Thursday 21 September 2017

SERIKALI KUGHARAMIA MATIBABU YA LISSU




SERIKALI imesema iko tayari kugharamia matibabu ya Mbunge wa Singida Mashariki (CHADEMA), Tundu Lissu, popote duniani pindi itakapopata maombi kutoka kwa familia yake.
Taarifa ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, iliyosambazwa kwa vyombo vya habari jana, ilieleza kwamba, mbali ya maombi hayo, serikali pia inasubiri taarifa rasmi kutoka kwa madaktari wanaomtibu kuhusu mahitaji halisi.
“Akiwa kama Mtanzania na Mbunge, serikali iko tayari kugharamia matibabu zaidi ya Lissu, popote duniani mpaka apone ili aweze kuendelea na kazi ya kuwahudumia Watanzania na wana Singida,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.
Waziri wa wizara hiyo, Ummy Mwalimu, alisema kwamba, serikali iko tayati kufanya hivyo, endapo maombi yatawasilishwa rasmi, ikiwa ni pamoja na kupata maendeleo ya afya yake kutoka kwa madaktari wanaomhudumia hivi sasa jijini Nairobi, Kenya.
Ummy alisema, anashangazwa na dhana ya kuchangishana kwa ajili ya matibabu ya Lissu, akatahadharisha kwamba, matapeli wanaweza kutumia mwanya huo kujipatia fedha.
Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu, Profesa Ibrahim Juma, amesema tukio la kushambuliwa Lissu na watu wasiojulikana, ni funzo kwa namna gani nchi zimejipanga kupambana na uhalifu na kitu cha kwanza ni kukusanya ushahidi.
Amesema nchi nyingine zimefunga kamera katika barabara kuu, ambapo Nairobi kumefungwa kamera za CCTV kila sehemu katika barabara na nyumba, ambao huo ni ushahidi wa kutosha.
Jaji Mkuu Profesa Juma aliyasema hayo jana, jijini Dar es Salaam, alipokuwa akijibu swali lililoulizwa na waandishi wa habari juu ya tamko la Chama cha Mawakili cha Uingereza, kuhusiana na tukio la kushambuliwa kwa mbunge huyo.
Akizungumzia tamko hilo, Jaji Mkuu alisema kwa kanuni zao, hawaruhusiwi kutoa maoni wala kuzungumza jambo moja kwa moja, ambalo litafika mahakamani, ndiyo maana wamekaa kimya.
Kuhusu uhuru wa mahakama nchini, ikilinganishwa na Kenya, Jaji Mkuu alisema, Tanzania ipo huru na kuwataka Watanzania kuendelea kujidai na sheria na kuzitumia.

No comments:

Post a Comment