Sunday 5 March 2017

ALIYEMPA MAKONDA HEKARI 1,50 AMJIBU WAZIRI LUKUVI

 SIKU chache baada ya mfanyabiashara Mohamed Ikbal, kudaiwa kumpa hekari 1,500 zenye  mgogoro, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, mfanyabiashara huyo ameibuka na kutoa ufafanuzi juu ya sakata hilo na kusisitiza kwamba eneo hilo anamiliki kihalali.

Ikbal, ameibuka wiki chache baada ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi,  kueleza kuwa eneo hilo lililoko Lingato, Kisarawe II , Kigamboni jijini Dar es Salaam, ni  mali ya serikali baada ya mfanyabiashara huyo kushindwa kesi dhidi ya wananchi.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, mjini Dar es Salaam, kwa niaba ya mfanyabiashara huyo, Kamugisha Katabaro, alisema Ikbal anamiliki hekari 3,500, katika eneo hilo la Lingato, Kisarawe II, tangu mwaka 2005.

Alisema Ikbal alinunua eneo hilo kutoka kwa wananchi, ambao waliuza kwa hiyari yao wenyewe bila kushurutishwa na kwa kufuata taratibu zote za kisheria.

“Ushahidi wa nakala za barua za mawasiliano kati ya serikali ya mtaa wa Lingato, muhtasari wa vikao vya maamuzi ya serikali ya mtaa na mikutano ya wananchi waliokuwa wamiliki maeneo hayo ipo,”alisema Katabaro.

Aliongeza: “Nakala za stakabadhi za malipo ya ushuru wa  serikali ya mtaa kama sheria inavyotaka, mikataba ya mauziano ya maeneo ya ardhi, sambamba na picha za wamiliki wa maeneo wakipokea fedha za malipo ya mauziano ya ardhi zipo na zitawekwa bayana zikihitajika.”

KUZUKA KWA MGOGORO

Katabaro alisema miaka michache baada ya mauziano hayo, baadhi ya wananchi waliingwa na tamaa kutokana na kupanda kwa thamani ya ardhi.

“Kwa kushirikiana na baadhi ya viongozi wa serikali ya mtaa wasio waaminifu, walianza kuvamia eneo hilo na baadaye kuwasilisha malalamiko  kwa Kamishna wa Ardhi kwamba wananyanyaswa katika ardhi yao na kwamba, hawakuuza maeneo hayo kwa hiari yao,”alisema Katabro.

Alisema Ofisi ya Ardhi katika  barua  yake  ya  Oktoba 31, 2006,  yenye Kumbukumbu Na. LD/164035/CB, iliuomba uongozi wa Halmashauri ya Manispaa ya Temeke, kutoa taarifa  juu ya malamiko ya kundi hilo.

“Katika barua yenye kumbukumbu Na. TMC/MD/M.13/83/79 ya Desemba 18, 2006, Mkurugenzi wa Manispaa ya Temeke alimjulisha  Kamishna wa Ardhi  kuwa, mgogoro huo  ulishughulikiwa na Kamati ya Rais ya Kushughulikia Migogoro chini ya Mstahiki Meya wa manispaa hiyo," alibainisha Katabaro.

Aliendelea kueleza kwamba, kufuatia majibu hayo,  Kamishna wa Ardhi  alilitaarifu kundi hilo la walalamikaji kupitia barua yenye Kumb. Na. LD/164035/VOL.V/39 ya Februari 26,2007.

“Licha ya majibu ya Kamishna wa Ardhi, bado  mgogoro huo uliendelea  na kumfanya Mkuu wa Wilaya ya Temeke, kufanya mkutano kati ya wananchi na Ikbal, uliofanyika Oktoba 8, 2007, ambao ulianyika  katika eneo la Asha Ngoma, Kisarawe II ,”alisema.

Aliongeza: “Baada ya kusikiliza  maelezo  ya pande zote mbili, alihitimisha  mkutano  huo kwa kuwataka  wale wote, ambao wanahisi kudhulumiwa  kupeleka malalamiko yao mahakamani.”

Katabaro alisema kutokana na kuendelea kwa uvamizi katika eneo hilo, Ikbal aliwasilisha  malalamiko  yake katika  Ofisi ya  Mkuu wa Wilaya ya Temeke, ambaye alimuandikia barua Mkuu wa Polisi wa Wilaya  ya Kipolisi ya Kigamboni,  kupitia barua  ya Februari 26, 2008, yenye kumbukumbu Na. E.40/9/VOL.1/64, kumjulisha  juu ya malalamiko hayo na kumtaka kuchukua hatua.

“Kundi la  pili la wavamizi  liliwasilisha malalamiko yao kwenye Ofisi ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, kupitia barua ya Machi 4, 2008,”alibainisha Katabaro.

Aliongeza kuwa baada ya kufuatilia kwa kina, Wizara ya  Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi,  iliwajibu kwa barua ya Mei 9, 2008 yenye kumbukumbu Na. EA71/176/01.B/49, ikibainisha kwamba wananchi hao waliuza maeneo yao kwa hiari.

KUMKABIDHI ENEO MAKONDA

Katabaro alisema mchakato wa  kulipitia eneo hilo ili kukamilisha mchakato wa kulikabidhi kwa Serikali ya Mkoa wa Dar es Salaam, ulizingatia taratibu zote.

“Ikbal aliamua kutoa ene hilo kwa mkoa wa Dar es Salaam, kwa hiari ili kuunga mkono jitihada za serikali katika kukuza viwanda,”alieleza.

Alisema hakuna utata wowote katika eneo hilo kwani taratibu za kumkabidhi Makonda zilifuatwa.

Katabaro alisema Ikbal ameamua kutoa maelezo hayo sio kwa kumjibu Waziri Lukuvi, bali kuweka ukweli wa mambo ili jamii iweze kuufahamu.

No comments:

Post a Comment