Monday 28 September 2015

NAPE AWALIPUA LOWASSA, MCHUNGAJI MSIGWA




KATIBU wa NEC, Itikadi na uenezi, Nape Nnauye, akizungumza kwenye mkutano huo, alisema mapungufu ya CCM yalisababishwa na watu wachache ambao leo hawapo tena ndani ya chama hicho.
Alisema wachache hao walikuwa wakifanya maovu kwenye madaraka waliyopewa seriakalini kisha kukigeukia Chama na kukifanya kichaka cha kujifichia, jambo lililofanya wengi kukinyooshea kidole.
Aidha, aliwaasa Watanzania kuwa Taifa halihitaji rais wa majaribio na kwamba, ifikapo Oktoba 25, mwaka huu, wamchague Dk. Magufuli ambaye ana nia ya dhati ya kuleta mabadiliko ya kweli.
Alisema Dk. Magufuli ni kiongozi sahihi wa kukabidhiwa Tanzania kwa kipindi cha miaka mitano ijayo kwa sababu hana kasoro ya uadilifu kwenye miaka yake yote ya utendaji wake serikalini, tofauti na mgombea wa CHADEMA, Edward Lowassa. 
Nape alisema Lowassa anamfahamu na kwamba, alipotaka kuwa miongoni mwa makada waonesha nia ya kutaka kuchaguliwa kuiwakilisha CCM kwenye nafasi ya urais mwaka huu, alimwambia kutokana na historia yake ya ufisadi asingeweza kufanikiwa.
Alisema mgombea huyo ambaye aliwahi kuwa Waziri Mkuu wa Tanzania kwa miaka miwili na kisha kujiuzulu kwa kashfa ya zabuni ya kampuni ya Richmond, si msafi na kila alipopewa majukumu ya uongozi serikalini, aliharibu kwa kuhusishwa na ubadhirifu wa rasilimali fedha.
Alisema tangu Lowassa alipofika Makao Makuu ya CCM kwa mara ya kwanza, alikuwa na tabia ya udokozi na kwamba, hata baada ya kushika nyadhifa nyingine nje ya Chama, ikiwemo uongozi wa Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC), aliendelea na tabia zake.
Nape alisema Lowassa alipokuwa kwenye wizara mbalimbali aliendelea kutumia vibaya madaraka aliyokuwa nayo ambapo, mfano mzuri ni alipokuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, ambako alijilimbikizia maeneo mengi makubwa ya ardhi sehemu mbalimbali za nchi.
“Lowassa si msafi, anadanganywa na akina Mbowe ajiamini, lakini ukweli ni hafai. Wapi kapewa majukumu bila kuharibu? Kama anabisha ajitokeze hapa akatae hadharani. Hakuna, kote alikopita kaharibu, hivyo hatuwezi kumpa Ikulu mtu wa aina hiyo na Watanzania msimruhusu hata kuikaribia,” alisema.
Aliongeza kuwa Lowassa ni gamba namba moja lililokisumbua Chama kwa muda mrefu, lakini baada ya kutoka na kwenda upinzani, CCM imetulia na usafi wake wa zamani umerejea na kipo imara kuwahudumia Watanzania kwa kipindi kingine cha uongozi wa nchi.
“Tulitembea nchi nzima miezi 28, kukagua utekelezaji wa ilani ya uchaguzi na sera za chama, kweli kulikuwa na sehemu hazikuwa sawa na wananchi walituambia, rushwa, dhuluma, urasimu yote haya tumepambana nayo hayapo,” alisema Nape.
AMSHUKIA MSIGWA
Kuhusu Mchungaji Peter Msigwa, Nape alisema hafai kuchaguliwa na wananchi wanapaswa kumpinga hadharani kutokana na kulamba matapishi yake.
Alisema Mchungaji Msigwa aliwahi kutamka kuwa wanaomuunga mkono Lowassa wanapaswa kupimwa kwanza akili, lakini akabadilisha mawazo na msimamo wake baada ya kununuliwa.
“Msigwa aligoma kumkubali Lowassa mpaka apewe ‘uji mdomoni’, akapewa uji na mpango mzima ulifanyika hotelini na kamera ziliwakamata na picha zipo, kama anabisha ajitokeze,” alisema Nape.
Nape alisema Msigwa aliwahi kuwataka wananchi wa Iringa kuacha kununua bidhaa za Kampuni ya ASAS, ambayo inaongoza kwa kuwaajiri vijana wengi wa Iringa ili wamsaidie kwenye maandamano, kitu kinachodhihirisha kuwa hafai kuwa kiongozi.
Alisema badala ya kuwa kiongozi wa mfano kutokana na kuwa na kofia ya dini, Msigwa amegeuka kuwa tapeli, ambaye alisababisha kambi ya ujenzi wa barabara ya Iringa kwenda Dodoma kuhamishwa Isimani kutokana na eneo lililopangwa kuwekwa kambi hiyo awali, kuwa mali ya mchungaji huyo kwa ajili ya kanisa lake.
Nape alisema wana Iringa umefika wakati wa kulikomboa jimbo na kumpa kura ya ndiyo, Fredrick Mwakalebela na kuachana na Msigwa, ambaye ameshindwa kusimamia msimamo wa kumkataa Lowassa kukinunua chama chao cha CHADEMA.
Kuhusu Fredrick Sumaye, ambaye naye alihama CCM kwenda CHADEMA, Nape alisema alikuwa akimheshimu, lakini kiongozi huyo aliyewahi kuwa Waziri Mkuu katika awamu ya tatu ya serikali, amejivua heshima kuungana na Lowassa upinzani.
Alisema Sumaye kwa sasa amekosa hoja zaidi ya kupiga kelele kudai wataibiwa kura Oktoba 25, mwaka huu, jambo ambalo halina ukweli kwa sababu wanatambua hawawezi kushinda uchaguzi mkuu mbele ya CCM.
LUKUVI ANG’AKA
Akizungumza kwenye mkutano huo, mgombea Ubunge wa Jimbo la Isimani, William Lukuvi, amewataka watendaji wa serikali wasiowajibika kuandika barua ya kuacha kazi kabla ya Dk Magufuli hajaingia madarakani.
Alisema Dk Magufuli ni mchapakazi asiyetaka mzaha kwenye utendaji kazi, hivyo watendaji wanaofanya kazi kwa kuwadhulumu wananchi, muda wao wa kuacha kazi umewadia.
“Anayetaka kufanya kazi na Magufuli afahamu kwamba, hataki mchezo. Kama kuna mtendaji anayevurunda na kujificha kwenye kivuli cha CCM, aandike barua ya kuacha kazi kabla Magufuli hajashika madaraka,” alisisitiza.
Lukuvi, ambaye pia ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, aliwaambia wananchi waliofurika kwenye uwanja wa Samora kumsikiliza mgombea urais wa CCM, Dk Magufuli, kuwa mtindo wa baadhi ya watendaji kutumia madalali kuwanyanyasa wafanyabiashara ndogondogo umekwisha.
Alisema Dk. Magufuli ana uwezo wa kuwatumikia wananchi kwa kuwa ana uzoefu na utendaji kazi wake umetukuka na usiotiliwa shaka.

No comments:

Post a Comment