Thursday, 3 September 2015

MWIGULU: ACHENI KUTUMIA VIBAYA HOTUBA ZA MWALIMU NYERERE


 
Na Nathaniel Limu, Mkalama
WANASIASA wa upinzani wameonywa kuacha kutumia hotuba za Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, kwa lengo la kujinuifaisha kisiasa.
Badala yake wametakiwa kutumia hotuba hizo kujikosoa kutokana na kufanya mambo kinyume na kuliweka taifa kwenye hatari ya kuingia kwenye machafuko.
Onyo hilo limetolewa juzi jioni na Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba, wakati akizindua kampeni za kuwania ubunge na madiwani katika Jimbo la Mkalama mkoani Singida.
Alisema hivi karibuni kumekuwa na wimbi la baadhi ya wagombea wakiwemo wanaowania urais, kutumia baadhi ya hotuba za Mwalimu Nyerere wakilenga kuwaaminisha wananchi wawachague kwa madai watafuata nyayo zake.
“Wengi wa viongozi hawa wanajaribu kuwahadaa wananchi na kuwa kuhama CCM kimezingatia maneno ya Mwalimu Nyerere kuwa, mabadiliko usipoyapata ndani ya CCM, unaweza kuyapata nje ya CCM,” alisema.
Mwigulu, ambaye anatetea nafasi hiyo alisema mabadiliko ya kweli aliyoyazungumza Mwalimu Nyerere sio ya kuhama vyama kusaka nafasi za uongozi bali ni ya kiutendaji ambayo yatafanyika ndani ya CCM na si kwa kukimbilia upinzani.
Alisema itapendeza zaidi iwapo wanasiasa hao mabingwa watazungumzia pia kauli za Mwalimu Nyerere kuwa, 'anayekimbilia Ikulu kwa kutumia fedha hafai na atazirejeshaje'.
"Kama wao ni mabingwa wazungumzie maneno ya Mwalimu Nyerere kuwa 'Ikulu ni mahali patakatifu na kuna nini hadi mtu apakimbilie’. Mwalimu alisema hawa watu wanatoa wapi fedha za kuhonga,” alisema Mwigulu.
Aidha, Mwigulu aliwataka wana CCM waliohama baada ya kushindwa katika kura za maoni huko walikokimbilia kutimiza tamaa zao za kutaka uongozi, wasipopata wanaweza kurejea  CCM iwapo watakaribishwa tena.
"Wewe fikiria mtu kama Lowassa (Edward)  amelelewa na CCM zaidi ya miaka 40 sasa, kichwa chake chote hakina kitu kingine kimejaa CCM. Mambo ambayo atataka kuyaanzisha kwenye UKAWA yatakuwa na harufu kubwa ya CCM tu. Kwa hiyo, huko walikokimbilia kusaka uongozi kwa gharama yoyote ikiwemo ya matumizi makubwa ya fedha hakuna cha ziada,” alisema.
Alisema upinzani katika uchaguzi mkuu mwaka huu haupo kabisa bali kilichopo ni CCM (A) na CCM (B) ndizo zinazochuana.
Mwigulu aliwaeleza wananchi hao kuwa chaguo la Watanzania kwa urais ni Dk. John Magufuli, ambaye ni kiongozi safi na asiye na kashfa.

No comments:

Post a Comment