Friday 13 October 2017

'NYERERE ALIASISI UZALENDO, UONGOZI BORA'




BAADHI ya Wasomi na Wanasiasa nchini, wamemwelezea Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, kwamba alikuwa kiongozi aliyeasisi uzalendo, misingi ya uongozi bora na uadilifu
Wamesema misingi hiyo, haijawahi kutekelezwa kikamilifu kwa vitendo na yeyote, isipokuwa Rais Dk. John Magufuli.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha, akifungua kongamano la maadhimisho ya Kumbukizi ya Mwalimu Nyerere, Dar es Salaam, jana, alisema kumekuwa na mmomonyoko wa maadili kwenye jamii.
“Rais Magufuli amerejesha kwa kiasi kikubwa nidhamu katika misingi aliyoiweka Mwalimu Nyerere, hivyo ni wajibu wa kila mmoja katika nafasi yake, kumuunga mkono,” alisema.
Maadhimisho hayo, yalifanyika katika Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Kigamboni, naibu waziri huyo alikipongeza chuo hicho kwa kurejesha mitaala ya mafunzo ya uongozi, maadili na utawala bora.
“Chuo kinayo nafasi nzuri ya kutoa viongozi wengi waadilifu katika misingi aliyoiasisi Mwalimu Nyerere, hivyo endeleeni kutoa mafunzo kwa viongozi wa vyama mbalimbali vya siasa, watakaosimamia uzalendo,” alisema.
Vile vile, aliitaka jamii kuhakikisha inawaokoa watoto kutoka katika wimbi la mitandao ya kijamii ambamo wanajifunza mambo yasiyofaa, badala yake watafiti, kusoma na kufuata misingi ya Baba wa Taifa.
Alisema, anaamini ikiwekwa mikakati imara, vijana watapata malezi na makuzi ya kimaadili, baadaye kushika uongozi katika ngazi za juu.
Alihimiza kuunga mkono sera ya kukuza uchumi wa viwanda kwa kuwa Mwalimu Nyerere alihimiza kuendeleza viwanda vya ndani ikiwa ni njia ya kujinasua na mabepari.
Akitoa mada, Mzee Samuel Kasori,  alisema  Mwalimu Nyerere alihimiza matumizi mazuri ya raslimali, masoko ikiwemo kutumia wataalamu kuondoa umasikini.
“Lakini baada ya kuondoka, watu wanafanya mambo ya hovyo kila mtu anavyojisikia ili kujinufaisha, leo nawatia moyo Watanzania watekeleze nia ya rais Magufuli kwani ndiye anayeendeleza misingi hiyo,” alisema.
Alisema, inapaswa kuwekwa sera nzuri ya ardhi, kwa kuwa mwaka 1958, kabla ya Uhuruardhi isichezewe kwa kuwa ni mali ya Watanzania wote.
“Uzalendo, uadilifu na utaifa si kuvaa nembo au kupamba bendera ofisini kwenye magari na nyumbani huku mnafanya uozo, dhuluma na hujuma kwa Watanzania wenzenu, bali ni kutekeleza kwa vitendo,” alisema.
Mzee Kasori alinukuu kauli iliyosemwa na Mwalimu Nyerere mwaka 1959 kuwa Afrika inaonewa kwa kufanywa bara la kuuzwa nje, kutokana na kunyonywa.
Msajili wa Hazina, Dk. Oswald Mashindano, akitoa mada alisema Rais Magufuli anatekeleza ajenda ya uchumi wa viwanda iliyoasisiwa na Mwalimu Nyerere, dhamira ilikuwa kulifanya taifa lijitegemee kiuchumi.
Alisisitiza kuchunguza changamoto zilizoangusha viwanda vya awali, ili kuziepuka na taifa kusonga mbele.
Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo hicho, Profesa Mark Mwandosya, alisema wanayo kazi kubwa ya kuhakikisha wanarudisha misingi iliyowekwa na Baba awa Taifa, kwa kuwa misingi yake ina umuhimu hususan kipindi hiki cha awamu ya tano.
Spika wa Bunge Mstaafu, Anne Makinda, alisema ukweli utabaki pale pale kuwa misingi aliyoiweka Baba wa Taifa inafaa na kuopaswa kurithishwa kwa vizazi vyote.
Anasema Nyerere alikuwa kama mtabiri kwani yote aliyoyasema ndiyo tunayohangaika nayo hivi sasa, hivyo si ya kupuuzwa.
Kaimu Mkuu wa chuo hicho, Profesa Shedrack anasema watahakikishja wanapika viongozi watakaowafikisha Watanzania wanapopataka.

No comments:

Post a Comment