Friday 13 October 2017

KIBANO KWA WALIOFOJI UMRI CHAJA




SERIKALI baada ya kupata mafanikio makubwa katika uhakiki wa watumishi hewa na wenye vyeti vya kughushi, sasa inahamia kwa wale waliodanganya umri wa kuzaliwa ili wasistaafu mapema.
Imesema watumishi wa umma 40,000 nchini, wamedanganya umri wa kuzaliwa kwa kutoa taarifa tofauti kwa mwajiri na kwenye Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA).
Kubainika kwa watumishi hao, kunafuatiwa na tamko la Rais Dk.John Magufuli, alilolitoa Mei Mosi, mwaka huu, wakati wa maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniani, yaliyofanyika mkoani Moshi mkoani Kilimanjaro.
Dk. Magufuli, alisema baada ya kukamilika kwa uhakiki wa wafanyakazi hewa na wenye vyeti feki, kuwa kwa sasa wamejipanga kufanya uhakiki wa wafanyakazi waliobadilisha umri wao.
Alisema, kuna watu ambao ni wazee kwenye ofisi za umma, lakini hawataki kustaafu.
Alisema, mtu wa namna hiyo, hana tofauti na mfanyakazi hewa kwa sababu hataki kutoka kazini ili wengine nao waajiriwe.
Rais alisema, hao ambao hawataki kuachia ofisi, lakini ni wazee dawa yao inachunguzwa.
Akizungumzia kuhusu watumishi waliodanyanga umri baada ya kuulizwa wakati wa makabidhiano ya wizara kati yake mtangulizi wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angella Kairuki na Waziri mpya, George Mkuchika.
Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dk.  Laurean Ndumbaro, alisema kuna watumishi ambao walighushi umri wakati wanaajiriwa na walivyokwenda kwa ajili ya kupatiwa vitambulisho vya NIDA, walitaja umri mwingine tofauti na waliotaja serikalini.
“Sijui wamebadilisha kwenda kwenye umri halali au kwa kughushi, takribani watumishi wa umma 40,000 ambao taarifa zao katika mfumo wanaonekana umri wao wameubadilisha, katika miaka ya hivi karibuni,” alisema.
Alisema, serikani walijaza umri ambao sio sahihi ambapo NIDA walijaza umri sahihi,”alisema.
Dk. Ndumbaro, alisema walipokwenda NIDA kulinganisha taarifa zao ambao zipo kwenye mfumo, walibaini kuna baadhi yao wana umri wa aina mbili tofauti.
Kwa mujibu wa Dk. Ndumbaro, wanaendelea kusoma taarifa zao na ni wengi waliobadilisha umri.
Alisema taarifa hizo wanazo na wanazifanyia kazi kadiri muda itakavyokwenda ili watumishi hao waweze kurekebisha umri wao na kubakia na ule ambao ni halali.
Kwa upande wake, Angellah ambaye ni Waziri wa Madini, alisema katika wizara hiyo alikumbana na changamoto mbalimbali ikiwemo uhakiki wa vyeti ambapo kazi yake haikuwa nyepesi.
Waziri huyo alisema kuna maofisa utumishi wengine hawakuwa waaminifu katika mchakato huo, walidiriki kuwasaidia watu kuficha sifa zao.
“Naamini kama wapo masalia na kwa timu iliyopo itafanyiwa kazi na wataondolewa,”alisema.
Kuhusu maslahi ya watumishi wa umma, Angellah alisema  kuna idadi  kubwa ikilinganishwa na mapato yanayopatikana serikali.
Alisema katika mwaka wa fedha, zimetengwa fedha kwa ajili ya kuwapandisha watumishi 193,666 katika madaraja na kinachosubiriwa ni utekelezaji wake.
Naye, Mkuchika alimpongeza waziri mwenzake kwa kazi kubwa aliyoifanya katika wizara hiyo na kusema huo ni mtaji na amemrahisishia sehemu ya kuanza na kupita.
“Umeeleza kulikuwa na operesheni ya kuwaondoa watumishi hewa na umefanya kazi kubwa ya kujua idadi  hasa ya watumishi waliopo.
“Nafikiri ni busara ya Rais, kabla ya kuwapandisha watu vyeo na mishahara, je watu hao wapo na ni watumishi halali, kazi hiyo wewe umeifanya.
“Sasa ni muda muafaka tutakaka na kuangalia jambo hilo, baada ya kujiridhisha, msingi tayari umewekwa na kufanikiwa kuwaondoa na kurejesha nidhamu ya watumishi na mambo mengine,”alisema.
Mkuchika alisema zamani watu walikuwa na heshima ukiambiwa kuwa wewe ni mtumishi wa serikali kuliko mtumishi mwingine katika taasisi binafsi na walitambulika kutokana na nidhamu waliyokuwa nayo.
Waziri huyo alisema wataendeleza pale alipoishia na zaidi ni kuongeza kasi ya kufanya kazi kwa maadili ya utumishi wa umma na mapambano dhidhi ya rushwa.
Pia, Mkuchika aliiagiza sehemu zitazokuwa zinafanya   makongamano na semina, wataalamu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana (TAKUKURU), waalikwe kwa ajili ya kutoa  elimu kwa wananchi kuhusu masuala ya rushwa.
“Ukienda katika nchi zilizofanikiwa katika rushwa, Norway na Sweden, wananchi wanafahamu rushwa ni adui wa haki, hata muombaji wa rushwa anaogopa kwa sababu wanajua.
“Watanzania wangapi wanajua ni wachache, mtu anaombwa rushwa, sijui hospitalini, anatafuta vipimo, ukitaka vipimo vyake viende haraka lete kiasi fulani, anatoa masikini yule hana anaumia,”alisema.

No comments:

Post a Comment