Monday 17 July 2017

CCM YAITIKISA CHADEMA NYUMBANI KWA MBOWE





NA WILIUM PAUL, HAI
WAKATI bundi akiendelea kukitafuna Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kutokana na kukimbiwa na viongozi wake, Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimeitikisa ngome ya mwenyekiti wa chama hicho taifa, Freeman Mbowe, baada ya wanachama zaidi ya 200 kurudisha kadi na kujiunga na CCM.
Wanachama hao walioongozwa na aliyekuwa Mwenyekiti wa CHADEMA katika Kijiji cha Mijongweni, Hasan Hamisi,  walirudisha kadi zao jana na kukabidhiwa za  CCM.
Tukio hilo lilitokea katika kikao cha Chama, kilichofanyika kijijini hapo, wilayani Hai,  ikiwa ni hitimisho la ziara ya Katibu wa NEC, Siasa na Uhusiano wa Kimataifa, Kanali Ngemela Lubinga, mkoani Kilimanjaro.
Akizungumza mbele ya wana-CCM, baada ya kurejesha kadi yak, Hamisi alisema tangu ashike nafasi hiyo kwa miaka mitano, hakuna faida yoyote ya maendeleo iliyotekeleza na chama hicho.
Hamisi alisema sababu zilizosababisha aamue kuhamia CCM ni kutokana na kuridhishwa na kazi nzuri inayofanywa na serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dk. John Magufuli.
“Nimeamua kurudi CCM baada ya kuvutiwa na kazi nzuri inayofanywa na Chama Cha Mapinduzi. Wametambua vilio vya wananchi na kuamua kuvifanyia kazi kwa vitendo bila kujali kipato cha mtu. Wananchi walio na kipato cha chini ndilo hitaji lao kubwa,” alisema.
Alisema  sababu nyingine ni kutokana na utawala bora uliopo ndani ya  CCM pamoja na kuwepo viongozi wenye uchu wa kuwaletea wananchi maendeleo.
Hamisi alidai kuwa, viongozi wa CHADEMA hawapo kwa ajili ya kuwatumikia Watanzania, bali wapo kwa ajili ya maslahi yao binafsi.
Alisema hakulazimishwa wala kufuatwa na viongozi wa CCM ili kumshinikiza ajitoe CHADEMA, bali alifanya hivyo kwa mapenzi yake na kuwataka viongozi wa upinzani, kuachana na siasa za propaganda za kudai CCM  imekuwa ikiwafuata viongozi wao na kuwahujumu.
Mara baada ya kuwapokea wanachama hao, Kanali mstaafu Lubinga, alisema CCM ni chama kinachojitambua na kushughulikia matakwa ya wananchi wake kwa vitendo, bila kujali hali ya kipato chao.
Kanali Lubinga alisema katika kudhihirisha hilo, serikali ya awamu ya tano imeanza kuwashughulikia mafisadi walioko katika serikali na kwamba, wapo baadhi ya mafisadi walioko katika Chama na kuwataka wajiandae kwani hawapo salama.
Aliwataka wananchi wa jimbo la Hai, wanapokwenda katika nyumba za ibada kusali, wakumbuke kumuombea mbunge wao ili aweze kurudi na kusikiliza kero zao na kuzifutia ufumbuzi, badala ya kukaa Dar es Salaam muda wote na kula bata.
LAIZER: CHADEMA INAANDIKA TAARIFA ZA UONGO
ALIYEKUWA Diwani wa Kata ya Ngabobo (CHADEMA), wilayani Meru mkoani hapa, Solomon Laizer, amekitaka chama hicho kuacha kuandika taarifa za uongo kwenye mitandao ya kijamii dhidi yake.
Laizer, alijiuzulu nafasi hiyo wiki iliyopita na kuhamia Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Akizungumza na  gazeti hili jana, Laizer alisema taarifa iliyotolewa na Katibu wa CHADEMA, Kanda ya Kaskazini, Aman Golugwa, kwenye mkutano wake na waandishi wa habari na baadaye kurushwa katika  mitandao ya kijamii, kwamba barua yake ya kujiuzulu hakuandika yeye wala kutia saini, ni za uongo na kuwataka wananchi wazipuuze.
Kwa mujibu wa Laizer,  aliandika barua hiyo akiwa na akili timamu , nyumbani kwake Ngabobo na kuiwasilisha kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Meru,  Chirstopher Kazeri,  Julai 9, mwaka huu.
"Taarifa inayosambaa kwenye mitandao ya kijamii ya katibu wa CHADEMA kanda ya Kaskazini dhidi yangu sio za kweli, sijafanya kikao na CHADEMA na barua yangu ya kujiuzulu nimeandika pekee yangu na kutia saini yangu, kisha kuiwasilisha kwa mkurugenzi wa Meru kwa mkono wangu mwenyewe,"alisema.
Laizer alisema alifanya maamuzi ya kuondoka CHADEMA na kujiunga na CCM kwa utashi wake, baada ya kuona kazi nzuri inayoyofanywa na Rais Dk.John Magufuli.
"Nilitafakari nikaona nchi ilikuwa inahitaji Rais mzalendo na Mungu ametupa Rais Magufuli, ambaye amejitoa mhanga kutetea rasilimali za nchi zilizokuwa zinawanufaisha watu wachache pamoja na kutatua kero mbalimbali za wananchi wanyonge. Haya yote tulikuwa tunayahitaji kwa nini nisimuunge mkono?” Alihoji.
Alisema aliamua kuachana na CHADEMA na kurudi CCM ili aweze kumuunga mkono Rais Magufuli kwa utendaji wake uliotukuka hasa wa kuwashughulikia mafisadi, ambao walikuwa wanatumia rasilimali za nchi vibaya.
"Ninampenda Rais wangu Magufuli, nimeamua kurudi CCM, sioni sababu ya kuendelea kubaki CHADEMA. Ili niweze kuunga mkono na kumuombea aendelee kututumikia sisi wananchi wanyonge, nimeamua kurejea CCM,"alisema.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Meru,  Kazeri alikiri kupokea barua ya Lazeir, Julai 9, mwaka huu na kwamba, ameshaindikia Tume ya Taifa ya Uchaguzi.

No comments:

Post a Comment