Tuesday 1 March 2016

LUHWAVI: MABADILIKO MAKUBWA CCM YAJA



CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kinajiandaa kufanya mabadiliko makubwa ndani ya miaka mitano ijayo ili kuwa cha kisasa na kujiendesha kwa ufanisi zaidi katika kuwahudumia Watanzania.
Kimesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha Watanzania wanaendelea kufurahia matunda ya uhuru na kuwa na maendeleo ya haraka, ambapo suala la uboreshwaji wa maslahi ya watumishi, uwezo wa kiutendaji na mazingira bora katika sekta zote ni mambo yatakayopewa kipaumbele zaidi.
Hata hivyo, kimeonya kuwa serikali yake haitasita kuwawajibisha watumishi na watewndaji wote, ambao watakwenda kinyume cha taratibu na kukwamisha utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi kwani, kufanya hivyo ni kurudisha nyuma jitihada za nchi kujikwamua.
Hayo yameelezwa jana na Naibu Katibu Mkuu wa CCM (Bara), Rajab Luhwavi, alipokuwa akizungumza na watumishi na watendaji, ambapo alisema kupitia mpango huo, CCM inalenga kuwa Chama kinachokwenda na wakati kwa kuwa na watumishi wenye uwezo kulingana na wakati.
Alisema Chama kimewaagiza watumishi wake wote kujiendeleza kielimu na kwamba, kipo tayari kugharamia mafunzo yao kitaaluma katika vyuo vya ndani na nje ili kuongeza tija na ufanisi katika utendaji.
Kwa mujibu wa Luhwavi, amewataka watumishi wa CCM wenye elimu ya darasa la saba, kuhakikisha kati ya sasa na Juni, mwaka huu, wanajitokeza kujiorodhesha na kujisajili kwenye mpango maalumu wa elimu ili waweze kujiunga na masomo ya kidato cha kwanza.
“Tunatoa miaka mitatu kwa walio na elimu ya darasa la saba wahakikishe wanamaliza kidato cha nne na baada ya hapo watakaoshindwa kwenda na agizo hili tutaachana nao kwa amani. Katika hili hatutanii kwani Chama sasa kinataka kujijenga zaidi na kuwa bora katika kila idara,” alisema.
Alisema chini ya mpango huo, mtumishi wa chama katika kila ngazi ya elimu atatakiwa kujiendeleza na kwamba, CCM itashirikiana nao kuhakikisha azma hiyo inatimia.
Luhwavi alisema mpango huo wa maboresho pia utahusu kuwajengea uwezo watumishi wa chama kupitia mafunzo mbalimbali yatakayoanza kutolewa na CCM kupitia chuo chake cha Ihemi kilichoko mkoani Iringa.
“Tutaanza na makatibu muhtasi kuwapeleka Ihemi ili wakapate mafunzo maalumu na kurudi kwenye utaratibu wetu wa awali, ambao ulituwezesha kuwa na watumishi makada, wenye uwezo na ari ya kukitumikia Chama,” alisema.
Awali, akizungumza katika mkutano huo uliofanyika kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Katibu Msaidizi Mkuu wa CCM, anayeshughulikia vyama vya wakimbizi kusini mwa Afrika, Amos Siyantemi, aliwaomba wana-CCM kutembea kifua mbele kutokana na kazi nzuri ya Rais wa awamu ya tano, Dk. John Magufuli.
Siyantemi alisema kila mwana-CCM anapaswa kujivunia mafanikio hayo na kuwapinga wanaojaribu kumtenganisha Dk. Magufuli na CCM.
Mkutano huo uliwahusisha watumishi wa CCM na jumuia zake kutoka mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Simiyu, Geita na Mara.

No comments:

Post a Comment