Tuesday 28 June 2016

MAJAMBAZI HATARI YAUAWA DAR, YADAIWA KUHUSIKA NA MAUAJI YA MWANZA NA TANGA, YAKUTWA NA MABOMU

JAMBAZI sugu Salum Said, aliyekuwa akituhumiwa kuhusika na mauaji yaliyotokea msikitini mkoani Mwanza, ameuawa wakati wa majibizano ya kurushiana risasi na polisi.

Wakati Said akiuawa baada ya kuwekewa mtego na polisi huku akikutwa na bomu la kurusha kwa mkono, Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, imefanikiwa kumuua mtuhumiwa mwingine wa ujambazi, anayedaiwa kuhusika katika mauaji ya watu wanane yaliyotokea Tanga.

Kamishna wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro, alisema hayo jana, mjini Dar es Salaam, alipozungumza na waandishi wa habari.

Akizungumzia kuuawa kwa Said, Kamishna Sirro alisema mtuhumiwa huyo baada ya kufanya tukio hilo Mwanza, alikimbilia Dar es Salaam.

Alisema polisi wakati wa ufuatiliaji wa mtuhumiwa huyo aliyehusika na mauaji msikitini mkoani Mwanza,  asubuhi ya Juni 27, mwaka huu, maeneo ya Buguruni, kikosi kazi kilimwekea mtego kwa kutumia msiri.

“Alipokaribia kwa msiri huyo, ghafla akagundua kuwa ni askari, hivyo alirusha bomu la mkono na kuanza kukimbia, hivyo polisi walitumia risasi za moto na kufanikiwa kumjeruhi sehemu mbalimbali za mwili wake na kufariki dunia,” alisema Sirro.

Kuhusu mtuhumiwa wa mauaji yaliyotokea Tanga, Kamishna Sirro alisema Juni 25, mwaka huu, polisi katika kanda yake walifanikiwa kuwakamata watu wawili walioonekana kufanya mawasiliano ya mara kwa mara na mtuhumiwa Mohamed Abdallah au Abuu Seif.

Alisema mtuhumiwa Abdallah ndiye mhusika wa kutekeleza mauaji ya watu hao katika kitongoji cha Kibatini, Tanga.

Kamishna Sirro aliwataja watu waliokuwa wakifanya mawasiliano na mtuhumiwa huyo kuwa ni Saada Abdallah (27), mkazi wa Segerea na Maramba Mawili, ambaye ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Udaktari Muhimbili na dereva wa malori wa Kampuni ya TITANIC, Rashid Mangwena (26), mkazi wa Kigogo Mkwajuni.

Alisema watu hao walifuatiliwa baada ya kupatikana kwa taarifa kwamba, mtuhumiwa baada ya kufanya mauaji hayo, alikimbilia Dar es Salaam kama sehemu ya maficho ili kuepuka kukamatwa.

Kamishna Sirro alisema walipohojiwa, watu hao wawili walieleza mahali anapoishi Abdallah, ambaye alikuwa akitafutwa kwa miaka mitano kwa tuhuma za mauaji na unyang’anyi wa kutumia silaha maeneo mbalimbali nchini.

Alisema baada ya polisi kutambua mahali anakoishi mtuhumiwa, Juni 26, mwaka huu, saa mbili usiku, timu iliandaliwa kwa lengo la kuizingira  nyumba ya  Saada, ambaye taarifa zilisema huwa anatembea na bastola  na bomu  la kutupa kwa  mkono.

Kamanda Sirro alisema baada ya askari kuzunguka nyumba hiyo,  ghafla mtuhumiwa  alitoka ndani  ya nyumba  na kuanza kukimbia  huku akiwarushia risasi  askari, kitendo kilichosababisha  askari kuanza kujibu mashambulizi dhidi ya  mtuhumiwa huyo na kufanikiwa kumjeruhi sehemu mbalimbali za mwili  wake.

Alisema baada ya kumkagua mtuhumiwa huyo, alikutwa na bastola aina ya Norinco, iliyofutwa namba, ikiwa  na risasi  tatu ndani ya magazini  na risasi nyingine 19, zikiwa kwenye mfuko wa  suruali aliyokua amevaa na bomu  la kurusha kwa mkono.

Pia, alisema mtuhumiwa huyo  alikuwa anatafutwa kwa muda  mrefu  kwa kujihusisha na matukio ya unyang’anyi  wa kutumia silaha, ikiwemo jaribio la  uvamizi  wa Kituo cha Polisi  Korogwe, mwaka 2013, ambapo walimjeruhi askari polisi mkono.

Matukio mengine  ni uvamizi wa  vituo vya mafuta  na  uporaji  katika maduka  ya Tigopesa  na Mpesa  mkoani Tanga, mauaji  ya watu watano na uporaji  wa fedha Central  Bakery  Tanga,  mauaji ya  askari na uporaji wa silaha  Kituo cha Polisi  Stakishari, Dar es Salaam.

Pia, anadaiwa kuhusika na mauaji ya ya askari wa JWTZ katika mapango ya Amboni na mauaji ya askari polisi maeneo ya TAZARA, Dar es Salaam kisha kufanikiwa kumpora bunduki aina ya SMG.

Mtuhumiwa huyo anadaiwa kujihusisha na kuwaingiza vijana kwenye kundi la kihalifu kwa kuwapa mafunzo ya kijeshi vijana 150.
  
Kamanda Siro alisema polisi wanaendelea kuwasaka watuhumiwa  wengine waliotoroka  kutoka mapangoni  ili kukomesha wimbi la uhalifu nchini.

Wakati huo huo, Polisi  Kanda Maalumu ya Dar es Salaam wamefanikiwa kuwakamata  watuhumiwa wawili, raia wa Uganda,  wakiwa na pembe za ndovu  660 na mashine ya kukatia  pembe hizo.

Watuhumiwa hao ni  Juma Said (54) na  Ally  Sharif (26), ambao  walikamatwa Juni  26, mwaka huu, maeneo ya  Mbezi  Msakuzi, Dar es Salaam.

Sirro  alisema watuhumiwa hao walikamatwa  katika nyumba  ya kupanga waliyokuwa wanaishi   na kukutwa na  pembe hizo.

Kamanda huyo wa polisi aliwataka wamiliki wote wa nyumba kuhakikisha wanakuwa na  picha  za wapangaji wao katika mikataba.


No comments:

Post a Comment