WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema serikali
haijaridhia viwango vipya vya nauli ya mabasi yaendayo kasi vilivyopendekezwa
na waendeshaji wa huduma ya mabasi yaendayo kasi Dar es salaam (UDART).
Amesema gharama hizo ni kubwa mno kwa wananchi na
watumishi na kwamba mradi huo, ulilenga kumrahisishia mtumishi wa serikali
anayeishi nje ya jiji.
“Serikali iliwekeza katika mradi huu ili kusaidia
watumishi na wananchi ambao hawana vipato vikubwa,” amesema Waziri Mkuu.
Majaliwa alisema hayo jana, alipowasili kwenye Uwanja wa
Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam, akitokea mkoani Ruvuma,
alikokwenda kwa ziara ya siku tatu.
Kwa mujibu wa mapendekezo ya DART, nauli ya kutoka Mbezi
hadi Kimara sh. 700, Mbezi hadi Kariakoo sh. 1,200 na nauli ya kutoka Mbezi
hadi Mwenge sh. 1400 wakati wanafunzi watatozwa nusu ya viwango hivyo vya
nauli.
Waziri Mkuu alisema endapo UDA-RT itashindwa kutoa
huduma ya usafiri huo kwa kuzingatia maisha halisi ya Mtanzania, serikali
itauchukua na kuuendesha.
Aidha, ameagiza Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais
anayeshughulikia Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, George Simbachawene na
Waziri wa Ujenzi , Uchukuzi, na Mawasiliano pamoja na wadau, wakutane kupanga
upya viwango hivyo na kama watashindwa serikali itaendesha mradi huo.
Novemba 25, 2015, Waziri Mkuu alimuagiza aliyekuwa
Katibu Mkuu Wizara ya TAMISEMI na waendeshaji wa mradi huo kupitia misuada yote
na kurekebisha miundombinu ili mradi huo uanze kufanyakazi ifikapo Januari 10,
mwaka huu.
Imebainika kuwa UDART hawakuandaa mpango wa biashara
wala kuanisha gharama za uendeshaji.
Aidha, imebainika kuwa licha ya kampuni hiyo kutokuwa na
mpango wa biashara na uwekezaji, vigezo vya nauli ilivyoviwasilisha kwenye
Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi kavu na Majini (SUMATRA) havina
uhalisia.
Majaliwa alisema lengo la kuanzisha mradi huo wa usafiri ilikuwa kutoa huduma kwa kuwapunguzia kadhia wananchi pamoja na watumishi wa sekta
mbalimbali, kutumia gharama kubwa kufika kwenye maeneo yao ya kazi.
“Kama mtumishi wa ngazi ya nchini anayelipwa mshahara wa
sh. 260,000 kwa viwango vya nauli vilivyopangwa, atalazimika kutumia robo tatu
ya mshahara wake kwenye nauli.
“Lazima ifahamike kuwa, mradi huu umeanzishwa
kumuhudumia mwananchi, hivyo serikali haitosita kuuchukua na kuuendesha
kama wakishindwa kuweka nauli kwa mujibu
wa gharama za uwekezaji na uendeshaji,” alisisitiza Majaliwa.
Alisema, serikali
haiwezi kuruhusu viwango hivyo vya nauli kutumika kwa sababu vitamuongezea
mzigo mwananchi wa kulipa gharama kubwa zaidi kuliko uhalisia wa vipato vyao.
Hivyo aliagiza mradi huo haupaswi kuanza hadi viwango
vya nauli vitakapoangaliwa upya kwa kuzingatia nauli zitakazomwezesha mwananchi
kuzimudu.
No comments:
Post a Comment