Friday 4 March 2016

DAR YAPATA HASARA YA BILIONI NNE KWA SIKU




MSONGAMANO katika barabara za Jiji la Dar es Salaam, unadaiwa kusababisha hasara ya sh. bilioni nne kwa siku na sasa mkakati mpya ni kuzuia magari yenye uzito wa zaidi ya tani 10 kuingia mjini.
Mkuu wa Mkoa wa huo, Said Mecky Sadiki, alisema hayo jana, wakati akifunga mkutano wa Bodi ya Barabara na kuongeza kuwa, fedha hizo hupotea kutokana na wananchi kukaa kwenye msongamano, ambapo hukwamisha uzalishaji mali na kupunguza tija.
Alisema hali hiyo inatokana na jiji hilo kuwa na mtandao finyu wa barabara uliopo,  ikilinganishwa na idadi kubwa ya magari na vyombo vingine vya usafiri na kwamba, jitihada zinaendelea ili kumaliza tatizo hilo.
“Ndiyo maana Rais Dk. John Magufuli, kwa kuliona hilo alitoa sh. bilioni nne kwa ajili ya upanuzi wa barabara ya Ali Hasan Mwinyi kutoka Morocco hadi Mwenge. Fedha hizo ni zile ambazo zilikuwa zitumike kwa ajili ya sherehe za Uhuru mwaka jana. Tunamshukuru rais na ujenzi unaendelea vizuri,” alisema Sadiki.
Ameziagiza manispaa za jiji hilo kuweka alama za barabarani zinazoonyesha zuio kwa magari yote yenye uzito wa zaidi ya tani 10, kupita kwenye barabara za lami katikati ya jiji ili wamiliki na madereva watakaokiuka agizo hilo wachukuliwe hatua kali za kisheria.
Alisema manispaa hizo zinatenga fedha nyingi za kujenga barabara mpya na kufanya matengenezo ya zile zilizopo, ambazo nyingi zinaharibiwa na malori ya mizigo.
Alifafanua kuwa matumizi hayo mabaya ya barabara kwa kiasi kikubwa yanachangiwa na ukiukwaji wa sheria za barabarani, ambapo malori makubwa ya mizigo huegeshwa na kuziba maeneo ya waenda kwa miguu, jambo linalowanyima haki wananchi kutumia maeneo yaliyotengwa kwa ajili yao.

No comments:

Post a Comment