Thursday 6 April 2017

JPM AWAAPISHA MAKATIBU WAKUU WAPYA





RAIS Dk. John Magufuli amewaapisha viongozi aliowateua kushika nyadhifa mbalimbali, wakiwemo makatibu wakuu, naibu katibu mkuu, mabalozi na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)
Hafla ya kuapishwa kwa viongozi hao, ilifanyika jana, Ikulu, Dar es Salaam, ambapo ilihudhuriwa na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan.
Walioapishwa ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk. Leonard Akwilapo na Profesa Kitila Mkumbo, ambaye ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji.
Viongozi wengine ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Ave Maria Semakafu; Baraka Luvanda aliyeapishwa kuwa Balozi wa Tanzania nchini India na Sylvester Ambokile, aliyeapishwa kuwa Balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini.
Aidha, Dk. Magufuli amemwapisha Charles Kichere kuwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), ambapo baada ya kuapishwa, viongozi hao walikula kiapo cha uadilifu kwa viongozi wa umma, kilichoongozwa na Katibu wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Waziri Kipacha.
Akizungumza baada ya kuapishwa kwa viongozi hao, Makamu wa Rais Samia, aliwapongeza kwa kuteuliwa kushika nyadhifa hizo na kuwataka kufanyakazi kwa kutanguliza maslahi ya Taifa na kwa kuzingatia sheria na taratibu zilizowekwa.
“Tutawapa ushirikiano wote mtakaouhitaji ili kufanikisha kazi zenu, lakini na nyinyi msituangushe. Kichere tunakutegemea ukaimarishe ukusanyaji wa mapato pale TRA na pia ukawaambie maofisa wako na mameneja wa mikoa, waache kutoa kauli za kuigombanisha serikali na wafanyabiashara, wakusanye kodi kwa kufuata sheria na taratibu na pia wawe na lugha nzuri.
“Profesa Kitila Mkumbo, tunategemea utaongeza msukumo kutatua matatizo ya maji, utasaidia kufanikisha kampeni ya kumtua mama ndoo ya maji kichwani, Watanzania wapate maji safi na salama, ”alisema Makamu wa Rais.

No comments:

Post a Comment