Friday 1 July 2016
AMSON GROUP KUJENGA MAJENGO MATATU YA HOSPITALI DAR
KAMPUNI ya Amsom Group imejitolea kujenga majengo matatu katika Hospitali za Amana, Temeke na Mwananyamala, jijini Dar es Salaam, yatakayotumika kwa ajili ya kinamama wanaojifungua.
Ujenzi wa majengo hayo, kila moja likiwa na ghorofa mbili, utakaogharimu zaidi ya sh. bilioni 3.6, unatarajiwa kuanza Agosti, mwaka huu na kukamilika mapema mwakani.
Akizungumza wakati wa hafla fupi ya kukakibidhiwa ramani ya majengo hayo, iliyofanyika katika Hospitali ya Amana, jana, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, alisema serikali mkoani humo inakusudia kumaliza kabisa tatizo la mazingira duni kwa kinamama wanaojifungua.
Alisema ujenzi wa majengo hayo, yatakayokuwa na wodi za kisasa, utaondoa kabisa tatizo la kinamama kulala zaidi ya mmoja katika kitanda kimoja.
“Moja ya changamoto kubwa, ambazo mkoa wangu unakumbana nazo ni idadi ya kinamama wengi kulala chini na hata tunapotafuta magodoro, hatuna mahala pa kuyaweka,”alisema Makonda.
Aliongeza kuwa kufuatia bajeti ndogo ya serikali kuu, serikali ya mkoa iliamua kutafuta njia mbadala ili kukabiliana na changamoto hiyo, ambapo kampuni ya Amsom Group ilijitokeza kusaidia ujenzi huo.
“Lengo letu ni mama mmoja kitanda kimoja. Tunakwenda kuondoa tatizo la kinamama kulala chini, na si tu kulala chini, bali hata kulala kinamama zaidi ya mmoja katika kitanda au godoro moja,”alisema mkuu huyo wa mkoa.
Meneja Ukuzaji wa Biashara wa Amsom Group, Suleiman Amour, alisema kila jengo moja litakuwa na uwezo wa kuchukua wagonjwa 150 kwa wakati mmoja.
Alisema tayari maandalizi yameshafanyanyika, ikiwa ni pamoja na ramani ya majengo.
“Lengo kuu ni kuisaidia jamii ili nayo iweze kunufaika na biashara tunayoifanya kwa kuwarudhishia kile ambacho tunakipata. Nia yetu ni kuisaidia jamii ili nayo ijisikie ni watu wenye kuthaminiwa na kuishi maisha ya kusaidiana,” alisema Amour.
Wakati huo huo, Makonda jana alikabidhi magodoro 100, katika Hospitali ya Amana, yaliyotolewa na Kampuni ya GSM Foundation kwa ajili ya wagonjwa.
Akikabidhi magodoro hayo, Meneja Mkuu wa GSM Foundation, Shanon Kiwamba, alisema lengo ni kuondoa changamoto za mahali pa kulala kwa wagonjwa.
Alisema wamepanga kusambaza magodoro hayo katika hospitali za Amana, Mwananyamala na Temeke.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment