Wednesday 27 September 2017

KAMATI KUU CCM KUKUTANA LEO




KAMATI ya Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), inakutana leo, jijini Dar es Salaam, kuanza vikao vyake vya siku mbili, huku ajenda kubwa ikiwa ni kuwajadili wanachama wake walioomba uongozi katika ngazi za wilaya.
Kikao hicho kitafuatiwa na kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, ambavyo vyote vitafanyika chini ya Mwenyekiti wa Chama Taifa, Rais Dk. John Magufuli.
Vikao hivyo ni vya kawaida kwa mujibu wa kanuni na utaratibu wa CCM, ambapo ajenda kubwa ya vikao hivyo ni  kujadili, kupitisha na kufanya uteuzi wa mwisho wa wagombea wa nafasi za uongozi wa  CCM ngazi ya wilaya.
Kwa mujibu wa Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi  wa CCM, Humphrey Polepole, kamati kuu inakutana kwa siku mbili, leo na kesho kabla ya kikao cha NEC.
Polepole alisema baada ya vikao hivyo, Septemba 30 na Oktoba mosi, mwaka huu, itakuwa zamu ya vikao vya NEC, ambavyo vitakamilisha kazi ya uteuzi wa wagombea wa nafasi hizo.
Alisema vikao hivyo vitafanyakazi ya kujadili, kupitisha na kufanya uteuzi wa mwisho wa wagombea, kabla ya uchaguzi wa CCM ngazi ya wilaya.
Kwa mujibu wa ratiba ya uchaguzi wa CCM na jumuiya zake, uchaguzi huo kwa wilaya zote umepangwa kufanyika kuanzia Oktoba 2, mwaka huu, baada ya kukamilika kwa uteuzi wa mwisho.
Vikao hivyo vinafuatiliwa kwa karibu na wanachama  CCM, wakereketwa, mashabiki na Watanzania kwa ujumla, kutokana mvuto wa ajenda kubwa ya kuwajadili, kupitisha na kufanya uteuzi wa mwisho wa wagombea wa ngazi za wilaya.
Hatua hiyo inatokana na mkakati wa mabadiliko unaoendelea ndani ya CCM, wenye lengo la kujenga CCM mpya, itakayokuwa na viongozi waadilifu na wasio na kashfa za usaliti wala ubadhilifu wa mali za Chama.
Hivi karibuni, Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Philip Mangula, alisema CCM haitamteua mwanachama wake, atakayethibitika kutoa rushwa na kufanya kampeni kinyume na utaratibu.
Alisema kamati ndogo inaendelea kufuatilia mienendo ya makada wake, hususan katika maeneo yaliyolalamikiwa na iwapo itathibitika, hawataeuliwa kugombea uongozi wa Chama.
Tangu kuanza kwa uchaguzi katika ngazi za mashina, CCM imekuwa ikifuatilia kwa karibu uchaguzi wake, ambapo hivi karibuni, ililazimika kufuta uchaguzi wa kata zaidi ya 40, kutokana na kasoro mbalimbali zilizojitokeza kwenye uchaguzi.
Wiki iliyopita, CCM ilikamilisha uchaguzi wa jumuiya zake katika ngazi za wilaya kwa maana ya UVCCM, UWT na Wazazi, ambapo baadhi ya viongozi waliochaguliwa ndio watakakuwa wapigakura katika uchaguzi wa Chama ngazi ya wilaya, unaotarajiwa kufanyika wiki ijayo.

No comments:

Post a Comment