Wednesday 29 June 2016

SERIKALI KUONGEZA VIKOSI VYA ULINZI PEMBA





SERIKALI imesema ni vyema vyama vya siasa kutii amri ya jeshi la polisi ya kutofanya mikutano ya kisiasa, vinginevyo hatua kali zitachukuliwa bila kujali ni chama gani au kiongozi gani aliyehusika.

Mbali ya hilo, imesema  itaongeza vikosi vya ulinzi na usalama katika visiwa vya Pemba ili kuhakikisha kuwa wananchi wanaishi kwa usalama na mali zao.

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Yusuph Masauni, alisema hayo bungeni jana, wakati akijibu swali la Yusuph Salim Hussein (Chambani-CUF).

Alisema kauli iliyotolewa na jeshi la polisi ya kuzuia mikutano hiyo kufanyika ni halali kwani hakuna mtu, ambaye yupo juu ya sheria.

“Polisi ndiyo chombo pekee cha kuangalia ulinzi wa watu na mali zao, hivyo hakutakuwa na mikutano mpaka hapo itakapotoa taarifa nyingine,’’ alisema.

Alisema serikali inatambua kuwa kila inapofika wakati wa uchaguzi mkuu katika kisiwa cha Pemba, baadhi ya watu hujichukulia sheria mikononi kwa kuwapiga wengine na kuharibu mali zao.

Naibu waziri huyo alisema hadi sasa tayari watuhumiwa kadhaa wamekamatwa kutokana na matukio yaliyojitokeza, ikiwemo kuchomwa moto nyumba ya Kamishna wa Polisi Zanzibar.

Alisema kesi mbili zimeshafikishwa mahakamani na zingine zipo kwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) na kumuomba mkurugenzi huyo kuharakisha kesi hizo ili ziende mahakamani.

“Naomba kupitia bunge hili nitoe wito kwa wananchi wote kuacha mihemko ya itikadi za kisiasa wakati na kabla ya uchaguzi kwani hatua kali zitachukuliwa dhidi yao,” alisema.

Katika swali lake, Hussein alitaka kujua iwapo serikali inajua kuwa raia hupigwa na kuharibiwa mali zao, hasa wakati wa uchaguzi kwa upande wa Zanzibar na hatua gani zimechukuliwa.

No comments:

Post a Comment