Monday 25 September 2017

DAKTARI BINGWA AMUONYA MANJI




DAKTARI bingwa wa magonjwa ya moyo na tiba kutoka Hospitali ya Aga Khan, Mustapha Bapumia, ameelezwa kushangazwa na mfanyabiashara Yussuf Manji kuwa na vyuma kwenye moyo akiwa na umri mdogo.
Amedai kuwa kutokana na hilo, kitaalamu Manji anatakiwa ajiangalie sana kwa kuwa yupo kwenye hatari na kama anatembea kwenye kamba nyembamba.
Dk. Bapumia alidai hayo jana, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi, Cyprian Mkeha, alipokuwa akitoa ushahidi kwa upande wa Manji, anayetuhumiwa kutumia dawa za kulevya.
Akiongozwa na Wakili wa Manji, Hajra Mungula, kutoa ushahidi, Dk. Bapumia alidai alikutana na mshitakiwa huyo, Februari 21, mwaka huu, ambapo alipelekwa hospitalini hapo akiwa na maumivu ya moyo.
Alidai akiwa na timu yake, walimpokea ambapo tatizo la moyo kwa Manji ni sugu pamoja na umri wake mdogo.
Shahidi huyo alidai alipata historia ya Manji, kwamba alizibuliwa mishipa yake ya damu India, Dubai na Marekani na mishipa mitatu tayari ilikuwa imerekebishwa.
Alidai walimshauri Manji wazibue mshipa, lakini aliwaeleza waiache kwa sababu familia yake iko Marekani na matibabu yake hufanyika huko, hivyo aliomba apatiwe dawa.
Shahidi huyo alidai walimwandikia Manji, atumie dawa nne, ambazo ni za kupunguza koresto, hofu na kama usingizi tatizo na maumivu sugu ya mgongo.
Alidai Manji aliruhusiwa kutoka hospitalini hapo, Machi 14, mwaka huu, na siku hiyo hiyo saa mbili usiku, alirudishwa tena hospitalini hapo, ambapo alilazwa na aliwapa ridhaa wakaingia kurekebisha chuma.
Alidai kwa wagonjwa wenye matatizo ya moyo, hupewa dawa zenye morphine kwa ajili ya kupunguza maumivu makali.
Manji aomba mahakama imuachie huru
Akitoa ushahidi wake, Manji aliiomba mahakama imuachie huru huku akidai kuwa, dawa anazotumia kutokana na matatizo ya afya yanayomkabili, zina kiwango kidogo cha morphine na benzodiazephine.
Manji (41), ambaye kwa sasa ni mshauri wa kampuni za familia, alidai mara ya kwanza aliposomewa mashitaka mahakamani hapo, alikataa kwa kuamini kwamba angepata nafasi ya kusilizwa ili iweze kutoa uamuzi wake.
Alidai morphine na benzodiazephine ni sehemu ya dawa zake, lakini aliona apate nafasi ya kusikilizwa. Manji alidai tuhuma hizo zimemchafua yeye binafsi na kibiashara.
Manji alidai anatumia dawa za aina tano na kwamba, amekuwa analetewa uthibitisho na daktari wake kutoka Marekani na mara ya mwisho kwenda Marekani ni Januari, mwaka huu.
Akielezea historia yake kiafya, Manji alidai ana matatizo ya moyo, ambayo ni ya kurithi kutoka kwenye familia yake kwani baba na babu yake walikuwa nayo.
"Nilianza kusumbuliwa tangu nina umri miaka 26 na ripoti zangu zipo tangu mwaka 2002 hadi mwaka jana. Nina vyuma vya kupitisha damu kwenye moyo, hesabu za daktari vipo vinne za kawaida zimefiki tano," alidai.
Alidai kila baada ya miaka miwili, anakwenda kubadilisha chuma na ripoti za zamani hazijawahi kueleza kama anatumia dawa za kulevya.
Pia, alidai kwa siku anatumia vidonge 30 hadi 35 na dawa hizo alipata fursa ya kutumia alipokuwa polisi na hata mahabusu katika Gereza la Keko.
Kuhusu mashitaka yanayomkabili, Manji alidai Februari 8, mwaka huu, alipata taarifa kwamba ametajwa kuwa miongoni mwa watumiaji wa dawa za kulevya na muuzaji, hivyo walitakiwa kuripoti kwa mkuu wa upelelezi wa makosa ya jinai wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam.
Alidai kwa taratibu za kiofisi, aliitisha mkutano na vyombo vya habari, ambapo alikana na kueleza hatasubiri kwenda kuripoti polisi kama alivyotakiwa, bali  atakwenda siku moja kabla.
Manji alidai Februari 8, mwaka huu, alizungumza na vyombo vya habari na Februari 9, mwaka huu, alienda polisi tangu saa 4.30 asubuhi na katikati ya tarehe hizo alikuwa ofisini.
Alidai morphine inakaa kwenye mkojo ndani ya saa 48.  Manji alidai aliamua kwenda polisi kabla ya tarehe aliyopangiwa kwa sababu hakuwa na taarifa kamili kwani aliipata kupitia vyombo vya habari na hakutaka kuchafua jina wala kiti chake.
Alidai baada ya kwenda polisi, alipelekwa kwa mkemia mkuu wa serikali kupima sampuli ya mkojo  na kisha polisi walienda kupekua nyumbani kwale, ambako walichukua kompyuta yake.
Manji aidai shutuma hizo zimemuathiri binafsi kwa kuwa wakati yuko mdogo, baba yake alikuwa akimweleza juu ya jina zuri na maadili kwani zimechafua jina lake.
Pia, alidai anaona aibu kwa watu wanaomfahamu  na alianza matibabu mwaka 2009 na amejitahidi kuacha kuvuta sigara bila mafanikio.
Akihojiwa maswali na Wakili wa Serikali Mkuu, Timon Vitalis, mshitakiwa huyo alidai  daktari wake hajamkataza kutumia dawa za kulevya kwa ajili ya matibabu.
Alidai amejua morphine ni dawa za kulevya baada ya kuletwa mahakamani na kwamba, dawa anazotumia anapewa na daktari wake, ambapo zina uthibitisho na namna ya kutumia.
Shahidi mwingine wa Manji, alikuwa Dk. Khan, ambaye aliieleza mahakama kumfahamu Manji tangu akiwa na umri wa miaka mitatu, mwaka 1978 na alikuwa akimtibu pamoja na familia yake. Shauri hilo linaendelea leo.

No comments:

Post a Comment