Thursday 20 July 2017

MTUMISHI ATAKAYETOA SIRI ZA SERIKALI KUKIONA CHA MOTO


SERIKALI  imetahadharisha kuwa, mtumishi wa umma atakayetoa siri za serikali na kuzisambaza kwenye mitandao ya kijamii, atafikishwa  mahakamani na kuhukumiwa kifungo cha miaka 20.

Waziri wa Nchi Ofisi  ya Rais, Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angella Kairuki, alisema hayo juzi, alipokuwa akifungua mkutano wa watumishi wa umma wa Manispaa  ya Ubungo.

Alisema mtumishi atayejihusisha na usambazaji wa taarifa  za serikali, atachukuliwa hatua za kisheria, ikiwa ni pamoja na kufikishwa mahakamani na kuhukumiwa kifungo cha miaka 20 jela.

Kwa mujibu wa  Angella, serikali  inao utaratibu wa kuupasha umma taarifa zake mbalimbali na pia kutoa machapisho yake kwa jamii.

Alisema watumishi wa umma wanaojihusisha na utoaji wa taarifa za serikali  na kuzisambaza kwenye mitandao, wanafanya kinyume cha sheria.

“Hivi mtumishi unaposambaza taarifa za serikali, ambazo ni  siri, unakuwa  na lengo gani. Na utakapojulikana kuwa wewe ni chanzo, utajisikiaje? Ni vyema kuiacha serikali ifanyekazi zake kwani inao utaratibu wa kuupasha umma.

"Maadili ya  utumishi wa umma na  usalama wa taifa hayaruhusu mtumishi wa umma kutoa taarifa au siri za serikali na kuzisambaza kwenye mitandao ya kijamii, mtu akibainika kufanya hivyo, atafukuzwa kazi au kifungo cha miaka 20 jela,” alisema.

Angella aliwataka watumishi hao kuhakikisha  kuwa, wanafuata kanuni na sheria za utumishi wa umma ili kujiepusha  na vitendo visivyofaa  kwa taifa.

Pia, aliwaasa  watumishi hao kuhakikisha wanatoa ushirikiano katika  mapambano dhidi  ya rushwa.

Mkutano huo uliwakutanisha watumishi wa umma takriban 600 wa Manispaa ya Ubungo, ukiwa na lengo la kuwapa miongozo mbalimbali ya utumishi  wa umma.

No comments:

Post a Comment