Sunday 26 June 2016

MAGUFULI AWATAKA POLISI KUDHIBITI MAJAMBAZI NCHINI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akihutubia kwenye uzinduzi wa kituo cha Mawasiliano cha Polisi Call Centre Biafra Kinondoni.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akizindua kituo cha polisi kinachotembea

Jonas Kamaleki, MAELEZO

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli amelitaka jeshi la polisi nchini kuwadhibiti majambazi ipasavyo kwa kuwanyanganya silaha kwenye matukio ya kiuharifu ili kukomesha vitendo viovu katika Taifa.

Rais Magufuli ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa Mpango wa Usalama wa Jamii.

“Inashangaza jambazi anavamia kituo cha polisi anaua na anaondoka wakati polisi wapo na wana silaha na risasi wanazo lakini wanashindwa kumnyang’anya silaha,”alishangaa Rais Magufuli.

Ameongeza kuwa ujambazi na vitendo vya uharifu nchini inabidi vikomeshwe mara moja ili watanzania waishi kwa amani na kufanya maendeleo kwani wananchi wanataka maendeleo.

Akiongelea kuhusu maslahi na vitendea kazi kwa jeshi la polisi, Rais Magufuli amesema kuwa serikali yake itafanya kila iwezalo kuliwezesha jeshi hilo ili liweze kufanya kazi kwa ubora zaidi.

Rais Magufuli ameonyesha kuwa na imani na jeshi la polisi licha ya kuwa na kasoro ndogo ndogo kwa baadhi ya polisi ambao wanalichafua jeshi hilo.

Aidha ametoa agizo kwa TCRA kushirikiana na jeshi la polisi nchini ili kuweza kurekodi simu na kutoa print out mara moja tofauti na ilivyo sasa.

Kuhusu kundi la wafanyakazi wanaofanyakazi kwenye Dawati la Taarifa la polisi, Mhe. Rais amemtaka Mkuu wa Jeshi hilo, IGP Ernest Mangu kuwafikiria na kuwapatia posho ya kazi kwani kazi wanayoifanya ni ngumu mno na inahitaji umakini zaidi.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amemwomba Mhe. Rais kuliongezea fedha jeshi hilo ili liweze kufanya kazi kwa ustadi zaidi na kukomesha vitendo vya uharifu nchini.

Makonda amelipongeza jeshi la polisi kwa kudhibiti matukio ya ujambazi hapa nchini hususan kwenye mabenki.

Mpango huu wa Usalama wa Jamii umezinduliwa leo na utadumu hadi 2019 na unatarajiwa kutoa matokeo makubwa ya kudhibiti uharifu nchini.

No comments:

Post a Comment