Tuesday 18 July 2017

WAUMINI WAWILI WAFARIKI WAKATI WA UBATIZO


WATU wawili waumini wa Kanisa la Siloamu, lililoko Manda Kilesi, kijiji cha Keni, wamefariki dunia wakati wakiwa wanabatizwa katika Mto Ugwasi, wilayani Rombo, mkoani Kilimanjaro na kuzua taharuki kwa wananchi.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa Polisi mkoani Kilimanjaro, Hamisi Issah, alisema tukio hilo lilitokea Jumapili, iliyopita, ambapo marehemu hao walizama katika maji yenye kina kirefu wakati wa kubatizwa.

Kamanda Issah alisema wakati waumini hao wakiwa katika ibada ya ubatizo na waumini wengine, ndipo walipozama katika maji hayo na kukosa msaada, hali iliyosababisha vifo vyao.

Aliwataja waliofariki kuwa ni Gasper Utoh (47), mkulima na mkazi wa kijiji cha Makiidi na Proches Mrema (30), mkulima na mkazi wa kijiji cha Manda Chini na kwamba,  watu watatu na mchungaji wa kanisa hilo wanashikiliwa na polisi.

Kamanda huyo alidai wanawashikilia watu hao watatu, akiwamo mchungaji kiongozi wa kanisa hilo, kwa tuhuma za kuhusika na mauaji ya waumini wao.

“Tunawashilia watu watatu, wkiwemo Mchungaji wa Kanisa la Siloamu kutokana na vifo vya waumini wake wawili wakati wa ibada ya ubatizo aliyokuwa akiendesha katika Mto Ugwasi, wilayani Rombo,”alisema.

Aliwataja wanaoshikiliwa kuwa ni Faida Upendo (35), mkazi wa kijiji cha Makiidi, ambaye ni mchungaji wa kanisa hilo, Akili Elia (37), mkazi wa Manda na Philbert Shirima (27), mkazi wa Kijiji cha Keni.

No comments:

Post a Comment