RAIS Dk. John Magufuli amesema, Tanzania haipaswi
kuona aibu kujifunza maendeleo yaliyofikiwa na Vietnam na endapo ikishindwa
kufanya hivyo, falsafa ya HapaKaziTu, haitofikia malengo yaliyokusudiwa.
Amesema licha ya taifa hilo kupigana vita kuanzia
mwaka 1945 hadi 1976, lakini limepiga hatua kubwa kiuchumi na kufanikiwa
kupunguza umasikini kwa asilimia 50.
Adha, Rais wa Vietnam, Truong Tang San, amebainisha
kuwa wataongeza uhusiano na ushirikiano kati ya taifa hilo na Tanzania kwenye
njanya za kijeshi, kilimo, ufugaji na uvuvi.
Awali, kabla ya kuwasili Ikulu, jijini Dar es Salaam,
wananchi walikusanyika kwenye viwanja vya Ikulu, wakiwa na shauku ya kumlaki
kiongozi huyo, ambaye aliambatana na ujumbe wa viongozi na wafanyabiashara
zaidi ya 50.
Alipowasili kwenye viwanja hivyo saa tatu asubuhi,
alilakiwa na mgeni wake, Rais Dk. Magufuli na baadaye kwenda kwenye jukwaa
maalumu, kisha kupigwa nyimbo za taifa pamoja na mizinga 21.
Rais Truong, pia alipata fursa ya kukagua gwaride
maalumu lililoandaliwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi (JWTZ).
Baada ya hapo, kiongozi huyo akiambatana na Rais
Magufuli, Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa,
Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John Kijazi pamoja na viongozi wengine wa serikali,
walilakiwa na wananchi kwenye viwanja vya Ikulu, wakati walipokuwa wakiingia
kwa ajili ya mazungumzo.
Viongozi hao walifanya mazungumzo maalumu yaliyohusu
ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.
Wakati viongozi hao wakiendelea na mazungumzo, ujumbe
wa Rais Truong, ulionekana kupendezewa na mazingira, amani na ukarimu wa
Watanzania.
Mara kwa mara walikuwa wakipiga picha na baadhi ya
wananchi katika maeneo mbalimbali yanayozunguka Ikulu, hususan ufukwe wa bahari
ya Hindi.
Baada ya kumaliza mazungumzo, Rais Dk. Magufuli,
alipata fursa ya kuzungumza na waandishi wa habari, ambapo alisisitiza umuhimu
wa kujifunza kutoka kwa Vietnam.
Alisema licha ya nchi hiyo kuchukua mbegu ya korosho
nchini, lakini kwa sasa inaongoza duniani kwenye uzalishaji wa zao hilo
duniani.
Alisema mbali na korosho, pia imepiga hatua kubwa
katika kilimo cha mpunga, ambacho kinalimwa mara tatu kwa mwaka wakati hapa nchini,
zao hilo linalimwa mara moja kwa kila mwaka.
Dk. Magufuli aliongeza kuwa, taifa hilo lililopata
Uhuru mwaka 1945 na kupigana vita hadi mwaka 1976, limeweza kupunguza umasikini
kwa asilimia 50, huku pato la wananchi wake likifikia dola za Marekani 2,000,
kutoka dola 100 kwa mwaka.
“Hatupaswi kuona aibu kujifuza katika nchi
zilizotutangulia kimaendeleo, hivyo ujio huu ni fursa muhimu kwa sababu Vietnam
imepiga hatua kubwa hususan kwenye kilimo.
“Licha ya kuwa na ardhi zaidi ya asilimia 80 yenye
kufaa kwa kilimo, lakini bado haijatumika ipasavyo,” alisisitiza.
Kwa upande wake, Rais Truong alisema, Tanzania ni
miongoni mwa nchi za mwanzo kuanzisha mahusiano na Vietnam, katika kipindi cha
harakati za ukombozi.
Alisema Vietnam itahakikisha inashirikiana na
Tanzania kwenye nyanja za ulinzi, biashara, kilimo na ufugaji pamoja na kufanya
mikutano ya mara kwa mara ili kuboresha mahusiano.
Aliongeza kuwa ushirikiano huo utajikita pia katika
kuhamasisha maendeleo, amani na utulivu kwenye mataifa mengine.
Rais huyo pia alitembelea Ofisi Ndogo ya Makao Makuu
ya CCM na kukutana na Mwenyekiti wa CCM, Rais mstaafu Jakaya Kikwete na Katibu
Mkuu wake, Abdulrahman Kinana.
Baada ya mazungumzo yao, Kikwete alisema lengo la
Rais huyo kuitembelea CCM ni kuimarisha uhusiano kati yake na Chama cha
Kikomonisti cha Vietnam.
Alisema vyama hivyo vina uhusiano wa karibu kwa muda
mrefu na kwamba, ipo haja ya kuuendeleza kwa maslahi ya vyama vyote.
Kwa mujibu wa Kikwete, wakati Vietnam ikipigana na
Marekani, vyama vya TANU na ASP, vilifanya kazi kubwa kuwasaidia Wavietnam kwa
kuwapa misaada mbalimbali.
"Vyama vyetu vina uhusiano wa karibu kwa muda
mrefu sana. Wakati ule wakipigana na Marekani, sisi tukiwa vijana, tulikuwa
tukikusanya michango na kuwasaidia mahitaji mbalimbali. Nakumbuka wakati fulani
Rais mstaafu Mzee Benjamin Mkapa ndiye aliyeteuliwa kuifikisha nchini
humo," alisema.
Wakati huo huo, Mke wa Rais, Mama Janeth Magufuli,
amaemkaribisha, mke wa Rais wa Vietnam, Mama Mai Thi Hanl, ambapo alisema ujio
huo utafungua fursa muhimu za kiuchumi.
Alisema Watanzania wanatarajia kupata wawekezaji
kwenye sekta mbalimbali za kibiashara,zitakazosaidia kuiinua kiuchumi.
Baada ya kukaribishwa, Mama Mai Thi Hanl, alieleza
kufurahishwa kwake na ushirikiano wa kihistoria uliodumu zaidi ya miaka 50.
Vilevile, Mama Janeth na mgeni wake, walimtembelea Makumbusho
ya Taifa, ambapo walijionea mambo mbalimbali ya kihistoria.
Leo, Rais Truong anatarajiwa kutembelea Eneo Maalumu
la Uwekezaji (EPZ), Ubungo, Dar es Salaam, kujionea shughuli mbalimbali kabla
ya kwenda Hifadhi ya Taifa ya Saadani.
Kesho Rais Truong na ujumbe wake utaondoka nchini
kwenda Msumbiji kuendelea na ziara.
No comments:
Post a Comment