Wednesday 16 September 2015

MAGUFULI NI SHIDAAAAA


 Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,kupitia CCM Dk. John  Magufuli akiwahutubia wakazi wa mji wa Kaliua katika Uwanja wa Kolimba
 Wakazi wa mji wa Kaliua wakimsikiliza Mgombea urais wa CCM, Dk. Magufuli alipokuwa akiwahutubia
 Mgombea Urais wa CCM Dkt Magufuli akimkabidhi Ilani ya CCM mgombea ubunge wa jimbo la Kaliua, Profesa Juma Kapuya
  Mgombea urais wa CCM, Dk Magufuli akisalimiana na mgombea ubunge wa jimbo la Urambo,.Margareth Sitta. Kulia kwake ni mbunge wa zamani wa jimbo hilo,.Samwel Sitta.


NA SELINA WILSON, URAMBO
MGOMBEA urais wa CCM, Dk. John Magufuli, amezidi kuchanja mbuga huku akiahidi utendaji kazi uliotukuka kwa maendeleo ya haraka ya Watanzania.
Akionekana tofauti na wagombea wengine, akiwemo Waziri Mkuu aliyejiuzulu kwa kashfa ya Richmond na anayelalamikiwa kwa kushindwa kukata kiu ya wananchi kwa kuhutubia dakika sita hadi tatu, Edward Lowassa, Dk. Magufuli amekuwa kivutio kikubwa kwenye mikutano yake.
Jana, alitua Urambo huku akiendelea na utaratibu wake wa kutumia barabara, ambaapo alihutubia mkutano wa hadhara na kuahidi kujenga kilometa sita za barabara ya lami katika mji wa Urambo.
Alisema pia ataharakisha ujenzi wa barabara ya lami ya Kaliua/ Urambo unakamilika haraka ili kufungua fursa za kiuchumi kwa kurahisisha usafiri na usafirishaji wa mazao.
Dk. Magufuli alisema serikali yake ya awamu ya tano itaendelea kuunganisha wilaya na mikoa kwa lami ili wananchi wawe na uwezo wa kusafirisha bidhaa zao kwenda maeneo mbalimbali hadi nje ya nchi.
Alisema anatambua tatizo kubwa la Urambo, hivyo atahakikisha wanajenga mabwawa makubwa na kuhifadhi maji na kuyasukuma kwenda kwa wananchi.
“Tunajenga madaraja kuzuia maji, tutatumia magreda kuchimba mabwawa na kuelekeza maji kutoka kwenye madaraja hayo na kutengeneza miundombinu ya kuyatunza na kuyafikisha kwa wananchi,”alisema.
Katika hatua nyingine, Dk. Magufuli alisema kwamba ataziba mianya ya fedha zinazovuja na kuchotwa na wajanja wachache wanaokwamisha maendeleo ya wananchi.
“Nitatumia jina langu la Magufuli kuwadhibiti watu hao na kuzitumia fedha hizo kuboresha elimu na kuanzia mwakani wanafunzi kuanzia darasa la kwanza hadi kidato cha nne hawatalipa karo,” alisema.
Alisema pamoja na kufuta karo, serikali yake pia itaangalia suala la michango ili kuliondoa  wanafunzi wasome bila kusumbuliwa kwa kuwa anataka kujenga Taifa la wasomi.
Dk. Magufuli alisema akichaguliwa, atakuwa Rais wa vyama vyote, makabila yote, dini zote kwa kuwa anajua mahitaji ya Watanzani sio vyama bali ni mtu wa kuwafanyia kazi.
Kuhusu kodi alisema ataweka utaratibu mzuri wa ukusanyaji wa kodi ambao kwa sasa unawalenga wanyonge wakiwemo wafanyabiashara ndondogo na wafanyakazi ambao wamekuwa wakibeba mzigo mkubwa.
Alisema akiingia Ikulu, atapunguza makato ya kodi kwa wafanyakazi kutoka asilimia 11 ili ibakie tarakimu moja na kwa wafanyabiashara ndogondogo hatokubali wabanwe na kodi za hovyo hovyo, badala yake wafanyabiashara wakubwa ndio walipe kodi.
Dk. Magufuli aliwaponda wanasiasa wanaofanya kampeni kwa kuwaahidi Watanzania mambo ya uongo, jambo ambalo alisema ni dharau kubwa ambayo dawa yake ni kuwanyima kura.
Aliwaomba wananchi wa Urambo wamchague Magreth Sitta kwa kuwa ni mtu anayemfahamu vyema.
“Ni mchapakazi, ni mwana mama mahiri, ni mwalimu na mimi mwalimu pia ni jasiri,
Nimesoma  naye Chuo Kikuu, ninamfahamu Magreth. Ninaomba kwa heshima kubwa mniletee huyu. Namkabidhi Ilani ya Uchaguzi ili yote yanayotakiwa kutekelezwa ndani ya Ilani ayasimamie huyu,”alisema.
Akizungumza katika mkutano huo, Magreth aliwaomba wana Urambo wamchague Dk. Magufuli kwa kuwa anayatambua matatizo ya zao la tumbaku, hivyo akiwa rais atayamaliza.
Bulembo
Mwenyekiti wa Jumuia ya Wazazi Taifa, Abdalla Bulembo, aliwataka wananchi wa Urambo wamchague Dk. Magufuli kwa kuwa ni mtoto wa masikini, aliyepitia maisha ya kawaida na anazijua shida za Watanzania.
Hatuwezi kupeleka Ikulu wapiga dili. Msichague CCM B, chagueni viongozi mliowazoea. Msihangaike na mtu ambaye hata hawezi kushika kalamu kuandika,”alisema.
Mpanju
Kwa upande wake, Mjumbe wa Kamati ya Kampeni, Amon Mpanju, aliwataka wananchi wa jimbo hilo wamchague Magreth kwa kuwa ni kiongozi anayejali makundi ya watu mbalimbali wenye ulemavu.
Alisema wasikubali kupotoshwa na wapinzani ambao mgombea wao, Edward Lowassa, amekuwa akihubiri udini kwa kuwataka Walutheri wamchague yeye kwa kuwa ni mwenzao.
Kabla ya kwenda Urambo, Dk. Magufuli alifanya mkutano katika jimbo la Kaliua na kumnadi mgombea ubunge wa jimbo hilo, Profesa Juma Kapuya, akisisitiza kwamba ni mchapa kazi hodari.
Aliwaahidi wananchi wa jimbo hilo kwamba anajua changamoto za jimbo hilo kuwa ni maji na miundombinu ya barabara na kwamba hilo ni eneo lake, hawezi kushindwa hivyo wampe kura awatumikie.
Katika mikutano yake katika kila jimbo, Dk. Magufuli amekuwa akipokea wanachama kutoka vyama vya upinzani, ambao wamekuwa wakirudisha kadi za vyama vya CUF na CHADEMA, baada ya kuchoshwa na siasa za hovyo.
Miongoni mwa wanachama hao ni viongozi waandamizi wa CHADEMA, wakiwemo wenyeviti na makatibu wa wilaya, ambao walisema kwamba wameamua kurudi CCM kutokana na kukerwa na mtindo wa kukataa wagombea na kusimamisha ‘makapi’ kutoka CCM.
Akizungumza katika moja ya mikutano hiyo, aliyekuwa Katibu wa CHADEMA Wilaya ya Urambo, Obeid Obeid alisema ameamua kutoka ili awe huru kwa kuwa CHADEMA kuna mambo mabaya yanakera ikiwemo kuuza chama.
Obeid alisema Dk. Magufuli anatosha kuwa Rais wa Tanzania na wagombea wa vyama vingine ni makapi, hawana sifa ya kuongoza nchi.
Alisema Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe anachukua ruzuku sh. milioni 334, lakini anashindwa kuwezesha ofisi na hivi karibuni ofisi yao walitolewa vyombo nje kutokana na kukosa kodi.

No comments:

Post a Comment