Thursday 20 July 2017

MASAUNI AMTUMBUA KAMANDA WA USALAMA BARABARANI PWANI


NAIBU Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi, Hamad Yusuph Masauni, amemuondoa kazini Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani (RTO), Abdi Issango, kutokana kuzembea kutekeleza  maelekezo aliyopatiwa na wizara kipindi kilichopita.

Issango anadaiwa kushindwa kusimamia mkakati wa serikali wa kudhibiti makosa ya usalama barabarani yanayosababisha ajali.

Aidha, Masauni ametoa maelekezo kwa Kamanda wa Polisi mkoani Pwani, kuhakikisha mkuu wa kitengo cha usalama barabarani mwingine atakayeteuliwa, afanyekazi ipasavyo na kama kuna changamoto, wazieleze ili ziweze kutatuliwa. 

Masauni pia ameitoa siku tatu kwa askari wa usalama barabarani, kuhakikisha wanawakamata madereva wa bodaboda, ambao wanakiuka sheria za usalama barabarani.

Masauni alitoa msimamo huo jana, kwenye Stendi ya Maili Moja, wakati wa ziara ya kutembelea utendaji kazi wa askari wa kikosi cha usalama barabarani.

Alisema wameanza kula sahani moja na watendaji wazembe na wale wasiokwenda na kasi ya serikali ya awamu ya tano.

Masauni aliwataka makamanda wengine wa usalama barabarani katika wilaya na mikoa, ambao hawawajibiki, wajiandae kuchukuliwa hatua kama hiyo.

Alisema askari ama mtumishi yeyote aliye chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, ajitume kikamilifu kwani serikali haitawavumilia wasioweza kutimiza majukumu yao.

No comments:

Post a Comment