Thursday 2 March 2017

OPERESHENI ONDOA VIROBA MTAANI YAANZA RASMI JIJINI DAR ES SALAAM


Na Lilian Lundo – MAELEZO

Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira ikishirikiana na Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA), Shirika la Viwango Tanzania (TBS) na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)  leo imefanya operesheni kwa baadhi ya wasambazaji wa pombe za kali zinazofungashwa katika plasti maarufu kama kiviroba ili kujiridhisha kama wameitikia wito wa kusitisha utengenezaji, usambazaji na uuzaji wa pombe hizo.

Akiongea na vyombo vya habari Mkurugenzi wa Idara ya Mazingira Ofisi ya Makamu wa Rais, Richard Muyungi amesema kuwa operesheni hiyo imeanza na wasambazaji, wauzaji na watumiaji huku wakiendelea kupitia baadhi ya maombi ya wamiliki wa viwanda juu ya usitishaji wa pombe hizo.

Aidha operesheni hiyo imefanyika katika wilaya za Kinondoni, Temeke na Ilala kwa kutembelea maghala yanayohifadhi pombe hizo ili kujua idadi ya pombe ambazo bado zipo katika maghala hayo pamoja na kufuatilia ikiwa wamiliki wa maghala hayo wametii amri ya kusimamisha usambazaji wa Pombe hizo zilizofungiwa kuanzia Marchi 01, 2017.

Msimamizi wa ghala la Pombe za Viroba  aina ya Kiroba Original lililopo Mabibo wilaya ya Kinondoni  Mhina Rashid amesema kuwa akiba ya pombe hizo za viroba zilizobaki katika maghala yao ni katoni 6600  za ujazo wa Ml 50 na katoni 4909 zenye ujazo wa Ml100.

“Kwa sasa tumefunga maghala na hakuna usambazaji wowote wa pombe aina ya kiroba unaofanyika hapa tunasubiri taratibu za Serikali kujua nini cha kufanya kwa pombe ambazo bado zipo katika maghala,” alifafanua Mhina Rashid.

Aliendelea kwa kusema kuwa ikiwezekana Serikali iongeze muda wa matumizi ya pombe hizo kutokana na kuwa na mzigo mkubwa katika maghala mengi yanayohifadhi pombe hizo.

Kwa upande wake, Afisa Mwandamizi wa Viwango na Mkaguzi wa TBS Banza Suleiman amesema kuwa viroba Original vina nembo ya TBS lakini kutokana na sheria mpya ambayo imepiga marufuku matumizi ya pombe hizo hivyo wasambazaji hawaruhusiwi kusambaza pombe hizo bali wanapaswa kusubiri maelekezo toka Serikalini.

Vilevile operesheni hiyo imefanyika katika kiwanda cha Afro American kilichopo Mwenge ambao ni watengenezaji wa pombe za viroba aina ya Zed, Royal na Dollors na kukuta zaidi ya tani 5 ya pombe hizo.

Msimamizi wa kiwanda hicho Muhandisi Sabra Voleti amesema kuwa wamesimamisha uzalishaji wa pombe za viroba huku wakisubiri maelekezo toka Serikalini. Aidha amesema kuwa kiwanda hicho kinaendelea na uzalishaji wa pombe ambazo vifungashio vyake ni vya chupa.

Kwa upande wake Mwanasheria wa NEMC Manchare Heche Suguta amesema kuwa adhabu ya matumizi ya vifungashio vya plastiki (Viroba) vinatofautiana kati ya mtengezaji, msambazaji, muuzaji na mtumiaji. Aidha adhabu yake ni faini kati ya shilingi elfu 50 na Milioni 5 au kifungo kisichopungua miaka 3.

Hivyo amewataka watanzania kujiepusha na matumizi ya pombe hizo pamoja ikiwa ni pamoja na utengenezaji na usambazaji wake.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Manyara Februari, 2017 aliagiza pombe hizo kutoendelea kutumika kuanzia Marchi 1, 2017.

No comments:

Post a Comment