Sunday 20 September 2015

TUNDU LISSU AKIMBIWA JIMBONI



Na Nathaniel Limu, Ikungi
HARAKATI za Tundu Lissu kutetea ubunge  jimbo la Singida Mashariki zimeingia dosari baada ya baadhi ya viongozi na wanachama wa CHADEMA kukihama chama hicho na kurejea CCM kwa madai chama hicho cha kimedumaza maendeleo ya jimbo hilo.
Baadhi ya viongozi waandamizi katika jimbo hilo, waliohama hivi karibuni  na kurejea CCM ni Mwenyekiti CHADEMA Kata ya Mungaa, Ali Juma Kiemi, Katibu Mwenezi CHADEMA Kata ya Mungaa, John Mpaki na Katibu Mwenezi CHADEMA Kata ya Ikungi, Khamisi Mazonge.
 Viongozi hao kwa sasa wanatumiwa na CCM katika kampeni ya kuiondoa CHADEMA Jimbo la Singida Mashariki.
Akizungumza kwenye mkutano wa kampeni CCM katika Kijiji cha Kinyamwandio, Tarafa ya Ikungi, Mazonge alisema CHADEMA jimbo la Singida Mashariki katika miaka yake mitano iliyopita, haijaleta maendeleo  na kusababisha jimbo hilo kushika mkia kimaendeleo mkoani Singida.
 “Kilichofanyika katika miaka hiyo ni maneno matupu tena ya upotoshaji, maendeleo katika sekta zote yamesimama, wananchi tumedanganywa kuwa serikali ndiyo yenye jukumu la kuliletea jimbo letu maendeleo na si wakazi wake. Ilidaiwa kuwa serikali ina fedha za kutosha kuleta maendeleo, lakini hadi sasa hatujaziona hizo fedha,” alifafanua Mazonge.
 Katika hatua nyingine, Mazonge aliwataka mgombea urais kupitia UKAWA, Waziri Mkuu aliyejiuzulu kwa kashfa ya Richmond, Edward Lowassa na Waziri Mkuu wa zamani, Frederick Sumaye, wawatangazie Watanzania kuwa sasa wanaunga mkono serikali tatu.
Kwa upande wake, aliyekuwa Mwenyekiti CHADEMA Kata ya Mungaa,  Kiemi alitumia fursa hiyo kuwataka wana CHADEMA katika jimbo hilo kuhama kwa kuwa licha ya kudumaza maendeleo, jimbo hilo litakuwa tanuru la kuzalisha vijana watumishi na walinzi wa nyumba za wasomi.
 “Niwatake wenzangu waliobakia CHADEMA wafanye maamuzi sahihi mapema ya kurejea CCM na waondokane na fikira potofu, kuwa Tundu Lissu, ni mkombozi wao. Lissu hawezi kuwa mkombozi kwa vile hajaleta maendeleo yoyote jimboni kwa miaka mitano. Alicholeta ni maneno matupu na kwake vitendo ni mwiko…maendeleo huletwa kwa vitedo na si vinginevyo,”alisema.
Pia, Kiemi alisema amechukizwa na kuhuzunishwa na kitendo cha CHADEMA kumpokea Lowassa na kumuuzia chama kizima.
 “Lowassa licha ya kununua CHADEMA,  amekilazimisha chama kupokea makapi marafiki zake kutoka CCM na kuyapa nafasi zikiwemo za ubunge. Makapi hayo yamewaengua wanachama wa CHADEMA waliokijenga chama hadi kikawa na nguvu, hii ni dhambi kubwa,”alisema.
 Baadhi ya wanachama wa CHADEMA na wakazi wa jimbo la Singida mashariki,wameanza kuingiwa na na hofu kwamba  Lissu anaweza kupoteza  nafasi yake mwaka huu, kama upepo wa kisiasa jimboni humo utaendelea kama ulivyo hivi sasa.

No comments:

Post a Comment