Thursday 20 July 2017

KESI YA KIGOGO WA TRA ALIYEPATA MGAWO WA ESCROW AGOSTI 17


KESI ya kuomba na kupokea rushwa kupitia akaunti ya Tegeta Escrow, inayomkabili aliyekuwa Meneja Misamaha ya Kodi  wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Kyabukoba Mutabingwa, imepangwa kuanza usikilizwaji wa awali Agosti 17, mwaka huu.

Mutabingwa, alipanda kizimbani jana, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbrad Mashauri.

Wakili wa Serikali, Adolf Mkini, aliiomba mahakama kuipangia kesi hiyo tarehe kwa ajili ya kumsomea mshitakiwa maelezo ya awali.

Hakimu Mashauri aliahirisha kesi hiyo hadi Agosti 17, mwaka huu, kwa usikilizwaji wa awali na kusema kuwa, dhamana ya mshitakiwa inaendelea.

Kwa mujibu wa hati ya mashitaka, mshitakiwa huyo anadaiwa Januari 27,2014,  katika benki ya Mkombozi, iliyoko wilayani Ilala, Dar es Salaalam, alipokea sh. bilioni  1.6, kupitia akaunti namba 00110202613801, kutoka kwa James Rugemalira, ambaye ni Mshauri huru wa kitaalamu, Mkurugenzi wa VIP na Mkurugenzi wa zamani wa IPTL.

Inadaiwa mshitakiwa alipokea kiasi hicho cha fedha kama tuzo, kwa kuiwakilisha mahakamani Kampuni ya  Mabibo Beer Wines and Spirits, ambayo ni mali  ya Rugemalira, kitu ambacho ni kinyume cha sheria.

Katika shitaka lingine, mshitakiwa huyo anadaiwa Julai 15,2015, akiwa  katika benki hiyo ya Mkombozi, alipokea rushwa ya sh. milioni 161.7.

No comments:

Post a Comment