Thursday 20 July 2017

TUNDU LISSU ASHAMBULIWA KILA KONA

BAADHI ya wasomi na wanasiasa nchini, wamemjia juu Mwanasheria Mkuu wa CHADEMA, Tundu Lissu, kutokana na kauli yake dhidi ya serikali.

Juzi, Lissu aliiomba jumuia ya kimataifa kuinyima misaada Tanzania, kwa
madai kuwa kuna ukiukwaji wa kidemokrasia.

Wakizungumza na Uhuru, jana, mjini Dar es Salaam, walisema kuwa maneno anayozungumza Lissu ni ya kiuchochezi na yana lengo la kuigombanisha serikali na Watanzania.

Akizungumzia kauli hiyo ya Lissu, aliyekuwa Mbunge wa Kasulu Mjini (NCCR-Mageuzi), Moses Machali, alisema kauli iliyotolewa na mwanasheria huyo inatakiwa kupingwa kwa nguvu zote.

“Huyu anataka Watanzania wakumbwe na matatizo kwa sababu tu yeye na CHADEMA yake waweze kunufaika kisiasa,” alisema.

Machali alisema kwa mtu yeyote mwenye akili timamu, kamwe hawezi kuunga mkono vitendo vya Lissu, kuzichochea jumuiya za kimataifa zisiisaidie Tanzania.

“Huu ni upuuzi. Vilevile huo ni uchochezi. Ni wazi Lissu na wenzake wanaounga mkono, wanaweza kuwa vibaraka wa watu wasioitakia mema nchi yetu,” alisema.

Mkuu wa Chama cha Alliance For Democrat Change (ADC), Rantis Doyo aliitaka CHADEMA iombe radhi kwa Watanzania kutokana na matamshi yaliyotolewa na Lissu.

Pia, alisema chama hicho kimeonekana wazi kuwa, kimeshindwa kupambana na Chama Cha Mapinduzi (CCM) na serikali yake iliyoko madarakani, ndiyo maana kinatapatapa.

Doyo alisema mwanasiasa, ambaye ni mwanasheria hakutakiwa kutoa maneno ya kuwakatisha tamaa Watanzania.

Pia, alisema ADC imeshtushwa na kauli hiyo ya kinyama, hivyo inaitaka CHADEMA itoe tamko la kuwaomba radhi Watanzania.

"Watanzania wanataka kujua kauli aliyotoa Lissu ni ya kwake au ni msimamo wa chama chake?” Alihoji.

Vilevile, alisema kauli zilizotolewa na mwanasheria huyo ni za kinyama na inaonekana wazi kuwa chama hicho hakiwatakii mema Watanzania.

Doyo alimtaka mwanasheria huyo kupambana na kupigania demokrasia kuliko kutangaza ugomvi wake kwa mtu asiyehusika, kitendo alichokielezea kuwa, kimeonyesha udhaifu mkubwa kwa kiongozi.

"Kwa mtu aliye makini na anayejua anachokifanya, kamwe ugomvi wake wa ndani hawezi kuupeleka nje kwa mtu mwingine.

"Kwa kauli hizi za CHADEMA, ni wazi wameshindwa mapambano ya ndani  na sasa wanafikiri njia nyingine, ambazo ni hatari zaidi katika nchi yetu," alisema Doyo.

Aliongeza kuwa kuna haja ya serikali kuzipima kauli za CHADEMA kwa uzito unaostahili na kwamba, chama hicho kinaweza kuitia nchi katika matatizo yasiyoweza kuzuilika.

Kutokana na kauli hiyo ya Lissu, katika ukurasa wake wa Twitter, Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe aliandika: “Huu ni uhayawani, hii ni nchi huru.”

“Kukaribisha wageni kuingilia mambo yetu ni upuuzi na umazwazwa. Tupambane ndani kuleta demokrasia.”

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Benson Banna, alisema Lissu anachanganya masuala ya siasa na uanaharakati, ndiyo maana anaongea maneno ya kuvuka mipaka.

"Lissu ni msomi, lakini hajaelimika. Kwa mtu kama yeye, ambaye ni kiongozi, hawezi kutamka matamshi ya kuwavunja moyo Watanzania," alisema.

Dk. Banna alisema ni vizuri mwanasheria huyo akaguliwe uraia wake kwa sababu Mtanzania halisi lazima awe na uchungu wa nchi yake pamoja na Watanzania wenzake.

"Demokrasia ya Tanzania inaeleweka na ina upana wake, lakini demokrasia sio kupayuka mambo yasiyofaa na ambayo hayatawasaidia kitu chochote Watanzania,” alisema.

Pia, alisema kutafuta madaraka sio kupayuka maneno ya kuchefua watu, inatakiwa kuongea busara.

Kwa upande wake, Mwalimu Shiganga Geogre, alisema kila mtu ana haki ya kuzungumza na kutoa maoni yake kwa manufaa ya nchi au kitu.

"Matamshi aliyoyatoa Lissu hayana mashiko yoyote kwa nchi ya Tanzania zaidi ya uchonganishi,” alisema.

Alisema Watanzania hivi sasa wameelimika, hivyo wanasiasa wasitumie nguvu kubwa ya kuwadanganya vitu ambavyo havina faida kwao.

Msemaji Mkuu wa Serikali, Dk. Hassan Abbasi, alitolea ufafanuzi kuhusu propaganda na upotoshaji wa Lissu na kumshauri atekeleze wajibu wake wa kusimamia weledi, badala ya kila wakati kuyatazama mambo kwa jicho la siasa.

Dk. Abbasi alisema madai ya kuwa serikali inakandamiza demokrasia ni propaganda za kisiasa.

Alisema Lissu anaonekana kuchanganya kati ya haki katika demokrasia, ambazo hata yeye (Lissu) amezitumia kuongea na wanahabari bila tashiti kwa upande mmoja na misingi ya wajibu kwa upande mwingine.

Habari zaidi kutoka Dodoma, zimeeleza kuwa, Lissu, jana, aling’angania ndani ya  Mahakama ya Wilaya ya Dodoma, akihofia kukamatwa na polisi nje ya mahakama ili apelekwe Dar es salaam.

Lissu, alikuwepo katika mahakama hiyo baada ya kuahirishwa kesi ya Chama cha Walimu (CWT) Manispaa ya Dodoma.

Katika kesi hiyo, Lissu alikuwa wakili wa utetezi upande wa viongozi wapya wa chama hicho, ambao wanatuhumiwa kufuja fedha na mali za chama hicho.

Akizungumza baada ya kuahirishwa kwa kesi hiyo, Lissu alisema amepata taarifa za kutaka kukamatwa kupitia ujumbe mfupi aliotumiwa na mkewe kutoka Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment