Tuesday 19 September 2017

POLISI YAZIDI KUWAKALIA KOONI MADEREVA





JESHI la Polisi Tanzania, limeeleza kwamba litaendelea kufuta leseni za madereva watakao bainika kutotii sheria za barabarani bila ya kujali cheo au umaarufu wa mtu.

Pia, limeeleza kwamba kamwe haliwezi kumfumbia macho dereva yeyote ambaye atabainika kufanya makosa ya kuhatarisha maisha ya watu na mali zao.

Kauli hiyo ilitolewa jana na Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani Tanzania, Kamishna Msaidizi Mwandamizi(SACP), Fortunatus Musilimu, wakati akihojiwa na gazeti hili, ofisini kwake Jijini Dar es Salaam.

Musilimu alisema  wanaendelea kufanya mageuzi katika kikosi cha usalama barabarani ili kuzuia vifo kutokana na ajali na kufanya kazi zao kwa weledi mkubwa.

Alisema amekuwa anafuatilia mienendo ya watendaji wa kikosi hicho ili kujiridhisha na utendaji wao na wale wote wenye udhaifu, atawaondoa kulingana na taratibu za polisi.

Kamishna huyo alisema mara alipotangazwa kushika nafasi hiyo Julai 15, mwaka huu, kutoka kwa Kamanda Mohamed Mpinga, amekuwa anafanya ziara za kushtukiza katika mikoa mbalimbali kwa lengo la kujitambulisha na kujionea mwenyewe kazi jinsi zinavyofanyika .

Alisema tayari amefanya hivyo kwenye mkoa wa Mbeya, ambapo alizifungia leseni za madereva saba wa magari  baada ya kubaini wamekiuka sheria za nchi, ikiwa ni pamoja na kusababisha ajali mbaya na vifo.

Pia, alifanya hivyo kwenye mkoa wa Arusha na kufuta leseni za madereva 13, Manyara alifuta leseni za madereva wanne na Kilimanjaro alifuta leseni 47 za madereva kutokana na makosa mbalimbali.

Kamanda Musilimu alisema leseni za madereva hao zitafungiwa katika kipindi cha miezi sita, mpaka watakapojirekebisha utendaji wao na kutii sheria bila shuruti.

Alitaja miongoni mwa sababu za kufuta leseni hizo kuwa ni  baadhi ya madereva kuwakuta wakiwa wamelewa.

Akizungumzia kitendo cha polisi kutoza faini, alisema
jeshi hilo halikusanyi mapato na kusisitiza kazi yao ni kuzuia uhalifu na kulinda mali za wananchi.

Kamishna  Musilimu alisema kauli zinazotolewa na baadhi ya watu kuwa askari wamekuwa wanapangiwa kiasi cha kutoza faini kwa watu wanaobainika kufanya makosa siyo za kweli.

Alisema serikali iliamua kutunga sheria ya watu kulipa faini kupitia mihamala ya mitandao kwa lengo la kupunguza mrundikano wa kesi.

Kamanda huyo alisema lengo la serikali ni kutaka kupunguza mrundikano wa kesi katika mahakama hapa nchini, kitendo ambacho kimepunguza kesi zilizokuwa zimefunguliwa kwa wingi katika mahakama mbalimbali.

Kamishna huyo alisema sheria itabakia kama ilivyowekwa kwa makosa makubwa, ikiwemo kusababisha vifo au kuendesha gari akiwa amelewa na kusababisha ajali.

Alisisitiza kwamba, kama watu wanafikiri serikali inaendeshwa kwa mapato ya faini, wanafanya makosa.

Pia, alisisitiza kuwa hakuna askari yeyote wa kitengo cha usalama barabarani aliyepangiwa kukusanya fedha kutokana na makosa ya madereva.

Alisisitiza kuwa yeye na watendaji wenzake watafanya kazi muda wote, iwe usiku wa manane au mchana, ndio maana amekuwa akiibuka ghafla kufanya ukaguzi katika vituo mbalimbali na kuchukua hatua kwa askari wote wanaofanya kazi zao kinyume na taratibu za jeshi hilo.

No comments:

Post a Comment