Friday 15 July 2016

MSAKO NYUMBA KWA NYUMBA WAJA DAR





MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Maonda, ametangaza rasmi kuanza msako mkali wa nyumba kwa nyumba ili kubaini shughuli za kila mkazi mkoani humo.
Aidha, amesema ataliagiza Jeshi la Polisi na Kuiomba Tume ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), kuwachunguza na kuwakamata  viongozi wa serikali za mitaa na yeyote, ambaye atathubutu kuzuia au kukataa kutoa ushirikiano kwa maofisa watakaoendesha sensa hiyo.
Makonda alisema hayo jana, wakati akipokea madawati  30, yaliyotolewa na Serikali ya Mtaa wa Karume, Kata ya Ilala, Dar es Salaam.
Alisema ameshaanza vikao na  wakuu wa wilaya zote  tano za mkoa huo, ambazo ni Ilala, Kinondoni, Temeke, Ubungo na Kigamboni,  ili kukamilisha  mpango huo, aliosema utaanza  muda wowote kutoka sasa.
“Tunaanza operesheni yetu  rasmi ya nyumba kwa nyumba  ili kubaini kila  shughuli anayofanya mkazi wa Dar es Salaam. Tunataka kuwasaidia watu. Kuna watu wanakaa katika nyumba za watu bila shughuli maalumu. Makonda anataka kuwasaidia,”alisema  mkuu huyo wa mkoa.
Aliongeza: “Usikae kwenye nyumba ya mtu kama huna jukumu. Wengine wanapewa mitaji, wanakula halafu wanarudi kuwa mizigo. Ni lazima kila mmoja afanye kazi na tutaandika.”
Alisema amepata taarifa za kuwepo kwa baadhi ya watu, ambao hawatoi ushirikiano kwa viongozi wa serikali za mitaa  wanaofanyakazi ya kuorodhesha kila shughuli katika kaya.
“Si muda mrefu nitaelekeza Jeshi la Polisi na TAKUKURU kuwachunguza na kuwakamata kwa sababu mtu anayezuia  serikali kujua shughuli za watu anaoishi nao, ni lazima  mtu huyo atakuwa na nia mbaya. Ni lazima atakuwa anauza dawa za kulevya, ana danguro,  anajihusisha na magendo au biashara ya binadamu,”alisema Makonda.
“Haiwezekani  ukamzua mwenyekiti wa serikali ya mtaa kujua watu unaoishi nao katika  nyumba yako wakati huyo ndiye mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama katika mtaa. Haiwezekani,” alisisitiza.
Alisema operesheni hiyo itakuwa kubwa na itakuwa ikifanyika usiku na mchana, kwa sababu baadhi ya watu wanapatikana mchana na wengine huonekana usiku.
“Ni lazima tujue kila mtu anafanya nini ili  wale ambao hawana shughuli maalumu, tujue namna ya kuwasaidia. Haiwezekani mtu ukaishi bila shughuli yoyote ya kujiingizia kipato. Nitafuatilia, nitasimamia hadi tuhakikishe operesheni hiyo inafanikiwa,”alisema.
Makonda aliupongeza uongozi wa serikali ya mtaa wa Karume kwa kuwa mtaa wa kwanza nchini  kuchangia madawati.
“Mtaa huu umeandika historia. Tokea tumeanza zoezi la kuchangisha madawati, mtaa huu wa Karume ndiyo wa kwanza kuchangia,”alisema.
Akikabidhi madawati hayo,  Mwenyekiti wa serikali ya mtaa huo,  Haji  Bechina, alisema wameamua kutoa mchango huo ili kuunga mkono  jitihada za Rais Dk. John Magufuli na mkuu huyo wa mkoa.
“Tunatambua jitihada za serikali yetu na juhudi zako binafsi kama mkuu wa mkoa katika kutatua changamoto ya  uhaba wa madawati,”alisema  Bechina.
Diwani wa Kata ya Ilala Sad Kimji, alisema  wanajisikia fahari kutoa madawati hayo kwa sababu ofisi ya mkoa wa Dar es Salaam, iko ndani ya kata  hiyo.

No comments:

Post a Comment