Wednesday 30 December 2015

PROFESA MBARAWA AZISHUKIA TRL NA RAHCO



Profesa Mbarawa azitaka TRL na RAHCO kujiimarisha Waziri wa Ujenzi,Uchukuzi na Mawasiliano Mhe.Prof. Makame Mbarawa amezungumzia umuhimu wa Shirika la Reli Tanzania (TRL) na Kampuni Hodhi ya Rasilimali za Reli (RAHCO) kufanya kazi kwa umoja na ushirikiano ili kuboresha huduma za reli. 
 
Akizungumza na watendaji wa TRL na RAHCO Prof. Mbarawa amewataka watendaji hao kutengeneza mkakati utakaowezesha usafiri wa reli nchini kuwa wa uhakika kwa abiria na mizigo ili kupunguza msongamano kwenye barabara na kuwezesha shehena kubwa ya mizigo kusafirishwa kwa njia ya Reli. 

“Karabatini njia ya reli na kuimarisha sehemu zote zenye usumbufu ili kukabiliana na changamoto zinazoweza kutokea wakati wa mvua za masika zinazotegemea kuanza hivi karibuni”, amesema Prof. Mbarawa. Prof. 

Mbarawa amemtaka Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TRL Eng.Elias Mshana kuhakikisha Shirika hilo linaongeza mapato yake ili kuboresha huduma za injini na mabehewa na hivyo kuvutia wasafirishaji wengi kutumia usafiri wa Reli. 

Aidha, amemuagiza Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa RAHCO Eng.Festo Mwanyika kuhakikisha ukarabati mkubwa wa kiwanda cha kutengeneza kokoto cha Tura Kwale kilichopo Mkoani Tabora kinakamilika kwa wakati na kuanza kuzalisha kokoto zitakazosambazwa katika miundombinu ya reli nchini, hatua itakayoendana na ukarabati wa reli katika maeneo korofi. 

Naye Naibu Waziri wa Ujenzi,Uchukuzi na Mawasiliano Eng.Edwin Ngonyani amewataka watumishi wote wa TRL na RAHCO kufanya kazi kwa weledi na ubunifu ili kuvutia wadau wengi kutumia huduma za Reli na hivyo kuboresha sekta hiyo muhimu kwa Uchumi wa taifa na nchi jirani.

Amekemea watendaji wanaofanya kazi kwa maslahi binafsi na kuleta hasara kwa nchi na kusisitiza kuwa hawatavumiliwa. 

Waziri Mbarawa na Naibu wake wapo katika ziara ya kukagua na kutoa muongozo kwa watendaji wa taasisi zilizopo chini ya Wizara ya Ujenzi,Uchukuzi na Mawasiliano ambapo msisitizo wao umekuwa kufanya kazi kwa uadilifu na uharaka ili kuleta matokea bora. Imetoleta na kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

No comments:

Post a Comment