MKURUGENZI wa Mashitaka
nchini (DPP), Biswalo Mganga amewafutia mashitaka washitakiwa 10, akiwemo
aliyekuwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala, Gabriel Fuime, waliokuwa
wakikabiliwa na kesi ya mauaji ya bila kukusudia, yaliyotokea baada ya
kuporomoka kwa jengo la ghorofa 16 kwenye mtaa wa
Indira Gandhi, Dar es Salaam.
Wakati Fuime na wenzake hao 10,
wakifutiwa mashitaka na kuachiwa huru jana, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi
Kisutu, washitakiwa wawili, mmiliki wa jengo hilo, Raza Ladha na Mhandisi
Mohamed Abdulkarim, wanaendelea
kushitakiwa.
Wakili wa Serikali Mkuu, Bernard
Kongola akishirikiana na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Mutalemwa Kishenyi,
waliwasilisha hati ya DPP ya kuwaondolea mashitaka washitakiwa hao mbele ya
Hakimu Mkazi Mkuu, Dk. Yohana Yongolo.
“Kutokana na mazingira ya shauri
hili, upande wa jamhuri umeamua kuwafutia mashitaka baadhi ya washitakiwa,”
alidai Wakili Kongola.
Hakimu Dk. Yongolo alimtaka Wakili
huyo kueleza sababu za uamuzi huo, ambapo Wakili Kongola alidai hatua hiyo
inatokana na upelelezi uliofanyika na ushahidi uliokusanywa.
Wakili Kongola alidai DPP
amewasilisha hati hiyo kuwafutia mashitaka washitakiwa 10 kati ya 12, kwa
kupitia kifungu cha 91(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai (CPA).
Kongola aliwataja washitakiwa, ambao
DPP amewasilisha hati ya kuwafutia mashitaka kuwa ni mhandisi wa jengo hilo,
Goodluck Mmbanga, Mkaguzi wa jengo, Willbrod Mugyabuso na aliyekuwa diwani wa
kata ya Goba, Ibrahim Kissoky, ambaye ni mfanyabiashara, anayemiliki Kampuni ya
Lucky Construction ya Dar es Salaam, iliyojenga jengo hilo.
Wengine ni Mhandisi wa Manispaa ya
Ilala Charles Ogare, Mhandisi Mshauri, Zonazea Oushoudada, anayemiliki Kampuni
ya Sou Consultancy Co. Ltd, ambayo ilikuwa ikisimamia ujenzi wa jengo hilo,
Msanifu Majengo, Vedasto Nzikoruhale na Mwandaaji Michoro ya Majengo Michael
Hema, Msajili Msaidizi wa Bodi ya Wasanifu na Wakadiriaji Majenzi (AQRB),
Albert Mnuo na Ofisa Mtekelezaji Mkuu wa AQRB, Joseph Ringo.
Kongola alidai washitakiwa waliobaki
taarifa zimefailiwa kwenda Mahakama Kuu kwa ajili ya taratibu za kuwasomea
maelezo ya mashitaka.
Baada ya kueleza hayo, Hakimu Dk.
Yongolo alisema kwa mujibu wa maombi ya upande wa jamhuri, watuhumiwa
walioorodheshwa katika hati ya kufutiwa mashitaka ya DPP, isipokuwa washitakiwa
wawili, wameachiliwa huru kama ilivyoombwa.
Hakimu Dk. Yongolo aliwaeleza
washitakiwa waliofutiwa mashitaka kwamba, kwa masharti ya kifungu kilichotumika
kuwafutia mashitaka, hakiwazuii upande wa jamhuri kuwakamata na kuwafungulia
mashitaka kama hayo.
Baada ya kusema hayo, Hakimu Dk.
Yongolo aliwaachia huru washitakiwa hao 10 na kuahirisha kesi kwa washitakiwa
wawili waliobaki hadi Septemba 7, mwaka huu.
Washitakiwa hao wawili wanakabiliwa
na kesi ya kuwaua bila kukusudia watu 27,
ambapo wanadaiwa kutenda makosa hayo Machi 29, 2013, katika mtaa huo.
No comments:
Post a Comment