Friday 26 February 2016

VIGOGO WATATU DART KIZIMBANI



VIGOGO watatu wa Mradi wa Mabasi yaendayo Haraka Jijini Dar es Salaam (DART) akiwemo Mtendaji Mkuu, Asteria Mlambo, wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Kiongozi huyo na watendaji wenzake wawili na mfanyabiashara Yuda Mwakatobe, walifikishwa mahakamani hapo jana na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), kwa tuhuma za kuisababishia hasara serikali ya sh. milioni 83.5.
Mbali na Asteria, vigogo wengine wa DART ni Mkurugenzi wa Fedha na Utawala, Evodius Katale na Mwanasheria Mkuu, Francis Kugesha.
Asteria, Katale, Kugesha na Mwakatobe walipandishwa kizimbani mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Respicious Mwijage na kusomewa mashitaka matatu na Wakili wa Serikali, Jacqline Nyantori, akishirikiana na Wakili wa Serikali, Esterzia Wilson na mawakili kutoka TAKUKURU, Vera Ndewoya na Stella Mafuru.
Akiwasomea mashitaka, Jacqline alidai shitaka la kwanza linawakabili Asteria, Katale na Kugesha, ambao wanadaiwa kuisababishia DART hasara ya sh. 83,564,367.
Alidai washitakiwa hao walitenda kosa hilo, kati ya Septemba Mosi na Oktoba 31, 2013, Kinondoni, Dar es Salaam, ambapo wakiwa na nyadhifa hizo, walishindwa kutekeleza majukumu yao kwa weledi, hivyo kuisababishia DART hasara ya kiasi hicho.
Shitaka la pili na tatu yanamkabili Mwakatore, ambaye anadaiwa kutoa taarifa za uongo kwa maofisa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), juu ya taarifa za fedha, hivyo kutozwa kodi chini ya kiwango anachotakiwa kulipa.
Inadaiwa Juni 29, 2005, katika ofisi za kodi za mkoa wa Ilala, Mwakatobe alitoa taarifa za uongo kwa maofisa wa TRA, wakati akiwasilisha taarifa za kampuni yake ya Yukan Business C. Ltd za mwaka wa fedha wa 2004, ambazo zilikuwa zina maelezo ya uongo, hivyo kuwafanya maofisa hao kumtoza kodi chini ya ile aliyotakiwa kutozwa.
Mshitakiwa huyo pia anadaiwa kutenda kosa kama hilo Mei 26, 2006, alipowasilisha taarifa za kampuni hiyo za mwaka wa fedha 2005.
Washitakiwa hao, ambao wanatetewa na Wakili Yuda Tadei, walikana mashitaka, ambapo upande wa jamhuri ulidai upelelezi haujakamilika na kwamba hauna pingamizi juu ya dhamana.
Hata hivyo, upande wa Jamhuri ulitoa angalizo kwa mahakama wakati unatoa masharti ya dhamana kwa washitakiwa Asteria, Katale na Kugesha, izingatie kifungu cha 36(3)(e) na cha 5 cha Sheria ya Uhujumu Uchumi juu ya kiwango kilichoko katika hati ya mashitaka.
Wakili Jacquline alidai kutokana na matakwa ya sheria, washitakiwa hao watatu wanatakiwa kuwasilisha mahakamani fedha sh. milioni 13.9 au hati ya mali isiyohamishika yenye thamani hiyo.
Kwa upande wa wakili wa utetezi, aliiomba mahakama kutoa masharti nafuu kwa kuzingatia kwamba, washitakiwa ni maofisa wa serikali ambao hawategemewi kuruka dhamana.
Baada ya kuelezwa hayo, hakimu aliwahoji washitakiwa iwapo wana hati za mali zisizohamishika, ambapo Kugesha alidai wameletwa mahakamani wakitokea ofisini huku Asteria akidai ana hati ya nyumba ipo nyumbani.
Hakimu Mwijage alitoa masharti ya dhamana ambapo aliwataka washitakiwa Asteria, Katale na Kugesha, kila mmoja kuwa na mdhamini mmoja atakayetia saini dhamana ya sh. milioni 15 na awe na barua ya utambulisho kutoka ofisi ya serikali, taasisi yoyote au kampuni inayosajiliwa kisheria.
Pia, washitakiwa hao wanatakiwa kuwasilisha mahakamani hati ya mali isiyohamishika yenye thamani sio chini ya sh. milioni 14, ambapo sharti hilo halitatimizwa kwa jana, lakini haliwezi kuzuia wasipewe dhamana. Hata hivyo, walitakiwa kuzileta baada ya siku saba.
Kwa upande wa mshitakiwa wa nne, alitakiwa kuwa na mdhamini mmoja atatayetia saini dhamana ya sh.milioni tano na awe na barua ya utambulisho kutoka ofisi yoyote ya serikali au taasisi na kampuni iliyosajiliwa kisheria.

Washitakiwa Asteria, Katale na Kugesha walitimiza masharti ya dhamana kwa kuwasilisha wadhamini. 
Sharti la kuwasilisha hati ya mali isiyohamishika liliweza kutimizwa na Kugesha, ambaye aliwasilisha hati ya nyumba yenye thamani ya sh. milioni 299, huku Asteria na Katale wakipewa muda hadi Machi 3, mwaka huu, kuwasilisha hati za mali zisizohamishika na wakishindwa kufanya hivyo watafutiwa dhamana.
Hakimu Mwijage aliahirisha shauri hilo hadi Machi 9, mwaka huu, kwa kutajwa.

No comments:

Post a Comment