Monday 27 June 2016

SHAKA: WALIOTAKA TUIIGE EU SASA WAMEUMBUKA





UMOJA wa Vijana wa CCM (UVCCM) umesema baadhi  ya wanasiasa  waliotaka Tanzania iwe na muundo unaofanana na Umoja wa Ulaya (EU), walikusudia kuudhoofisha Muungano wa Tanganyika na Zanzibar na kutaka uvunjike ili taifa lisambaratike.
Pia, alisema wanasiasa hao walilenga kuligawa taifa na kuwagawa wananchi kwa kuondoa mshikamano uliopo.
Kaimu Katibu Mkuu wa UVCCM, Shaka Hamdu Shaka, alisema hayo ofisini kwake jana, alipokuwa akitoa maoni yake baada ya Uingereza kupiga kura ya kujitoa EU.
Shaka alisema muundo wa EU ni wa jumuia ya kimaendelo na kwamba, hauna sura ya  kuwaweka watu katika mazingira na malengo ya kubeba maisha ya watu, maendeleo, kuimarika kwa uchumi au kupigania ustawi wa amani ya pamoja.
Alisema kwa sababu ya mfumo huo kuwa dhaifu na legelege au usio na masharti ya kudumisha umoja na
maisha ya watu wake kijamii, kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni,  jambo linalofanya mwanachama yeyote kutoka wakati wowote na wakati mwingine bila hata ya sababu ya maana na ya msingi.
"Tuliwaambia mamluki na wasaka madaraka kwa hila kwamba, muundo wa EU una mashaka, si imara kama  wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Marekani (USA), Afrika Kusini au Uingereza (UK), lakini walibisha, sasa ni wazi wanaaibika wanaposikia haya yanayoendelea kwa baadhi ya wanachama kujiondoa,"alisema Shaka.
Alisisitiza kuwa katika dhamira njema inayoheshimu, kulinda,  kuhifadhi na kuendeleza maisha ya watu kwa nyakati zote, ni rahisi kuuita muundo wa EU  kuwa ni legelege na usio na dhamira ya dhati kuwaunganisha watu wake.
Hata hivyo, Kaimu Katibu Mkuu Shaka, alisema UVCCM kila zilipotolewa hoja na wanasiasa wa upinzani, hususan chama cha CUF, kutaka muundo wa Muungamo wa Tanzania uwe kama EU, ilisimama kidete kupinga.
Alisema CCM hawakukaa kimya bali walikuwa wakiuchambua muungano huo na kuonyesha athari zake na kuongeza kuwa, umejikita kushirikiana katika nyanja za  kiuchumi huku ukiwa hauna kinga na msingi madhubuti wa kudumisha utaifa na umoja.

"Tutaendelea kuwaenzi, kuwasifu na kuwathamini waasisi wetu, ambao wamefanikiwa kuliweka taifa letu pamoja kwa zaidi ya miaka 50 sasa. Tuna muungamo imara unaojali na kulinda maisha na umoja wa kimaendeleo kwenye demokrasia, kisiasa na kiuchumi,"alisema.

Shaka alisema watu wa taifa moja wakiishi kwa umoja, kushirikiana na kuhurumiana, lazima itambulike kuwa, jambo hilo lilijengwa katika misingi imara na madhubuti isiyopaswa kuvunjwa.
"Kwa mfano Northern Island, Wales au Scotland zinaweza kujitoa EU wakati wowote, lakini nina hakika watu wake hawafikirii wala siamini kwamba watataka siku moja wajiweke kando na muungamo wa UK. Yawezekana wapo wachache wanaoweza kufikiria kinyume, lakini hawawezi kufanikiwa,"alisema.
Aidha, Shaka alisema nchi mbalimbali duniani zinautamani Muungano wa Tanzania kwa vile ni wa kipekee kwa kuwa unaweza kufananishwa na nchi chache duniani kama vile Ujerumani, Afrika Kusini, Uingereza, Pakistan na Marekani ambao  wameweza kuwa na muungano wa kweli kwa ajili ya watu wote.
Maoni ya Shaka yamekuja siku chache baada ya Waziri Mkuu wa Uingereza, David Cameron, kutangaza kujiuzulu baada ya serikali yake kushindwa katika kura ya maoni ya kuendelea au kujitoa kwenye EU.
Cameron alifikia uamuzi huo baada ya kura za maoni kuonyesha kuwa, wananchi waliotaka Uingereza ijitoe kwenye umoja huo ni asilimia 52 dhidi ya 48 waliopinga.
Alisema hawezi kuendelea kuongoza nchi hiyo huku ikiwa nje ya umoja huo, ambapo kwa hisia kali, Cameron alisema anakubali matokeo ya kujitoa kwenye umoja huo huku akisema kilichofanyika ni jambo la kidemokrasia.

No comments:

Post a Comment