Sunday 16 April 2017

MAJAMBAZI WALIOA ASKARI KIBITI WAUAWA




MAJAMBAZI wanne wanaodaiwa kushiriki katika tukio la mauaji ya askari wanane, ambao waliporwa silaha saba, zikiwemo aina ya SMG, katika maeneo ya Mkengeni wilayani Kibiti, mkoani Pwani, wameuawa huku silaha nne zikipatikana, zikiwemo mbili zilizoibwa kwa askari hao.
Kutokana na mwendelezo wa matukio ya ujambazi katika eneo hilo, Jeshi la Polisi nchini, limesema  linakwenda katika operesheni ya moto, ambayo haina mwisho, hivyo kuanzia sasa eneo hilo la tukio, Mkuranga, Kibiti na Rufiji marufuku kuendesha pikipiki zaidi ya saa 11 jioni.
Wakati jeshi hilo likitoa taarifa hiyo jana, Rais Dk. John Magufuli ametuma salamu za rambirambi kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Ernest Mangu na kuwataka Watanzania wote kutoa ushirikiano ili kukomesha vitendo vya kuwashambulia polisi, ambao wanafanya kazi kubwa na muhimu ya kulinda raia na mali zao.
Kamishna wa Operesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi, Nsato Marijani, alisema majambazi hao waliuawa kutokana na hatua za kiintelejensia na kiupelelezi, zilizochukuliwa, ambapo askari waliweza kufuatilia na kubaini maficho yao ya muda  baada ya kuwaua wenzao  waliokuwa wakitoka lindo.
“Katika  majibizano ya risasi kati ya polisi na watuhumiwa hao,  majambazi wanne waliuawa na bunduki nne kupatikana, mbili zikiwa zilizoibwa katika tukio la Mkengeni na nyingine mali za majambazi hao,” alisema Kamishna Marijani, wakati akitoa taarifa ya jeshi hilo kutokana na mauaji ya askari hao wanane.
Kamishna Marijani aliwataja askari waliofariki katika tukio hilo, wakiwa wanatoka kubadilishana lindo na kupigwa risasi katika barabara ya Dar es Salaam- Lindi kuwa ni Mrakibu Msaidizi Peter Kigugu, F. 3451 CPL Francis, F. 6990 PC Haruna, G. 3247 PC Jackson, H. 1872 PC Zacharia, H. 5503 PC Siwale, H. 7629 PC Maswi na H. 7680 PC Ayoub.
“Tukio hili la kuuawa askari ni baya sana. Ni kitendo ambacho hakikubaliki na mpaka sasa askari zaidi ya 10, wamepoteza maisha, hivyo inatosha, tutawasaka popote walipo kwa kuwa dawa ya moto ni moto,” alisema.
Alisema tukio hilo la juzi, lilitokea saa 12.15 jioni, maeneo ya Mkengeni, Kata ya Mjawa, wilaya ya Kibiti mkoani Pwani, ambapo majambazi, ambao idadi yao haijafahamika, wakiwa na silaha za moto, walilishambulia kwa risasi gari la polisi lenye namba PT. 3713, aina ya Toyota Land Cruiser na kuwaua askari wanane na kumjeruhi mmoja.
Alisema majambazi hao walifanikiwa kuwaua askari hao, baada ya kuweka mtego na kuanza kushambulia gari walilokuwa wamepanda, eneo hilo ambalo hakuna makazi ya watu.
Alisema majambazi hao waliwaua askari hao wanane na kumjeruhi mmoja, huku wakifanikiwa kupora silaha saba, zikiwemo SMG nne na Long Range tatu.
Kamishna Marijani alisema jeshi hilo sasa linakwenda katika operesheni maalumu na halitakuwa na mzaha wala msamaha, bali litafanya kile ambacho kinatakiwa kufanywa.
“Tutawafuata popote walipo, tutawashughulikia kikamilifu, hakuna atakayepona. Mapambano haya hayana mwisho.  askari wetu zaidi ya 10, waliopotea ni wengi sana, wananchi tunaomba mtuwie radhi, mtuunge mkono katika hili,” alisema.
Aidha, aliwaomba wananchi kutoa taarifa kuliwezesha jeshi hilo kuchukua hatua stahiki, huku akiwataka wanaofanya ujambazi wa kutumia silaha, kujua kuwa dawa ya moto ni moto.
JPM alaani mauaji ya askari
Rais Dk. Magufuli ameeleza kusikitishwa kwake na kifo cha askari hao, huku akiwataka Watanzania wote kutoa ushirikiano ili kukomesha vitendo vya kuwashambulia polisi, ambao wanafanya kazi kubwa na muhimu ya kulinda raia na mali zao.
"Nimeshtushwa na nimesikitishwa sana na vifo vya askari wetu
wanane, ambao wamepoteza maisha wakiwa wanalitumikia Taifa, "
alisema Rais Magufuli katika salamu zake za rambirambi kwa IGP  Mangu.
Dk. Magufuli alisema anaungana na familia za marehemu wote, Jeshi
la Polisi na Watanzania wote katika kipindi hiki kigumu cha huzuni na majonzi ya kuondokewa na vijana hao shupavu.
Rais Magufuli alituma salamu za rambirambi kwa IGP Mangu, familia za askari wote waliouawa, polisi wote na Watanzania wote walioguswa na vifo hivyo.
“Namuomba Mwenyezi Mungu atupe moyo wa subira, uvumilivu na ustahimilivu,” alisema.
Magufuli amelaani tukio hilo na matukio yote ya kuwashambulia polisi, ambao wanafanyakazi kubwa na muhimu ya kulinda raia na mali na amewataka Watanzania wote watoe ushirikiano katika
kukomesha vitendo hivyo.
CCM yawalilia polisi waliouawa
Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimetoa salamu za pole kwa Mwenyekiti wa Chama hicho, Rais Dk. John Magufuli, kutokana na mauaji ya askari hao.
Salamu hizo ziliwasilishwa jana, kwa Rais Magufuli na Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Humphrey Polepole, Ikulu, jijini Dar es Salaam.
Akiwa ameambatana na Naibu Katibu Kuu wa CCM Tanzania Bara, Rodrick Mpogolo na Katibu wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Amina Makilagi,  Polepole alisema, kwa kuwa Mwenyekiti wa CCM ndiye Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama,  ndio maana CCM imestushwa na tukio hilo na kutoa pole hizo.
Alisema vifo hivyo vinasikitisha,  kwa kuwa askari hao wamekuwa na jukumu kubwa la kulinda usalama wa wananchi na mali zao .
Alisema askari hao wamekuwa wakifanya kazi katika mazingira magumu wakati wote ili kuhakikisha Watanzania wanakuwa salama pamoja na mali zao, hivyo tukio la kuuawa kwao ni jambo la kusikitisha sana.
Aidha, Polepole alisema wamekutana na Rais Magufuli kumueleza mchakato wa uchaguzi wa ndani wa CCM, ambao unaendelea nchini kote kuanzia ngazi ya mashina hadi taifa.
Alisema CCM inampongeza Rais Dkt.Magufuli kwa kitendo cha kizalendo cha serikali ya awamu ya tano,  kutumia fedha zake za ndani katika ujenzi wa reli, itakayokuwa na kiwango cha kimataifa, yenye urefu wa kilomita 300, kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro.
Alisema ujenzi wa reli hiyo yenye kiwango cha kimataifa, itakayotumia treni ya umeme, unadhihirisha jinsi CCM inavyojishughulisha na shida za watu.
Zitto, ACT nao walaani 
Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe, ameelezea hisia zake kutokana na mauaji ya askari hao kupitia ukurasa wake wa twitter, ambapo amesema ni muhimu sasa JWTZ waingie kwenye operesheni kwenye eneo hilo.
“Salamu za pole kwa familia za askari wetu. Ni muhimu sasa  JWTZ waingie kwenye operesheni maalumu kwenye eneo hili. Nipo pamoja askari wetu,” alieleza Zitto kupitia ukurasa wake huo.
Wakati huo huo, Chama cha ACT Wazalendo kimewataka Watanzania kutoa ushirikiano kwa vyombo vya ulinzi na usalama ili kuhakikisha matendo ya namna hiyo yanakomeshwa.
Chama hicho kilieleza hayo kupitia taarifa iliyotolewa na Katibu, Kamati ya Amani na Usalama, Mohammed Said Babu, ambaye ilieleza kuwa, chama hicho kimepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya kushambuliwa na kuuawa kwa askari hao.

“ACT Wazalendo tunaungana na wito wa kuwataka Watanzania kushikamana na vyombo vya ulinzi na usalama katika kipindi hiki cha majonzi kwa Taifa na kutoa ushirikiano kwao kuhakikisha matendo ya namna hii yanakomeshwa.

“Tunachukulia kitendo hiki kama cha shambulio dhidi ya Jamhuri yetu na hatua kali na madhubuti zinapaswa kuchukuliwa. ACT Wazalendo tunaamini Jeshi letu la Polisi litahakikisha linawasaka, kuwakamata na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria wote waliohusika na mauaji haya ya askari wetu,” alisema.

Babu alisema mlolongo wa matukio ya namna hii unaonyesha kuwa, nchi inapambana na kundi lisilo la kawaida, hivyo weledi wa hali ya juu unatakiwa katika kukabiliana na tishio hili.

Pia, alisema Jeshi la Polisi linatakiwa kufanya kazi zake kwa uangalifu mkubwa na kuepuka kabisa kuwaingiza raia wasio na hatia kwenye mateso yeyote kwa kuwa adui asipopatikana, madhara yake ni makubwa zaidi.

“Matukio ya aina hii katika miezi ya hivi karibuni yawe funzo katika kukabiliana na uhalifu kama huu. Tunatahadharisha kutotumia mwanya huu kuingiza wasiohusika kwa kuwa kufanya hivyo ni kuwapa ushindi wahalifu,” alisisitiza. 

No comments:

Post a Comment