujiuzulu uenyekiti wa taifa wa CUF; na
3.    Kupinga uhalali wa kikao cha Baraza Kuu la Uongozi cha tarehe 28 Agosti, 2016 kilichofanyika Zanzibar na maamuzi yake.

Malalamiko na hoja zote tajwa hapo juu zinahusu hatma ya baadhi ya viongozi wa kitaifa wa chama cha CUF. Viongozi hao ni wafuatao:-
1.    Profesa Lipumba ambaye aliandika barua ya kujiuzulu uenyekiti wa Taifa na kuitengua;
2.    Mheshimiwa Mgdalenda Sakaya Naibu Katibu Mkuu Tanzania Bara aliyesimamishwa uanachama na Kikao cha Baraza Kuu la Uongozi Taifa cha tarehe 28 Agosti, 2016;
3.    Bwana Abdul Kambaya, Naibu Mkurugenzi wa Habari na Uenezi Taifa ambaye pia amesimamishwa uanachama na Kikao cha Baraza Kuu la Uongozi Taifa cha tarehe 28 Agosti, 2016; na
4.    Bwana Shashu Lugeye Katibu wa Baraza la Wazee ambaye alifukuzwa uanachama na Kikao cha Baraza Kuu la Uongozi Taifa cha tarehe 28 Agosti, 2016; 

MSIMAMO WA SHERIA

Hivyo, kwa kuwa kifungu cha 10(f) cha Sheria ya Vyama vya Siasa Sura ya 258 kinahitaji chama cha siasa kuwasilisha orodha ya viongozi wake wa kitaifa kwa Msajili wa Vyama vya Siasa, kifungu 8A(1) kinampa mamlaka Msajili wa Vyama vya Siasa kuhifadhi taarifa za viongozi wa kitaifa wa Vyama vya Siasa na Kanuni ya 5(1) ya Kanuni za Usajili wa Vyama vya Siasa toleo namba 111 la mwaka 1992, inakitaka kila chama cha siasa kuwasilisha taarifa kwa Msajili wa Vyama vya Siasa panapotokea mabadiliko katika uongozi wa taifa. Hivyo, Msajili wa Vyama vya Siasa anao wajibu wa kuhakikisha taarifa za mabadiliko ya uongozi anazoletewa na chama cha siasa, ni sahihi kwa maana ya kuwa, yamefanywa na mamlaka halali ya chama kwa mujibu wa Katiba na Kanuni za chama husika, ili kuepuka kupokea orodha ya mabadiliko ya uongozi wa kitaifa wa chama ambayo si halali kwa mujibu wa Katiba na Kanuni za chama.

Vifungu hivyo vinasema ifuatavyo:-

“10(f) it has submitted the names of the national leadership of the party and such leadership draws its members from both Tanzania Zanzibar and Mainland Tanzania; …”

“8A.-(1) There shall be a register of political parties into which names, addresses and other particulars of registered political parties or national leaders of political Parties shall be entered”


Kanuni ya 5(1) inasema ifuatavyo:-

“5-(1) Where an office –bearer of a registered party ceases to hold office or a person is appointed to be an office-bearer of a registered party, the party shall, within fourteen days, send notice thereof to the Registrar.”

Kwa kuzingatia ulazima wa Msajili wa Vyama vya Siasa kujiridhisha kuwa, mabadiliko yoyote katika uongozi wa kitaifa wa chama cha siasa yamefanywa kwa mujibu wa Katiba na Kanuni za chama husika, ndipo akubali kufanya mabadiliko katika orodha ya viongozi wa kitaifa iliyopo katika Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, ndiyo maana ikawepo kanuni ya 13(1) na 16 zinazompa mamlaka Msajili wa Vyama vya Siasa kuhitaji maelezo kutoka kwa chama cha siasa, kuhusu viongozi wa kitaifa wa chama cha siasa. Kanuni hizo zinasema ifuatavyo, nanukuu:-

       “13-(1) The Registrar may at any time require a party to submit to him a return or report relating to the constitution, objects, office-bearers or membership as well as the finances of the party.
 2) Every office-bearer and every person managing or assisting in the management of a party shall forthwith comply with any requirement made by the Registrar under paragraph (1) of this Regulation.”
  “16. In the event of a breach by a party of the provisions of Regulation 6,7,8,11,12 or 13, every office-bearer of the party concerned shall be guilty of an offence and shall be liable on conviction to a fine not exceeding thirty thousand shillings or to imprisonment for a term not exceeding six months or to both such fine and imprisonment.”
Kwa maana hiyo basi, Msajili wa Vyama vya Siasa anayo mamlaka ya kushughulikia malalamiko na hoja tatu zilizowasilishwa kwake na baadhi ya wanachama na viongozi wa CUF, kwa sababu malalamiko na hoja zote zinagusa mabadiliko katika uongozi wa kitafa wa CUF.

Inaeleweka kuwa, suala la uanachama wa chama cha siasa ni uhusiano wa kimkataba uliopo kati ya mwanachama na chama chake. Hivyo, endapo mwanachama anayechuliwa hatua za kiidhamu siyo kiongozi wa kitaifa wa chama cha siasa, basi Msajili wa Vyama vya Siasa hana mamlaka ya kuingilia mgogoro huo wa uanachama., labda chama cha siasa na mwanachama husika kwa hiari yao wamuombe Msajili wa Vyama vya Siasa kuwasuluhisha.

Isipokuwa, endapo mwanachama husika ni kiongozi wa kitaifa wa chama, basi Msajili wa Vyama vya Siasa anayo mamlaka ya kuingilia mgogoro huo ili kujiridhisha kuwa, mwanachama husika amesimamishwa au kufukuzwa uanachama wake kwa kuzingatia Katiba na Kanuni za chama husika, kwa sababu kusimamishwa au kufukuzwa uanachama wake kunaathiri nafasi yake ya uongozi wa kitaifa.
HITIMISHO
Hivyo, kwa kuwa kifungu cha 10(f) cha Sheria ya Vyama vya Siasa Sura ya 258 kinahitaji chama cha siasa kuwasilisha orodha ya viongozi wake wa kitaifa kwa Msajili wa Vyama vya Siasa, na kwa kuwa kifungu 8A(1) kinampa mamlaka Msajili wa Vyama vya Siasa kuhifadhi taarifa za viongozi wa kitaifa wa Vyama vya Siasa na kwa kuwa pia Kanuni ya 5(1) ya Kanuni za Usajili wa Vyama vya Siasa toleo namba 111 la mwaka 1992, inakitaka kila chama cha siasa kuwasilisha taarifa kwa Msajili wa Vyama vya Siasa panapotokea mabadiliko katika uongozi wa taifa.
Aidha, Msajili wa Vyama vya Siasa kwa mantiki ya majukumu yanayobebwa na vifungu hivyo, anao wajibu wa kuhakikisha taarifa za mabadiliko ya uongozi anazoletewa na chama cha siasa ni sahihi, kwa maana ya kujiridhisha kuwa mabadiliko hayo ya uongozi, yamefanywa na mamlaka halali ya chama na pia yametekelezwa kwa mujibu wa Katiba na Kanuni za chama husika.  Hatua hiyo inafanyika, ili kuepuka kupokea na kuhifadhi taarifa ya mabadiliko katika uongozi wa kitaifa wa chama cha siasa ambayo siyo halali, kwa mujibu wa Katiba na Kanuni za chama husika.
Kwa mantiki hiyo basi, nikijielekeza kwenye vifungu vya Sheria nilivyoainisha hapo juu, ni dhahiri kwamba, Msajili wa Vyama vya Siasa anayo mamlaka na wajibu wa kisheria, kuchunguza mabadiliko katika uongozi wa kitaifa wa chama yaliyofanyika na masuala yote yanayohusu na mabadiliko hayo. Mfano, pale ambapo mwanachama ni kiongozi wa kitaifa wa chama cha siasa Msajili anapaswa kujiridhisha kuwa, mwanachama husika amesimamishwa au kufukuzwa uanachama kwa kuzingatia Katiba na Kanuni za chama, kwa sababu kusimamishwa au kufukuzwa uanachama wake, kunaathiri nafasi yake ya uongozi wa kitaifa.

No comments:

Post a Comment