Tuesday 19 September 2017

MREMA AISHUKIA CHADEMA




MWENYEKITI wa Chama cha TLP, Augustine Mrema, amevunja ukimya na kuwaonya wafuasi wa CHADEMA, wanaofanya dua maalumu ‘Albadir’ kwamba, wasitumie visivyo dini ya Kiislamu, badala yake waviache vyombo vya dola vifanye kazi yake.

Kauli hiyo ya Mrema inatokana na taarifa iliyotolewa wiki iliyopita na Baraza la Vijana la Chadema (BAVICHA),  kutaka kusoma albadir, kufuatia Mbunge wa chama hicho jimbo la Singida Mashariki,Tundu Lissu, kushambuliwa kwa risasi na watu wasiojulikana, nyumbani kwake mjini Dodoma.

Akizungumza na gazeti hili jana, kwa simu, Mrema alisema watu wasitumie visivyo dini ya kiislamu kufanya mambo ambayo hayapaswi kufanywa, kwa sababu vyombo vya dola vinaendelea na kazi yake katika suala hilo ili watuhumiwa waliohusika waweze kukamatwa.

Mrema alisema dini ya Kiislamu inaheshimika duniani, hivyo kitendo wanachofanya cha kusoma dua, ni hatua kubwa mno kwani serikali haijaonyesha kushindwa kuwakamata waliohusika na shambulio hilo.

Kwa mujibu wa Mrema, wale wanaofanya kwa matakwa yao, ni vyema wakamatwe ili waseme ukweli.

Pia, Mrema aliwataka Watanzania ambao wanazo taarifa kuhusu watuhumiwa hao, waiarifu polisi ili wakamatwe na kufikishwa mahakamani.

Hivi karibuni, Kamishna wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa, alipiga marufuku maandamano yaliyotangazwa na BAVICHA kwa ajili ya kufanya dua ya albadir.

Licha ya agizo hilo, BAVICHA walidai kuwa, wataendelea na mpango wao wa kumwombea dua Lissu na kwamba, zuio la Mambosasa haliwahusu kwa sababu hawafanyi maandamano.

Juzi, Mwenyekiti wa BAVICHA, Patrobas Paschal na Katibu Mkuu wake, Julius Mwita, walitimua mbio na kuwaacha wafuasi wao watatu wakikamatwa na polisi, baada ya kutotii amri iliyokataza kufanya dua hiyo.
Tukio hilo lilitokea katika uwanja wa TIP, ulioko Sinza, jijini Dar es Salaam.

Akizungumzia suala hilo, Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhad Mussa Salum, alisema haoni mantiki yoyote ya watu kusoma dua kwa sababu vyombo vya dola vinafanya kazi yake.

“Unakimbilia kusoma albadir ya nini, wakati vyombo husika vinafanya kazi, waliopigwa risasi ni wengi, Sheikh wetu Ponda (Issa), alipigwa risasi hatujasikia watu wanafanya kisomo.

“Watu wengi wamepigwa risasi na wengine wamefanyiwa mambo yasiyofaa, hatujasikia watu wanasoma albadir, Chacha Wangwe ameuawa huko hatujasikia albadir, Saanane (Ben) amepotea mpaka leo hatujasikia watu kusoma albadir,” alisema.

Akieleza maana ya albadir, Sheikh Salum, alisema  ni kisomo au dua ambayo inatumiwa na viongozi wa Kiislamu kwa mtu ambaye anataka kumshitakia  Mwenyezi Mungu, kutokana na dhuluma atakayokuwa amefanyiwa.

“Ukimshitakia Mwenyezi Mungu kwa jambo ambalo ni sawa sawa, siyo kumshitakia kwa lile ambalo unataka kumuonea mtu.

“Au kumdhuru mtu bila sababu, inatumika kwa watu ambao wamedhulumu wenzao, heshima yake au chochote,  basi unamshitakiwa kupitia dua hiyo,”alisema.

Alisema kwamba, albadir maana yake ni kuwataja maswahaba waliopigana vita vya Badir katika mji wa Makha na sehemu hiyo imekuwa ikitumika kumshitakia Mungu.

No comments:

Post a Comment