Friday 13 October 2017

SETHI APELEKWA MUHIMBILI, AFANYIWA VIPIMO




UPANDE wa jamhuri katika kesi inayowakabili vigogo wa Kampuni ya IPTL, umeieleza mahakama kwamba, imetekeleza amri zake, ambapo mshitakiwa Harbinder Sethi, amepelekwa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) na kufanyiwa vipimo.
Umeieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kuwa mshitakiwa Sethi alipelekwa Muhimbili, juzi, ambapo kafanyiwa vipimo na wanasubiri ripoti itakayotolewa wiki ijayo.
Wakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Leonard Swai, alieleza hayo jana, mahakamani hapo, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi, wakati shauri hilo, linalomkabili Sethi na James Rugemarila, lilipopelekwa kwa kutajwa.
Swai alidai upelelezi wa shauri hilo unaendelea na kwamba, wametekeleza amri ya mahakama, ambapo Sethi alipelekwa Muhimbili juzi, ambako alifanyiwa vipimo na ripoti itatoka wiki ijayo.
Kwa upande wa Wakili wa Rugemarila, Respicius Didas alidai  kuna suala la ucheleweshaji wa upelelezi kwani washitakiwa walifikishwa mahakamani hapo Juni 19, mwaka huu, kwa mashitaka ambayo yanadaiwa kutendeka mwaka 2013.
Alidai washitakiwa wapo mahabusu na upande wa jamhuri kila kesi ikitajwa, wanaeleza upelelezi haujakamilika wakati wateja wao kwa kuendelea kukaa ndani kuna athari.
Akijibu hoja hizo, Wakili Swai alidai kuchelewa kwa upelelezi kunatokana na makosa ya kughushi, ambayo upelelezi wake huchukua muda mrefu, ambapo aliahidi kukamilisha.
Sethi na Rugemarila wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi, ikiwa na mashitaka  12, yakiwemo ya kula njama, kujihusisha na mtandao wa uhalifu , kughushi,  kutoa nyaraka za kughushi, kujipatia fedha kwa njia za udanganyifu na kutakatisha fedha  na kuisababisha hasara ya Dola za Marekani 22, 198,544.60 na sh. 309,461,300,158.27.


No comments:

Post a Comment