Monday 17 July 2017

JPM AMTUMIA SALAMU ZA RAMBIRAMBI DK. MWAKYEMBE





RAIS Dk. John Magufuli, amemtumia salamu za rambirambi Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Harrison George Mwakyembe, kufuatia kifo cha mkewe, Linah.
Linah, alifariki usiku wa kuamkia juzi, katika Hospitali ya Aga Khan, jijini Dar es Salaam, alikokuwa akipatiwa matibabu.
Katika salamu zake, Rais Dk. Magufuli ameelezea kushtushwa na kusikitishwa na kifo hicho.
Alisema yeye pamoja na familia yake wanaungana na familia ya Dk. Mwakyembe katika kipindi hiki kigumu cha majonzi.
“Nakupa pole Dk. Mwakyembe kwa kuondokewa na mkeo mpendwa Linah, natambua hisia za maumivu ulizonazo wewe na familia nzima, nyote nawaombea Mwenyezi Mungu awatie nguvu, awape subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha majonzi.
“Namuombea marehemu Linah George Mwakyembe, apumzishwe mahali pema peponi,”alisema.
Wakati huo huo, Dk. Magufuli jana, alisali Ibada ya Jumapili ya 15 ya mwaka wa Kanisa, iliyofanyika katika Kanisa la Bikira Maria Parokia ya Chato, mkoani Geita na aliendesha hafla ya kuchangia ujenzi wa kanisa hilo.
Katika hafla hiyo, Dk. Magufuli, ambaye aliongozana na mkewe Mama Janeth, alifanikiwa kuchangisha sh. milioni 13, ahadi sh. 920,000, mifuko ya saruji 33 na malori mawili ya mchanga.
Rais Dk. Magufuli aliwapongeza waumini wa Parokia ya Chato kwa hatua kubwa waliyopiga katika ujenzi wa Kanisa Kuu la Parokia hiyo na aliwataka waendelee kujitolea ili kukamilisha hatua ya mwisho ya ujenzi huo.

No comments:

Post a Comment