Tuesday 24 October 2017

OMAN KUWEKEZA SEKTA YA VIWANDA VYA NYAMA


WAZIRI wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina, amekutana na Waziri wa Uwekezaji wa Oman, Salim Al Ismail na kujadili uwekezaji wa viwanda katika sekta ya mifugo na uvuvi.

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita, Jijini Dar es Salaam, Mpina alimueleza Salim kuwa, Tanzania imekuwa ikizalisha nyama tani 36, kwa siku na inafanya  biashara hiyo kwa nyama ambazo hazijakatwa katika nchi za Falme za Kiarabu, ikiwemo Oman.

Alisema wakati umefika kwa nchi hizo mbili kushirikiana katika sekta ya mifugo na uvuvi, ili kuwekeza katika viwanda vya ndani vya nyama kwa kuendeleza vilivyopo na kujenga vipya.

“Ni wakati wa nchi hizi kuona namna ya uwekezaji tunaoweza kuufanya.
Tunatambua ujenzi wa kiwanda cha nyama cha Ruvu, ambao umefikia asilimia 51 kukamilika, lakini ipo haja ya kufungua fursa nyingine za uwekezaji,”alisema.

Alisema ni muhimu viwanda vyote vya nyama vya ndani, vikidhi mahitaji na kuweza kuuza nyama nje ya nchi.

Kwa upande wake,  Waziri wa Oman, Al Ismail alipoelezwa kuhusu viwango na madaraja mbalimbali ya nyama nchini na mtaalamu kutoka wizara hiyo, alisema kuwa ameridhishwa na hatua zilizopo.

Waziri huyo alisema wapo tayari kuwekeza katika sekta ya viwanda vya nyama na kuisaidia Tanzania kutafuta soko nchini Marekani kupitia Oman.

Alisema wanacho cheti  na kibali kilichothibitishwa na Mamlaka ya Dawa Marekani, hivyo ni vizuri kushirikiana katika kutumia fursa hiyo.

“Tunaweza kuchukua nyama kutoka Tanzania na kuingiza Marekani bila kulipa ushuru. Tunapaswa kuwa na vyeti halali ili kupata soko katika nchi nyingine,”alisema.

Waziri huyo alisema, kampuni binafsi kutoka Oman, zipo tayari kufanya biashara katika eneo hilo, hivyo ni wakati wa Tanzania kuonyesha utayari.

“Hizi bidhaa za nyama ni lazima zitoke kwenu kwa sababu sisi hatuna maji wala majani ya kulisha mifugo kama ng’ombe, mbuzi na kondoo, ambao huchinjwa kwa wingi baada ya Hijja,”alisema.

Akizungumzia sekta ya uvuvi, waziri huyo alisema wamenunua teknolojia ya kisasa ya uwekezaji katika fukwe ya Bahari kutoka Texas, Marekani, inayojulikana kitaalamu kama ‘Shrim farming’, inayoruhusu uzalishaji wa chakula cha samaki wavuliwao katika maji marefu bila kuharibu mazingira.

Waziri huyo alisema teknolojia hiyo inaweza kutumika katika uwekezaji wa fukwe ya bahari ya Hindi nchini, ikiwemo eneo la Bagamoyo, kwa kuzingatia tathmini ya athari ya mazingira na ujenzi wa miundombinu ya barabara ili kuwasaidia wavuvi wadogo.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dk. Yohana Budeba, alisema hii ni fursa pekee kwa wafanyabiashara wa Oman, kuwekeza au kushirikiana na wafugaji na wavuvi wa ndani, kwa kuwa kuna samaki wengi wa kutosha kumudu viwanda vya kuchakata  na kuwezesha biashara kubwa ya samaki ndani na nje ya nchi.

No comments:

Post a Comment