Sunday 10 July 2016

TCRA YAAKUNJUA MAKUCHA, YAZITOZA FAINI KAMPUNI SITA ZA SIMU


MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), imezipiga faini kampuni  sita za simu na kuzitaka zilipe sh. milioni 649, kabla ya Julai  30, mwaka huu.

Hatua hiyo inatokana na kampuni hizo kukiuka masharti  ya usajili  wa laini za simu za mkononi.

Mbali na hatua hiyo, TCRA pia imezitaka kampuni hizo  kuwasilisha  orodha  iliyohakikiwa ya mawakala wa kusambaza na kuuza  laini za simu nchini ifikapo Julai  15, mwaka huu.

Tamko hilo lilitolewa Dar es Salaam, jana na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, James Kilaba, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.

Alisema hatua hiyo inafuatia kampuni  hizo kukiuka masharti ya usajili wa namba au laini za simu za mkononi.

Kilaba alizitaja kampuni hizo kuwa ni  Airtel Tanzania Limited, Benson Informatics  Limited (Smart), MIC  Tanzania Limited (TIGO),  Viettel Tanzania  Limited (Halotel), Vodacom Tanzania  Limited na Zanzibar Telecon Limited (Zantel).

"Kampuni hizo zimekiuka  masharti  ya usajili  wa laini na matumizi ya laini kama yalivyoainishwa na sheria ya mawasiliano ya kielektroniki na posta ya mwaka 2010 na  kanuni ya  mawasiliano ya kielektroniki  na  posta ya mwaka  2011," alisema.

Aliyataja maeneo yaliyogungulika kuwepo na ukiukwaji wa  usajili  wa laini  za simu kuwa ni  namba kutolewa bila  mteja  kutakiwa kusajiliwa, namba kusajiliwa kwa majina, vitambulisho na nyaraka za watu wengine,  namba kutofungwa hadi usajili kukamilika na  namba kusajiliwa usajili wa awali.

Kilaba alisema Airtel Tanzania inatakilwa kuilipa TCRA sh. millioni
182,500 kabla  ya Julai 30, mwaka huu, ambapo  sh. milioni  74 ni faini kwa kuruhusu kuuzwa kwa laini  148 bila kutumia kitambulisho halisi cha mnunuzi,  sh. milioni 33,500 kwa kuruhusu laini 67, ziuzwe bila kujaza fomu za usajili,  sh. milioni  32,500 kwa kuruhusu laini  65 ziwashwe  kabla  ya  kuuzwa na sh. milioni  42, 500  kwa kuruhusu laini  85 zifanyiwe usajili wa awali  na kutumika kwenye mtandao wake.

Alisema SMART inatakiwa kulipa sh. milioni  17, ambapo  sh. milioni   saba  kwa kuruhusu  kuuzwa  kwa laini  14 bila kutumia  kitambulisho  halisi  cha  mnunuzi,  sh. milioni  saba kwa  kuruhusu laini  14 ziuzwe  bila kujaza fomu  ya usajili  na sh. milioni tatu  kwa  kuruhusu laini  sita ziwashwe  kabla  ya kuuzwa.

TIGO   inatakiwa kulipa sh. milioni  189, ambapo sh. milioni 93,500, kwa  kuruhusu  kuuzwa  kwa laini  187 bila kutumia kitambulisho, sh. milioni  43,500,  kwa  kuruhusu  laini  87 ziuzwe  bila kujaza fomu  ya usajili,  sh. milioni  41 kwa  kuruhusu laini  82 ziwashwe  kabla ya kuuzwa  na sh. milioni  11 kwa kuruhusu  laini 22  zifanyiwe  usajili  wa awali  na  kutumika kwenye  mtandao wake.

Kampuni ya Halotel  inatakiwa kulipa sh. milioni 107, ambapo sh. milioni 36 kwa kuruhusu  kuuzwa kwa laini 73, bila kutumia kitambulisho, sh. milioni 36,  kwa  kuruhusu  laini  72 ziuzwe  bila kujaza fomu  ya usajili,  sh. milioni 34, kwa  kuruhusu  laini  82 ziwashwe  kabla ya kuuzwa.

Vodacom inatakiwa kulipa sh. milioni  96, ambapo sh. milioni  49, kwa  kuruhusu  kuuzwa  kwa laini  98 bila kutumia kitambulisho, sh. milioni  24,  kwa  kuruhusu  laini  48 ziuzwe  bila kujaza fomu  ya usajili,  sh. millioni 19,  kwa  kuruhusu  laini  38 ziwashwe  kabla ya kuuzwa  na sh. milioni  4.5  kwa kuruhusu  laini tisa zifanyiwe  usajili  wa awali  na  kutumika wenye mtandao wake.

Aidha, Zantel inatakiwa kulipa  sh. milioni  57, ambapo sh. milioni  36.5, kwa  kuruhusu  kuuzwa  kwa laini  73 bila kutumia kitambulisho, sh. milioni  11.5 kwa  kuruhusu  laini  23 ziuzwe  bila kujaza fomu ya usajili,  sh. milioni  saba  kwa  kuruhusu laini  14 ziwashwe  kabla ya kuuzwa na sh. milioni mbili  kwa kuruhusu  laini  nne zifanyiwe  usajili  wa awali  na  kutumika kwenye  mtandao wake.

Kilaba aliwataka watoa huduma hao kuacha kuwatumia mawakala  wasioruhusiwa  kuuza  au kusambaza  laini  za simu nchini na kuzima
laini  zote  zilizopo sokoni,  ambazo zimewashwa na kuhakikisha wanawasilisha taarifa ya  utekelezaji  wa TCRA ndani ya siku saba, kuanzia tarehe walizopokea uamuzi huo.

Alionya kuwa mtoa huduma atakayekaidi utekelezaji huo,   hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yake, ikiwa ni pamoja na  kushitakiwa kwa makosa ya jinai.

No comments:

Post a Comment