WABUNGE
watatu wa CHADEMA, jana waliingia mitini na kushindwa kuwasilisha ushahidi
zaidi wa tuhuma za rushwa kwa madiwani 10, waliojiuzulu chama hicho.
Juzi,
wabunge hao waliwasilisha baadhi ya vielelezo kwa Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya
Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Valentino Mlowola, wakidai kuwa ni
ushahidi dhidi ya madiwani hao.
Hata
hivyo, Mkurugenzi huyo wa TAKUKURU, aliwaagiza wabunge hao kuwasilisha
vielelezo zaidi kuhusu tuhuma hizo dhidi ya wabunge hao jana, lakini
walishindwa kufanya hivyo.
Hayo
yalibainika baada ya wabunge hao, Joshua Nassari (Arumeru Mashariki), Godbless
Lema (Arusha Mjini) na Mchungaji Peter Msigwa wa Iringa Mjini, kushindwa
kuonekana kwenye ofisi za makao makuu ya TAKUKURU, Dar es Salaam, kama
walivyowaahidi waandishi wa habari.
Juzi,
walipofika kwenye ofisi hizo ili kuwasilisha ‘flash’ waliyodai kuwa na video za
ushahidi wa viongozi wa serikali kupanga njama za kuwanunua madiwani hao,
waliahidi wangefika tena jana, ili pamoja na mambo mengine kufungua jalada la
upelelezi huo.
Uhuru
jana, liliweka kambi maeneo ya Upanga, mpaka muda wa kufunga ofisi za serikali,
bila kuona dalili za ujio wa wabunge hao waliojitamba kwa wanahabari mkoani
Arusha kwamba, wanao ushahidi wa kutosha juu ya madai yao.
'Kukacha'
kwao kulithibitishwa na Msemaji wa TAKUKURU, Mussa Misalaba, ambaye alisema
bado wanaendelea kuwasubiri viongozi hao kwa ajili ya kuwasilisha ushahidi
zaidi, kwa kuwa video pekee haitoshi kukamilisha uchunguzi na kutoa haki kwa
anayestahili.
"Niko
nje ya ofisi, lakini bado uchunguzi wa tuhuma hizo unaendelea. Waheshimiwa
wabunge bado tunawasubiri watuletee ushahidi zaidi kwa kuwa hii video haitoshi
na bila ushahidi zaidi haina maana," alisema Misalaba.
Aliongeza
kuwa, sababu ya TAKUKURU kudai ushahidi zaidi ni kutokana na uwepo wa mambo
mengi kwenye madai yao na taratibu za uchunguzi wa taasisi hiyo zinazohitaji
ushahidi wa kutosha.
Mbali
na hilo, Misalaba alisisitizia kauli ya Mkurugenzi wake mkuu, Mlowola, ambayo
aliitoa juzi, kwa wabunge hao kuwa uchunguzi utafanywa kwa weledi mkubwa bila
kujali upande wa viongozi hao kisiasa.
Uhuru
kwa uchunguzi wake wa kuaminika, lilipata utetezi wa Nassari kuhusu kutokuonekana
kwao kwenye ofisi za TAKUKURU jana, kwamba walikuwa wanasubiri 'vitu fulani'
kabla ya kurudi tena ofisini hapo leo.
Wiki
iliyopita, Nassari na Lema walikutana na
wanahabari na kuonyesha video waliyodai kuwa ni ushahidi wao juu ya tuhuma
kwamba, madiwani waliokuwa CHADEMA na baadaye kujiuzulu, walinunuliwa.
Tuhuma
hizo walizielekeza kwa Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Alexander Mnyeti, Katibu
Tawala wake, Timothy Mnzava na madiwani husika waliojiuzulu na baadaye kujiunga
na Chama cha Mapinduzi (CCM).
Madiwani
hao na kata zao kwenye mabano ni Edward Sepunyo (Moita), Manda Ngoitiko (Viti
Maalumu), Rayson Ngowi (Kimandolu), Credo Kifukwe (Muriet), Solomon Laizer
(Ngabobo), Anderson Sikawa (Leguruki), Emmanuel Mollel (Makiba), Bryson Isangya
(Maroroni) na Josephine Mshiu wa viti maalumu.
Baada
ya kujiuzulu, madiwani hao walitangaza kujiunga na CCM, ambapo Rais Dk. John
Magufuli, ambaye ni Mwenyekiti wa CCM Taifa, aliwapokea na kuwakabidhi rasmi
kadi za uanachama, akiwa kwenye ziara yake mkoani Arusha.
No comments:
Post a Comment